Ushirikiano, maendeleo na uhamiaji ni chanda na pete!
Kumekuwepo na ushirikiano mkubwa miongoni mwa Makanisa katika kuwahudumia wahamiaji
na wakimbizi kutoka sehemu mbali mbali za dunia kwani uhamiaji ni dhana ambayo inajengeka
katika matumaini ya maisha bora zaidi, ingawa mara nyingi imekumbana na majanga makubwa.
Wahamiaji wanabeba ndani mwao utajiri mkubwa wa maisha ya kiroho na kitamaduni;
kwa matumaini ya kuweza kuchangia katika ustawi na maendeleo ya wengi; maisha, utu
na heshima yao kama binadamu vinapaswa kuheshimiwa. Kuna sababu nyingi ambazo zinapelekea
watu kuzikimbia nchi zao pamoja na kutambua madhara wanayoweza kukumbana nayo njiani.
Hayo yamesemwa na Baba Mtakatifu Francisko Ijuamaa, tarehe 21 Novemba 2014,
wakati alipokutana na kuzungumza na wajumbe wa Kongamano la Saba la Kimataifa la shughuli
za kichungaji kwa wahamiaji, ambao wanachambua vyanzo na sababu kuu zinazopelekea
watu kuzikimbia nchi zao: ukosefu wa usawa kati ya watu; umaskini, ongezeko la idadi
ya watu, upungufu wa fursa za ajira, majanga asilia, vita, dhuluma na nyanyaso za
kidini. Lakini ushirikiano katika mchakato wa maendeleo unaweza kuleta mabadiliko
makubwa katika maisha ya watu, kwa kuchangia maendeleo pamoja na kuziba pengo linalosababishwa
na upungufu wa idadi ya watu katika baadhi ya maeneo. Ushirikiano huu ni muhimu katika
maboresho ya maisha ya wahamiaji na familia zao na katika nchi walikotoka.
Baba
Mtakatifu anakiri kwamba, wakati mwingine, nchi husika hupoteza watalaam waliofundwa
wakafundika. Watoto wanapata malezi tenge, kwa kukuzwa na mzazi mmoja, jambo ambalo
ni hatari kwa ustawi na maendeleo ya watoto; kuvunjika kwa ndoa. Nchi wahisani wakati
mwingine zinakabiliwa na changamoto kubwa ya kuwapokea, kuwahifadhi na kuwaingiza
wahamiaji katika uhalisia wa maisha ya wenyeji wao kutokana na utofauti mkubwa wa
kijamii na kitamaduni.
Kutokana na changamoto zote hizi, wafanyakazi wanaowahudumia
wahamiaji na wakimbizi wana mchango mkubwa katika mchakato wa majadiliano, mapokezi,
sheria na uwakilishi. Madhara ni makubwa zaidi kwa familia na vijana katika nchi walimotoka.
Baba
Mtakatifu anasema kuna uhusiano mkubwa kati ya ushirikiano, maendeleo na wahamiaji,
changamoto kwa Kanisa kuendelea kuwaonjesha ukarimu wahamiaji sanjari na kuwashirikisha
karama mbali mbali ambazo wamekirimiwa na Mwenyezi Mungu, lakini zaidi zawadi ya imani,
kwa kuwaingiza katika mpango wa Uinjilishaji mpya sanjari na kuwasindikiza wahamiaji
katika hija ya maisha yao, hadi watakapofikia mwisho wa safari yao. Lengo ni kuhakikisha
kwamba, wahamiaji wanahudumiwa kikamilifu katika maisha yao ya kiroho kwa njia ya
Katekesi, Liturujia na Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa.
Baba Mtakatifu
anasikitika kusema kwamba, wahamiaji wanaishi katika mazingira magumu, duni na pweke,
kiasi hata kushindwa kupokelewa na wenyeji wao. Kanisa halina budi kuwa ni mahali
pa matumaini, katika kulinda na kutetea haki msingi za wahamiaji; kwa kuwapatia msaada
bila ubaguzi kwa kutambua karama walizo nazo wahamiaji badala ya kuangalia tu matatizo
na changamoto wanazoleta katika nchi wahisani, mwaliko wa kuwashirikisha katika uhalisia
wa maisha ya wenyeji wao. Ndani ya Kanisa hakuna mgeni, kila mtu anapaswa kukaribishwa
na kusaidiwa.
Licha ya Kanisa kuwa ni Jumuiya ya Waamini, lakini waamini wanamtambua
Yesu katika sura ya jirani zao na Mama alisiyekuwa na mipaka, anayewatamadunisha na
kuwapokea wote, ili kuwaonjesha mshikamano wa upendo, kwani kila mtu anathamani kubwa
machoni pa Mungu, kwani wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, kumbe utu na heshima
yao vinapaswa kulindwa na kudumishwa.
Wahamiaji kama binadamu, wenye tunu
msingi za maisha ya kitamaduni wanakuza udugu kati ya watu, changamoto ya kung'oa
kabisa mambo yanayosababisha ukosefu wa usawa, haki na udhalimu, ili kujenga utambulisho
mpana zaidi na wenyeji wao, ili kukoleza mchakato wa maendeleo unaojikita katika kipaji
cha ugunduzi na heshima kwa utu wa wote.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.