2014-11-19 11:11:54

Uchaguzi mkuu nchini Nigeria mwaka 2015 unaweza kusababisha majanga!


Askofu mkuu Ignatius Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria anasema kwamba, mchakato wa uchaguzi mkuu nchini humo unaotarajiwa kufanyika mwaka 2015 unaweza kuandamwa na matukio ya umwagaji damu kwa watu wasiokuwa na hatia kutokana na watu kupania kushika madaraka kwa udi na uvumba! Inasikitisha kuona kwamba, viongozi wa kisiasa wamesahau wajibu wa kulinda na kutetea amani, ustawi na maendeleo ya watu wao, na badala yake wameanza kugombania madaraka.

Askofu mkuu Kaigama ameyasema haya hivi karibuni wakati wa mkesha wa kuombea amani, umoja na upatanisho wa kitaifa kutokana na vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na Kikundi cha Boko Haram kuendelea kukithiri siku hadi siku, kiasi cha kuwakatisha watu tamaa ya kuishi. Mauaji yanaongezeka na Boko Haram inaendelea kujitanua kwa kuteka na kukalia miji mingi zaidi, mambo yanayoonesha udhaifu mkubwa wa Serikali katika kupambana na Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram, ambacho kwa sasa kimekuwa nguzo yao kisiasa.

Kanisa Katoliki litaendelea kukemea na kulaani vitendo vya kigaidi kwani limeathirika vibaya sana kutokana na mashambulizi yanayofanywa na vikosi hivi. Kuna watu wanaolazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha yao, lakini hata katika shida na mahangaiko haya, Maaskofu wameendelea kuwa bega kwa bega na waamini wao kwa kuwapatia faraja na matumaini mpaya; wameendelea kutoa huduma kwa wananchi wote wa Nigeria bila ubaguzi wa kidini au itikadi ya watu.







All the contents on this site are copyrighted ©.