2014-11-17 14:47:54

Familia ni madhabahu ya Injili ya Uhai inapaswa kudumishwa na kuendelezwa!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 17 Novemba 2014 amekutana na kuzungumza Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia linalofanya hija yake ya kitume mjini Vatican kwa kuwatakia kheri na baraka katika kipindi hiki cha sala na tafakari ya kina, ili kujenga na kuimarisha mshikamano na udugu, ili kuweza kupata mavuno mengi kadiri ya Roho Mtakatifu anavyowakirimia.

Imani, mapendo na matumaini miongoni mwa wananchi wa Zambia ni matunda ya kazi ya Roho Mtakatifu iliyofanywa na Wamissionari hata kama wakati fulani kazi hii ilikabiliana na kinzani pamoja na changamoto kubwa za kitamaduni, lakini imani ikaendelea kukua na kuota mizizi katika maisha ya wananchi wa Zambia, kiasi kwamba, tunu msingi za maisha ya Kikristo zimesaidia kuleta mabadiliko miongoni mwa wananchi wa Zambia, hasa katika sekta ya afya, elimu na Parokia zinazoendelea kuibuka kwa wingi nchini humo. Kuna ongezeko kubwa la waamini walei pamoja na miito ya kipadre na kitawa, neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Zambia inaendelea kukabiliana na changamoto mbali mbali katika maisha, hasa kutokana na ongezeko la umaskini, hali ambayo inazifanya familia nyingi kutafuta njia za mkato; mambo ambayo wakati mwingine yanahatarisha imani na matokeo yake ni watu kukata tamaa. Baba Mtakatifu anasema, Familia inapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza kwani ni msingi wa Jamii, mahali ambapo watu wanajifunza kuishi kwa pamoja, licha ya tofauti zao msingi na kwamba ni mahali pa kurithisha imani, dhamana inayotekelezwa na wazazi. Familia ni madhabahu ya Injili ya Uhai, inayopaswa kudumishwa na kuendelezwa.

Baba Mtakatifu anawataka viongozi wa Kanisa Katoliki nchini Zambia kuhakikisha kwamba, wanajifunga kibwebwe kujenga na kuimarisha tunu msingi za maisha ya kifamilia, kwa kutoa katekesi ya kina, ili watu wafahamu ukweli na imani yao kwa kina, ili waweze kulinda na kuitetea dhidi ya mashambulizi yanayoendelea kujitokeza.

Wanandoa wadumishe uaminifu na mapendo ya ndoa, wasaidie majiundo ya kina kwa watoto wao sanjari na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia yanayojikita katika Mafundisho tanzu ya Kanisa na kumwilishwa katika uhalisia wa maisha ya wananchi wa Zambia.

Viongozi wa Kanisa waendelee kuwa karibu zaidi na vijana katika malezi na makuzi yao, ili waweze kuwa na utambulisho makini, tayari kushiriki katika kazi ya uumbaji kwa kujikita katika wito wa ndoa au Daraja takatifu au maisha ya kitawa kwa ajili ya wokovu wa roho za watu. Vijana wafundwe kuchuchumilia usafi wa moyo pamoja na kukuza ushirikiano miongoni mwa utume wa vijana nchini Zambia, ili wote waweze kujisikia kuwa wako ndani ya Familia ambayo kimsingi ni Kanisa dogo la nyumbani.

Baba Mtakatifu anawataka viongozi wa Kanisa nchini Zambia kuhakikisha kwamba, wanawasaidia: maskini, wanyonge na wagonjwa, hasa wale wa Ukimwi, kwani hawa wana nafasi ya pekee katika maisha na utume wa Kanisa. Watangaziwe Neno la Mungu, wapewe Sakramenti za Kanisa na kusindikizwa katika hija ya imani yao, ili kufikia ukamilifu.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka Maaskofu Katoliki Zambia kuwa karibu na wasaidizi wao wao katika maisha na kazi za Kanisa, kwa kuwaonesha ukarimu na upendo wa kibaba; kwa kuwasaidia katika mahitaji yao msingi na kuwasaidia, ili wasimezwe na malimwengu, kwa kuwapatia mambo muhimu ya maisha. Maaskofu waendeleze hazina kubwa ya maisha ya kitawa katika majimbo yao, ili vijana wengi waweze kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake bila ya mioyo yao kugawanyika.

Baba Mtakatifu Francisko amemkumbuka kwa namna ya pekee, Marehemu Rais MIchael Sata aliyefariki dunia hivi karibuni, kwa kuwataka viongozi wa Kanisa kuendelea kushirikiana na viongozi wa Serikali kwa ajili ya kutafuta na kudumisha mafao ya wengi; kutoa ushuhuda wa kinabii kwa kuwatetea maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; daima wakiwa wameungana na kushikamana na Familia ya Mungu nchini Zambia, huku wakishirikishana matendo ya huruma.

Baba Mtakatifu amekazia umuhimu wa Maaskofu nchini Zambia kuendeleza mchakato wa Utamadunisho, ili kuweza kusafisha mila na tamaduni zinazosigana na Injili ya Kristo, ili Watu wa Mungu waweze kupata zawadi ya Injili itakayowaonjesha furaha na huruma, huku wakijitahidi kuishi kadiri ya changamoto za Kiinjili, ili kushiriki katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu unaosimikwa katika haki na amani.

Maaskofu wanakumbushwa kwamba, wao ni watenda kazi katika shamba la Bwana, dhamana inayohitaji sadaka binafsi, uvumilivu na upendo unaofumbatwa katika imani na sadaka iliyotolewa na watangulizi wao, ili kuweza kuliimarisha Kanisa nchini Zambia.







All the contents on this site are copyrighted ©.