2014-11-21 08:58:42

Siku ya wavuvi duniani na changamoto zake!


Sekta ya uvuvi duniani inakabiliwa na changamoto nyingi kiasi kwamba, wavuvi wenyewe hawaridhiki na mafanikio yanayopatikana kutokana na jitihada wanazofanya kila siku. Hili ni kundi la watu linalotumia muda wake mwingi kwa ajili ya kazi, kiasi kwamba, hata wakati mwingine wanakosa muda wa kukaa pamoja na familia zao. Ni kundi ambalo, halijapewa kipaumbele cha pekee katika shughuli na mikakati ya kichungaji na Makanisa mahalia.

Hii ni sehemu ya ujumbe kutoka kwa Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum katika maadhimisho ya Siku ya Wavuvi Duniani, inayofanyika kila mwaka ifikapo tarehe 21 Novemba. Sekta ya utume wa bahari, inakumbusha kwamba, sekta ya uvuvi inatoa ajira kwa watu zaidi ya millioni 58.3, kati yao asilimia 37% wana ajira ya kudumu, changamoto kwa Makanisa mahalia kuhakikisha kwamba, yanawashughulikia wavuvi katika mikakati yao ya shughuli za kichungaji, bila kuwatenga.

Sekta ya uvuvi ni kati ya kazi zenye hatari kubwa duniani, kwani kuna maelfu ya watu wanakufa maji baharini kila mwaka na wengine kupata vilema vya kudumu wakiwa kazini. Wavuvi ni watu ambao wananyonywa na kudhulumiwa kwa urahisi sana na wakati mwingine wamekuwa ni wahanga wa biashara haramu ya binadamu na kazi za sulubu, kama ambavyo inajionesha kwenye taarifa za vyiombo vya habari.

Ikiwa kama nchi mbali mbali duniani zitaweza kuridhia mkataba wa Shirika la Kazi Duniani, ILO wa Mwaka 2007, matatizo haya yanaweza kupewa ufumbuzi wa kudumu na wavuvi wakaanza kutekeleza wajibu wao katika mazingira bora zaidi. Itifaki inapania pamoja na mambo mengine ni kuhakikisha kwamba, wavuvi wanakuwa na maisha bora zaidi wanapokuwa kazini, wawe na makazi, huduma bora za afya, chakula bora na usalama kazini. Utume wa Bahari kwenye Makanisa mahalia unapaswa kusaidia kuhamasisha Serikali katika nchi husika kuridhia Itifaki hii.

Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa linabainisha kwamba, kuna uvuvi wa kupindukia, kiasi cha kuhatarisha kutoweka kwa baadhi ya samaki. Uvuvi haramu umepelekea kuharibu mazalia ya Samaki, hali ambayo inachangiwa pia na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na uchafuzi wa mazingira. Lakini ikumbukwe kwamba, sekta ya uvuvi inachangia kwa kiasi kikubwa katika ustawi na maendeleo ya binadamu. Hapa uvuvi unapaswa kuheshimu mazingira.







All the contents on this site are copyrighted ©.