2014-11-20 07:53:38

Caritas Afrika katika kupambana na majanga asilia!


Shirika la Misaada Barani Afrika, Caritas Africa, hivi karibuni lilifanya mkutano wake mkuu mjini Kampala, Uganda ili kuangalia pamoja na mambo mengine, taarifa ya kikosi kazi katika kupambana na majanga mbali mbali Barani Afrika. Wajumbe walipata nafasi ya kusikiliza taarifa ya shughuli za "Caritas Africa" kutoka katika nchi mbali mbali pamoja na kuangalia mwongozo wa utendaji wa shughuli zake. RealAudioMP3

Wajumbe walipitia mapendekezo ya mwongozo wa shughuli za "Caritas Africa" na kwamba, wajumbe watapewa mwongozo rasmi baada ya marekebisho yaliyofanywa mwishoni mwa mwezi Agosti, 2014. Caritas Africa imeangalia pia majanga mbali mbali yanayoendelea kujitokeza ndani na nje ya Bara la Afrika na kwamba, Bara la Afrika halina budi kuweka kanuni maadili, viwango vya uwajibikaji, ubora wa vifaa vya utekelezaji wa majukumu yaliyopo pamoja na kufanya tathmini ya utekelezaji wa mikakati ya Caritas katika nchi husika.

Wajumbe walionesha masikitiko yao makubwa kutokana na uwajibikaji wa "Caritas Africa" katika kuzisaidia nchi wanachama. Kati ya sababu zilizotolewa ni pamoja na ukata na ukosefu wa rasilimali fedha; baadhi ya viongozi wa Caritas katika nchi husika kutowajibika barabara kwa kuwa wakweli na wa wazi katika matumizi ya fedha za misaada pamoja na ukweli kuwa rasilimali iliyopo ni kidogo, ikilinganishwa na mahitaji makubwa yanayotolewa na nchi wanachama wa "Caritas Africa". Nchi na wafadhili mbali mbali wa "Caritas Africa" wamepunguza msaada wao kwa kiasi kikubwa Barani Afrika kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Pamoja na mapungufu haya, wajumbe wameamua kuimarisha mawasiliano, maamuzi, uwajibikaji pamoja na kuonesha thamani ya fedha halisi inayotakiwa katika kukabiliana na majanga. "Caritas Africa" inazihamasisha nchi wanachama kuchangia kwa hali na mali katika kupambana na majanga mbali mbali badala ya mtindo wa sasa kusubiri msaada kutoka kwa nchi na wafadhili mbali mbali.

Barani Afrika kuna nchi ambazo bado zinahitaji masaada wa dharura ili kuwasaidia watu waliolazimika kuyakimbikia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Jamhuri ya Afrika ya Kati, Mali, Niger, Chad, Cameroon na Nigeria ni kati ya nchi ambazo zinakabiliwa na mashambulizi ya kigaidi yanayofanywa na Kikundi cha Boko Haram. Namibia kwa sasa inakabiliwa na ukame wa muda mrefu ambao unahitaji msaada wa dharura. DRC licha ya vita, Caritas inaendelea kuwahudumia wahamiaji na wakimbizi wanaorudi nchini humo. Sudan ya Kusini ni kati ya nchi ambazo pia zinahitaji msaada wa dharura.

Wajumbe wa "Caritas Africa" wanaendelea kuhamasishwa kuhakikisha kwamba, wanashirikiana wao kwa wao pamoja na kujenga mtandao mkubwa zaidi wa mahusiano na mashirika ya misaada, ili kuwasaidia watu wanaohitaji msaada wa dharura.








All the contents on this site are copyrighted ©.