Sinodi imeliwezesha Kanisa kuona na kusikiliza kwa dhati!
Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia ni kielelezo cha mchakato
wa Mama Kanisa kutaka kusikiliza kwa dhati kabisa furaha, matatizo na changamoto ambazo
familia zinakabiliana nazo katika ulimwengu mamboleo. Ni maneno ya Kardinali Lorenzo
Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu alipokutana na kuzungumza na Wabunge
kutoka Uingereza, waliomtembelea mjini Vatican Alhamisi, tarehe 30 Oktoba 2014.
Katika
mazungumzo yake, amewashirikisha wabunge hao mambo makuu yaliyojitokeza wakati wa
maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia pamoja na changamoto
zilizoibuliwa na Mababa wa Sinodi. Kadiri ya maelezo yaliyokuwa yanatolewa na baadhi
ya vyombo vya habari inaweza kudhaniwa kwamba, maadhimisho ya Sinodi, yalikuwa ni
"patashika nguo kuchanika", lakini, kimsingi maadhimisho haya yalikuwa ni mang'amuzi
makubwa kwa Mama Kanisa kutembea kwa pamoja na kusikiliza kwa dhati changamoto zinazojitokeza
katika maisha na utume wa Kanisa kuhusiana na maisha ya ndoa na familia.
Mafanikio
makubwa yaliyojitokeza katika maadhimisho haya ni utambuzi wa umuhimu wa Sinodi katika
maisha na utume wa Kanisa, kwa kutambua kwamba, Kristo Mfufuka amewajalia wafuasi
wake zawadi ya Roho Mtakatifu, ili kuweza kushiriki kwa ukamilifu katika maisha na
utume wa Kanisa. Kanisa litaendelea kujikita katika Mafundisho yake tanzu, Maandiko
Matakatifu na Mapokeo, pamoja na kuendelea kusoma alama za nyakati, ili kuweza kukabiliana
na changamoto za nyakati hizi.
Kardinali Baldiserri anasema, kati ya changamoto
kubwa kwa sasa ni waamini kutalikiana, mwelekeo wa ndoa za watu wa jinsia moja na
ndoa za wake wengi. Changamoto hizi zimejadiliwa kwa kina na mapana katika maswali
dodoso yaliyotumwa kwa waamini na watu wenye mapenzi mema, jambo ambalo limewasaidia
Mababa wa Sinodi kufahamu ukweli wa maisha ya ndoa na familia katika undani wake.
Kuna
baadhi ya watu wameshutumu msimamo na ukweli wa Mafundisho ya Kanisa kuhusu ndoa na
familia na baadhi yao wamelishauri Kanisa kufanya maamuzi magumu kwa kuzingatia changamoto
za watu wa nyakati hizi. Kardinali Baldisseri anasema, jambo la kufurahisha ni kuona
kwamba, waamini wanaifahamu Injili na kanuni maadili katika maisha ya ndoa na familia,
mambo ambayo hayawezi kuwekwa kando kwani ni sehemu ya vinasaba vya maisha na utume
wa Kanisa. Viongozi wa Kanisa wamepewa dhamana ya kuhakikisha kwamba, wanatekeleza
utume wao wa kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza Watu wa Mungu kadiri ya mafundisho
ya Mama Kanisa.
Mababa wa Sinodi katika ukweli na uwazi; kwa moyo wa unyenyekevu
na hekima, wameshirikishana mambo msingi ambayo yanaweza kulisaidia Kanisa kuandaa
mikakati ya kichungaji kwa ajili ya watu wa ndoa na familia, ili Mama Kanisa aendelee
kutangaza Injili ya Familia kwa Watu wa Mataifa. Sinodi ilipania pamoja na mambo mengine
kuhakikisha kwamba, inafafanua Mafundisho ya Kanisa kuhusu maisha ya ndoa na familia
mintarafu mwelekeo wa kimissionari na kichungaji.
Kanisa linatambua kwamba
ni chombo cha wokovu, huruma na upendo, lina dhamana ya kuwapokea na kuwakumbatia
wote, watakatifu na wadhambi wanaopaswa kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu. Mababa
wa Sinodi wameshirikisha kuhusu uzuri na utakatifu wa maisha ya ndoa na familia; utu
na heshima ya maisha ya ndoa; mambo msingi katika maisha na utume wa Kanisa na Ulimwengu
katika ujumla wake.
Dhamana ya Mama Kanisa ni kuendelea kutangaza Injili ya
Familia kwa kuzingatia: ukweli na uwazi, kwa unyenyekevu na busara, huku akiwasindikiza
wanafamilia wanaogelea katika shida na mahangaiko mbali mbali ya maisha. Kwa kutambua
haya yote, hapa Mama Kanisa anataka kupiga hatua nyingine tena kwa kuwaalika watoto
wake kutubu na kumwongokea Mungu; daima wakijitahidi kutekeleza mapenzi ya Mungu katika
maisha yao; kwa kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa Kanisa.
Kardinali
Baldisseri anasema, huu ndio ukweli wa mchakato wa maadhimisho ya Sinodi maalum ya
Maaskofu kwa ajili ya familia, kama walivyoonesha Mababa wa Sinodi na Baba Mtakatifu
Francisko akaweka mkazo wa pekee kama mhimili wa umoja na mshikamano wa Kanisa, changamoto
kwa waamini kukumbatia kweli za Kiinjili.
Viongozi wa Kanisa wataendelea kuwaganga
na kuwaponya waamini wanaokabiliana na madonda makubwa katika maisha ya ndoa na familia,
kwa kutumia kweli za Kiinjili na Huruma inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa
lake. Mada zilizojadiliwa na Mababa wa Sinodi zilikuwa zinagusa maisha ya watu wengi
ndiyo maana vyombo vya habari vilikuwa vinafuatilia kwa makini mchakato wa maadhimisho
ya Sinodi.
Mababa wa Sinodi wamejitahidi kujikita katika mambo msingi ya maisha
ya ndoa na familia; kanuni maadili, utu na heshima ya binadamu; mambo msingi ambayo
yanapaswa kutolewa ushuhuda na Wakatoliki katika hija ya maisha yao ya kila siku!