Bwana Roland Msiska Katibu mkuu wa Baraza la Mawaziri Zambia anasema, mwili wa Marehemu
Rais Sata unatarajiwa kuwasili nchini Zambia, Jumamosi jioni tarehe Mosi, Novemba
2014 na kuzikwa tarehe 11 Novemba 2014, katika Uwanja wa Mabalozi mjini Lusaka. Rais
Guy Scott ataongoza protokali, wakati mwili wa Marehemu Sata utakapowasili kwenye
Uwanja wa Kimataifa wa Keneth Kaunda na baadaye mwili wake utawekwa kwenye Kituo cha
Mikutano kimataifa cha Mulungushi.
Wananchi wataanza kutoa heshima zao za
mwisho kwa Rais Sata kuanzia Jumapili tarehe 2 Novemba 2014. Ibada kwa ajili ya kumwombea
Marehemu Rais Sata itafanyika kwenye Uwanja wa Mashujaa, Lusaka hapo tarehe 11 Novemba
2014.
Marehemu Rais Michael Chilufya Sata aliyefariki hivi karibuni Jijini
London aliwahi kusema kwamba, atakatofariki dunia, watu wakumbuke kwamba, kuna “Mwanaume
aliyekuja kuleta mabadiliko nchini Zambia” kwa kusema “…ndefwaya nga nafwa mukalelanda
ati twalikwete abume pantu ndeisa mukuchinja Zambia”. Marehemu Sata alionesha moyo
wa uzalendo na majitoleo katika huduma kwa wananchi wa Zambia katika nafasi mbali
mbali alizobahatika kudhaminishwa na wananchi wa Zambia, kiasi kwamba, upendo kwa
wananchi wa Zambia, ukawa ni wimbo wake wa Taifa.
Alisimama kidete kulinda
na kutetea utu na heshima ya wale waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii, akajitambulisha
na watu wa matabaka mbali mbali, kiasi kwamba, wengi wakamkubali kuwa kweli ni mtu
wa watu!Unyenyekevu ilikuwa ni silaha yake madhubuti na msamaha kwa watu, kwake kilikuwa
ni kielelezo cha unyonge; lakini mambo haya mawili yakawagusa watu wengi ndani na
nje ya Zambia. Alipenda kuwaona Wazambia wengi wakijikita katika mchakato wa toba,
msamaha na upatanisho wa kweli; kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.
Hivi
ndivyo Bwana George Chella, Msaidizi wa Marehemu Rais Sata katika habari na mahusiano
ya kijamii anavyomkumbuka Marehemu Rais Sata enzi ya uhai wake. Kwa mila na tamaduni
nyingi za Kiafrika wakati wa maombolezo, watu wanapenda kusimulia mazuri ya yule ambaye
ametangulia mbele ya haki, kwa kutambua kwamba, kama binadamu alikuwa na mapungufu
yake, lakini si kazi yao kumhukumu, bali Mwenyezi Mungu ndiye hakimu mwenye haki kwani
binadamu anababaisha tu!
Wananchi wa Zambia wanaomboleza kwa kuondokewa na
Rais wao, waliyemtegemea kuwavusha katika bonde la umaskini, ujinga na maradhi, ili
hatimaye, Zambia iweze kucharuka kwa maendeleo endelevu. Mambo aliyoyasimamia katika
kipindi cha miaka mitatu ya Urais wake!