2014-11-20 11:52:20

Sikilizeni kilio cha watu wanaokufa kwa baa la njaa na lishe duni, ili kuokoa maisha yao!


Jumuiya ya Kimataifa haina budi kujenga umoja na mshikamano, ili kuibua mbinu mkakati utakaosaidia kupambana na baa la njaa na utapiamlo wa kutisha sanjari na mabadiliko ya tabianchi na kwamba, Kanisa kwa upande wake, linapania kumletea mwanadamu ustawi na maendeleo endelevu, yanayogusa maisha ya mtu mzima: kiroho na kimwili, lakini kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukimizwa pembezoni mwa jamii, ili usalama na utu wao viweze kulindwa.

Watu wanapaswa kutegemeana kama familia, lakini ukweli wa mambo ni kwamba, kinzani za kiuchumi zimekuwa ni kitovu cha misigano inayohatarisha urafiki wa kidugu, hali inayopelekea baadhi ya watu kutothaminiwa na hatimaye, kutengwa; mambo yanayowatendea watu wasiokuwa na fursa za ajira au wale wanaoteseka kutokana na baa la njaa. Hapa kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kushikamana, ili kupambana na baa la njaa na lishe duni, kwa kutambua haki ya mtu kupata lishe bora.

Hii ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko Alhamisi, tarehe 20 Novemba 2014 kwa wajumbe wa Jumuiya ya Kimataifa wanaoshiriki katika mkutano mkuu wa pili wa kimataifa unaojadili mikakati ya kupambana na baa la njaa pamoja na lishe duni, ulioandaliwa na Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani, WHO. Watu wengi leo hii wanazungumzia kuhusu haki, lakini haki ya mtu kupata chakula inahodhiwa na nguvu ya soko na faida kubwa, wakati mamillioni ya watu wanaendelea kufariki dunia kutokana na baa la njaa; hili ni kundi ambalo utu wake unahitaji kuheshimiwa.

Baba Mtakatifu anasema mbinu mkakati unaoibuliwa na Jumuiya ya Kimataifa wakati mwingine unaweza kubaki kama nadharia, lakini watu wanahitaji kuona haki ikitendeka, kwa kutambua mahitaji msingi ya binadamu; kwa kuheshimu na kuthamini haki za wale wanaoteseka kwa baa la njaa na lishe duni, kwa kutekeleza haya, Jumuiya ya Kimataifa itaweza kupata mafanikio makubwa katika utoaji wa misaada na utekelezaji wa mikakati ya maendeleo endelevu.

Uzalishaji, upatikanaji wa chakula, mabadiliko ya tabianchi na soko la mazao ya kilimo ni mambo yanayopaswa kuongozwa na kanuni za kitaaluma, lakini, binadamu na mahitaji yake msingi anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza. Kuna chakula kingi kinachozalishwa ambacho kinaweza kutosheleza mahitaji ya watu duniani kama alivyowahi kusema Mtakatifu Yohane Paulo II, lakini bado kuna kiasi kikubwa cha chakula kinaharibika na kutupwa wakati kuna mamillioni ya watu wanakufa kwa baa la njaa na lishe duni.

Baba Mtakatifu anasema, haya ni matokeo ya kuchakachuliwa kwa taarifa na takwimu muhimu; usalama wa taifa, rushwa na ufisadi na mbaya zaidi, ni madhara ya myumbo wa uchumi kimataifa. Hii ni changamoto ya kwanza ambayo Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuipatia ufumbuzi wa kudumu katika mapambano ya baa la njaa duniani.

Ukosefu wa mshikamano ni changamoto ya pili inayopaswa kufanyiwa kazi kwa kufisha ubinafsi na migawanyiko, mambo yanayowaathiri wanyonge kiasi hata cha watu hawa kuchukia Serikali zao. Mshikamano ni mchakato unaowawezesha watu kukutana na kusaidiana kwa hali na mali; kwa kujenga mahusiano bora, wote wakidhamiria kutafuta mafao ya wengi.

Binadamu wanapaswa kutambua kwamba, wao wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kuwa wanawajibika fika kulinda na kutunza mazingira, changamoto ya kushikamana kwa dhati badala ya kupigana; mambo yanayoitumbukiza dunia katika umaskini. Mwenyezi Mungu anaweza kumsamehe binadamu kutokana na dhambi zake, lakini, dunia kamwe haiwezi kumsamehe mwanadamu, atalipa hadi senti ya mwisho!

Serikali zitambue kwamba, ni mkusanyiko wa Jumuiya ya Watu, zinazopaswa kusaidiana, kwa kuzingatia sheria na kanuni za kimataifa, huku zikiongozwa na sheria asilia ambayo inaweza kueleweka na wengi kwani inazungumza lugha ya: upendo, haki, amani, mambo msingi yanayokumbatiana. Kama ilivyo kwa binadamu, Serikali na Mashirika ya kimataifa hayana budi kujenga moyo wa majadiliano na utamaduni wa kusikilizana na kwa njia hii, lengo la kufuta baa la njaa na utapiamlo duniani linaweza kufikiwa!

Serikali hazina budi kutekeleza wajibu wake kwa kutafuta na kulinda mafao ya raia wake bila ya kujibakiza hata kidogo, jambo linalohitaji utekelezaji na udumifu. Kanisa Katoliki linaendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya watu kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kwa kushirikiana na Jumuiya na Mashirika ya Kimataifa, ili kusaidia mchakato wa mikakati ya maendeleo inayozingatia usawa na kanuni msingi kama vile: ukweli, uhuru, haki na mshikamano pamoja na kutambua haki ya chakula, uhai na maisha bora zaidi; ni haki ya kulindwa kwa mujibu wa sheria na kwamba, ni sheria maadili ili kuweza kushirikishana utajiri wa uchumi wa dunia.

Baba Mtakatifu anasema kwa wale wanaoamini kwamba, umoja wa Familia ya binadamu unapata chimbuko lake kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Muumbaji na udugu miongoni mwa binadamu; hakuna maelezo yoyote yale ya kiuchumi na kisiasa yanayoweza kukubalika kwa kuona watu wanakufa kwa baa la njaa na lishe duni.

Mfumo wa kibaguzi kwa hali na haki hauna budi kuwekwa pembeni katika soko la chakula duniani na kamwe usiwe ni mfano wa mikakati katika kupambana na baa la njaa duniani. Baba Mtakatifu anawasihi viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kusikiliza kilio cha watu wanaokufa kwa baa la njaa na lishe duni, ili kutoa chakula kitakachosaidia kuokoa maisha ya watu wengi duniani.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.