Misale ya Altare kwa lugha ya Kiswahili yaanza kushughulikiwa!
Tume za Liturujia kutoka Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kenya na Tanzania, hivi karibuni
zimekutana Nairobi, ili kupanga mkakati utakaoziwezesha tume hizi kutafsiri Misale
ya Altare kutoka katika lugha ya Kilatini kwenda lugha ya Kiswahili, kwa ajili ya
matumizi ya waamini wanaozungumza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya Afrika Mashariki.
Mradi huu, utawashirikisha wadau wengine kama vile, Idara ya shughuli za kichungaji
ya AMECEA na Shirika la Uchapaji la Mabinti wa Mtakatifu Paulo. Misale ya Altare inayotumika
kwa sasa ni ile iliyochapishwa kunako mwaka 1969 na Mwaka 1975. Kwa sasa anasema Askofu
Salutaris Melchior Libena, Mwenyekiti wa Idara ya Liturujia ya Baraza la Maaskofu
Katoliki Tanzania kwamba, kuna mabadiliko makubwa yaliyofanywa na Kanisa kuhusiana
na Misale ya Altare yanayopaswa kurekebishwa kadiri ya tasfiri ya lugha ya Kilatini.
Askofu
Dominic Kimengich, Mwenyekiti wa Idara ya Liturujia, Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya
anasema, nchi hizi mbili, yaani Kenya na Tanzania zinatumia Kiswahili kama lugha ya
taifa, kumbe, wanaweza kushirikiana ili kufanya tasfiri ya Misale ya Altare, kama
ilivyoshauriwa wakati wa maadhimisho ya mkutano mkuu wa Shirikisho la Mabaraza ya
Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA wakati wa mkutano wake wa kumi
na nane, ulioadhimishwa huko Lilongwe, Malawi.
Wadau kwa pamoja, wameandaa
mpango kazi, utakaonyambulishwa wakati wa mkutano mwingine unaotarajiwa kufanyika
Jijini Dar es Salaam, Mwezi, Desemba 2014. Huu utakuwa ni mkutano utakaowashirikisha,
wajumbe watakaopewa dhamana ya kutafsiri vitabu hivi kutoka katika lugha ya Kilatini
kwenda katika lugha ya Kiswahili.
Inatarajiwa kwamba, tafsiri rasmi ya Misale
ya Altare kwa lugha ya Kiswahili inaweza kupatikana kati ya mwezi Mei na Juni 2015
na Muswada wake kuhakikiwa na Mabaraza ya Maaskofu mwezi Septemba 2015, kabla ya kutumwa
mjini Vatican kwa ajili ya kuidhinishwa rasmi na Baraza la Kipapa la Ibada, Nidhamu
na Sakramenti za Kanisa.