"Tunahitaji mbinu mkakati na mipango kazi ili kupambana na baa la njaa na utapiamlo"
Dr. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jumanne
tarehe 18 Novemba 2014 amekutana na kuzungumza na watanzania wanaoishi nchini Italia.
Amepongeza
juhudi zinazofanywa na watanzania katika kujenga na kudumisha umoja na mshikamano
wa kitaifa wanapokuwa ughaibuni kwa kukuza utaifa wao na kuendeleza lugha ya Kiswahili
licha ya maendeleo makubwa ya sayansi ya mawasiliano ya jamii, ambayo kwa sasa inawafanya
watu wengi kutopenda kushikamana na wengine kwa kujikita katika ubinafsi.
Kwa
ufupi amejibu changamoto mbali mbali zilizotolewa na Jumuiya ya Watanzania wanaoishi
nchini Italia katika risala iliyosomwa kwa niaba yao na Bwana Kagutta Nsangu Maulidi.
Amesema kwamba, Serikali inaendelea kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao
kwa kufumua mtandao wa kigaidi uliokuwa umeanza kusababisha hofu kubwa miongoni mwa
watanzania kutokana na milipuko ya mabomu iliyokuwa inasikika mara kwa mara, mambo
ambayo ni mageni sana kwa watanzania walio wengi, Jamii iliyozoea kuishi kwa amani
na utulivu. Amewataka watanzania, kuvumiliana, kuheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana,
ili amani na utulivu viendelee kuimarika zaidi na zaidi.
Serikali inaendelea
pia kusuluisha migogoro kati ya wakulima na wafugaji, ili amani na utulivu viweze
kurejea tena kwa kuzingatia misingi ya utawala wa sheria, dhana iliyofafanuliwa kwa
kina na mapana na Dr. Titus Malengeya Kamani, Waziri wa maendeleo ya mifugo na uvuvi
nchini Tanzania.
Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Makamu wa Rais ambaye
pamoja na ujumbe wake wanashiriki mkutano wa Lishe na Chakula ulioandaliwa na Shirika
la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO mjini Roma amebainisha kwamba, mkutano
huu unafanyika takribani baada ya miaka ishirini na miwili, tangu mkutano wa kwanza
ulipofanyika. Ni mkutano unaopania pamoja na mambo mengine kubainisha mbinu na mikakati
madhubuti ya kupambana na baa la njaa na utapiamlo wa kutisha unakwamisha makuzi ya
watoto wadogo wenye umri chini ya miaka mitano.
Upatikanaji wa lishe bora utasaidia
kupambana na magonjwa yanayosababisha vifo kwa wanawake wajawazito wakati wa kujifungua
pamoja na kuimarisha afya za watoto. Wajumbe wa mkutano hawana budi kufanya kazi kwa
kushirikiana, ili maamuzi yatakayofikiwa yasaidie kupambana na baa la njaa na utapiamlo
wa kutisha.
Hapa kuna haja anasema Makamu wa Rais kuwa na mikakati na mipango
kazi ya utekelezaji wa maazimio haya. Ni aibu kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa baa la
njaa na utapiamlo kuendelea kuwanyanyasa watu, wakati ambako dunia inaweza kuzalisha
chakula cha kutosha, kiasi kwamba, hata kingine kinatupwa kwenye mashimo ya taka!
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.