2014-11-21 08:54:32

Umoja kamili miongoni mwa Wakristo ni kipaumbele cha kwanza kwa Kanisa Katoliki


Kuanzia tarehe 18 hadi tarehe 21 Novemba 2014, Baraza la Kipapa linalohamasisha umoja wa Wakristo linafanya mkutano wake wa mwaka sanjari na maadhimishoya Jubilee ya miaka 50 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha hati inayokazia majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Wakristo, inayojulikana kwa lugha ya Kilatini, Unitatis redintegratio.

Baba Mtakatifu katika ujumbe wake kwa washiriki wa mkutano huu, anasema, Kanisa lina kila sababu ya kummshukuru Mungu kwani changamoto ya majadiliano ya kiekumene imepokelewa na Makanisa mengi na kwamba, katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, imekuwa ni kikolezo cha majadiliano ya kiekumene yanayojikita katika Maandiko Matakatifu na Mapokeo ya Kanisa.

Makanisa mbali mbali yamepembua kwa kina na mapana na kwamba, chuki na uhasama uliosababisha madonda makubwa miongoni mwa Wakristo ni kurasa chungu zilizopitwa na wakati, sasa Wakristo wanaendelea kushikamana kwa dhati, huku wakitambuana kuwa ni ndugu, umoja unaofumbatwa kutoka katika Sakramenti ya Ubatizo.

Wakristo wamepata mabadiliko makubwa ya mwelekeo na mawazo, dhana ambayo imesambazwa pia hata katika mikakati ya maisha ya shughuli za kichungaji katika Makanisa mahalia, kwa kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea umoja wa Kanisa, ili wote wawe wamoja! Hata hivyo, bado kuna haja kwa Makanisa kuendelea kutafuta njia nyingine zaidi za ushirikiano kwani hadi sasa kumekuwepo na tafsiri ya Biblia Takatifu kwa pamoja; huduma za kijamii pamoja na kusimama kidete kulinda na kutetea maisha, utu na heshima ya binadamu; kulinda na kutunza mazingira pamoja na kupambana na mambo yote yanayotatiza haki msingi za binadamu.

Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kielelezo cha upendo wa Kanisa. Baba Mtakatifu anapenda kuchukua fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza wale wote waliojibidisha kujenga na kukuza huduma ya upatanisho, umoja na mshikamano miongoni mwa wakristo, lakini zaidi wale walioshirikiana kwa karibu zaidi na Baraza la Kipapa la kuhamasisha umoja wa Wakristo.

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, bado kuna utengano ndani ya Kanisa unaosababishwa na tema za kibinadamu na kimaadili; mambo yanayogumisha hija ya umoja kamili, lakini hakuna haja ya kukata tamaa, bali kuendelea kumtumainia Mwenyezi Mungu, anayepandikiza mbegu ya upendo na umoja, ili kukabiliana na changamoto za kiekumene katika ulimwengu mamboleo. Hapa kuna haja ya kujenga na kukuza majadiliano ya kiekumene yanayosimikwa katika maisha ya kiroho kwa kuthamini uekumene wa damu na kutembea katika njia ya Injili.

Uekumene wa maisha ya kiroho kilele chake ni juma la kuombea umoja wa Kanisa, dhamana inayotekelezwa katika ngazi mbali mbali za maisha na utume wa Kanisa, ili kujenga upendo na umoja kwa njia ya tafakari ya Neno la Mungu. Mitandao ya kijamii iwasaidie Wakristo kufahamiana zaidi. Wakristo waendelee kuthamini Uekumene wa damu, kwa Wakristo walioyamimina maisha yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, mbegu ya ushuhuda wa maisha yao, ulete toba na wongofu wa ndani, ili kukuza na kudumisha udugu, kwani dhuluma na nyanyaso za kidini haziwabagui Wakristo kwa madhehebu yao.

Baba Mtakatifu anasema, kuna hamu kubwa mioyoni mwa watu kutembea, kusali, kufahamiana na kumpenda Kristo kwa pamoja sanjari na kuendelea kushirikiana na kujenga mshikamano kwa ajili ya huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Hii ni hija ya pamoja inayotekelezwa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Umoja kamili ni changamoto endelevu inayopewa kipaumbele cha kwanza na Kanisa Katoliki, kwa kutambua kwamba, umoja ni zawadi kutoka katika Fumbo la Utatu Mtakatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.