2014-11-25 10:32:54

Ebola bado ni tishio!


Mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ebola Barani Afrika bado hayajafanikiwa kupata ushindi unaotarajiwa, mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kusaidia kuchangia kwa hali na mali katika mchakato wa mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ebola ambao kwa sasa ni tishio kubwa la maisha, ustawi na maendeleo ya watu wengi duniani.

Ni kilio kilichotolewa hivi karibuni na Bwana Anthony Banbury, Mratibu wa ugonjwa wa Ebola kutoka Umoja wa Mataifa, alipokuwa anazungumza na wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, katika kikao chake kilichokuwa kinafanyika mjini New York. Taarifa za Shirika la Afya Duniani zinaonesha kwamba, kuna watu zaidi ya 5, 459 na watu wengine 15, 351 wameambukizwa ugonjwa wa Ebola. Hali bado ni mbaya nchini Guinea, Liberia na Sierra Leone.

Nigeria imeondolewa kwenye orodha ya nchi zenye ugonjwa wa Ebola. Mali na Senegal bado zinaangaliwa kwa tahadhari zaidi. Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon anazitaka nchi mbali mbali ambazo zina wagonjwa wa Ebola kujifunza kuwa makini zaidi kutoka katika nchi ambazo zimeathirika kutokana na ugonjwa huu, ili kuokoa maisha ya watu.

Wagonjwa wapewe huduma muhimu zinazohitajika sanjari na kudhibiti kuenea kwa ugonjwa wa Ebola kwa watu wengine. Na habari zaidi zinasema kwamba, Italia, Jumanne, imepokea mgonjwa wa kwanza wa Ebola, Daktari aliyekuwa anafanya kazi ya kutibu wa wagonjwa wa Ebola nchini Sierra Leone.







All the contents on this site are copyrighted ©.