Papa Francisko anatarajiwa kushiriki katika Maadhimisho ya Siku ya VIII ya Familia
Duniani, 2015 huko Philadelfia, USA.
Roho Mtakatifu amemkirimia kila mwamini karama tofauti ili kukamilishana, kwa ajili
ya mafao ya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa pamoja na kuendeleza maelewano
na utulivu yanayojikita katika kazi ya Uumbaji, kwa kutambua kwamba, Roho Mtakatifu
ndiye mhusika mkuu anayewezesha utulivu kupatikana.
Mkamilishano huu ndio msingi
thabiti kati ya Bwana na Bibi katika maisha ya ndoa na familia, mahali pa kwanza kabisa
ambapo mwanadamu anapata fursa ya kutambua karama za mtu binafsi na zile za jirani
yake na hivyo kuanza kujikita katika sanaa ya kuishi karama hizi kwa pamoja. Familia
ni mahali ambapo watu wengi wanapata fursa ya kujifunza tunu msingi za maisha pamoja
na kumwilisha karama mbali mbali katika mshikamano wa upendo.
Familia pia
ni mahali pa kinzani kati ya ubinafsi na mshikamano; kati akili na hulka; kati ya
malengo mpito na malengo ya muda mrefu. Familia ni mahali ambapo kinzani hizi zinaweza
kupatiwa ufumbuzi wa kudumu, kwa kuzingatia mkamilishano kati ya Bwana na Bibi, kila
mtu akijitahidi kuchangia katika kukuza na kudumisha ndoa pamoja na malezi ya watoto.
Huu
ni mchango uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu, tarehe 17 Novemba 2014
wakati alipokuwa anashiriki katika Kongamano lililoandaliwa na Baraza la Kipapa la
Mafundisho Tanzu ya Kanisa, kuhusu dhana ya Mkamilishano kati ya Bwana na Bibi, kila
mtu akichnagia kutoka katika hazina ya utajiri wake, uzuri na karama.
Baba
Mtakatifu Francisko anasema, nyakati hizi, Familia inakumbana na changamoto nyingi,
kwani watu wanaishi katika utamaduni wa mambo mpito, kiasi kwamba, watu hawaoni tena
ile thamani ya maisha ya ndoa; wakati mwingine kwa kupindisha kanuni maadili kwa kisingizio
cha uhuru wa mtu binafsi, lakini kimsingi hizi ni dalili za kumong'onyoka kwa tunu
msingi za maisha ya kiroho. Kushuka kwa utamaduni wa watu kufunga ndoa ni matokeo
pia ya umaskini, hali inayopelekea watu wengi kuteseka.
Kinzani za Familia
zimepekea kuibuka kwa tatizo kubwa la Ikolojia ya binadamu, kwani hata mazingira ya
maisha ya ndoa na familia yanapaswa kulindwa na kudumishwa, ingawa pengine hata Kanisa
limechelewa kuiona changamoto hii, mwaliko wa kuibua mbinu mkakati kwa ajili ya kuendeleza
utamaduni wa watu kufunga ndoa, ili kujenga jamii inayosimikwa katika msingi thabiti
wa mapendo ya dhati kati ya Bwana na Bibi, ili kuunda mazingira ya malezi na makuzi
kwa watoto wao, ndio maana Kanisa linahimiza umuhimu wa Sakramenti ya Ndoa.
Baba
Mtakatifu anawataka wajumbe hawa katika kongamano hili kuendelea kujadili kwa kina
na mapana kuhusu umuhimu wa Sakramenti ya Ndoa kama kielelezo cha mshikamano, uaminifu
na mapendo kamili yanayobubujika kutoka katika moyo wa binadamu. Vijana wafundwe kutambua
umuhimu wa Ndoa, ili waweze kutafuta upendo wa dhati na unaodumu, kwa kutambua kwamba,
familia inazama katika masuala ya kijamii na kitamaduni na wala si nadharia inayoelea
juu ya ombwe! Familia ina nguvu inayojitosheleza yenyewe!
Baba Mtakatifu anawahamisha
waamini na watu wote wenye mapenzi mema kulinda na kudumisha mahusiano ya upendo kati
ya Bwana na Bibi, kwa ajili ya mafao ya wengi, yanayojikita katika uzuri wa watu,
familia, jumuiya na jamii katika ujumla wake. Baba Mtakatifu anasema, panapomajaliwa,
kunako mwezi Septemba 2015 atakwenda huko Philadelphia, Marekani, ili kushiriki katika
maadhimisho ya Siku ya Nane ya Familia Duniani.