2014-10-31 11:46:28

Ebola ni janga la kimataifa!


Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni alionesha wasi wasi wake kutokana na kuongezeka kwa maambukizi ya ugonjwa wa Ebola sehemu mbali mbali za dunia, lakini kwa namna ya pekee Afrika Magharibi ambako kuna watu wengi wanaendelea kuathirika.

Baba Mtakatifu alionesha kwa kuguswa sana na mahangaiko ya watu hawa na kusema kwamba, anawakumbuka katika sala zake na kuwashuruku wafanyakazi katika sekta ya afya pamoja na watu wanaoendelea kujitolea kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu walioathirika kwa ugonjwa wa Ebola. Ni watu wanaoonesha ujasiri kwa kuwasaidia wengine.

Baba Mtakatifu Francisko alitumia fursa hii kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kujifunga kibwebwe kuhakikisha kwamba, ugonjwa wa Ebola unapatiwa ufumbuzi wa kudumu pamoja na kuwaomba watu kuendelea kuwaombea wale wote waliopoteza ndugu, jamaa na marafiki zao kutokana na ugonjwa wa Ebola.

Kwa upande wake, Bwana Ban Ki-moon, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kutoa jibu makini kama sehemu ya mchakato wa kupambana na ugonjwa wa Ebola, kwani kwa sasa Ebola linaonekana kuwa ni janga la kimataifa. Umoja wa Mataifa utaendelea kusaidia juhudi za kutokomeza ugonjwa huu kutoka katika sura ya dunia. Amewashukuru na kuwapongeza wafanyakazi wanaotoa huduma kwa watu walioathirika kwa ugonjwa wa Ebola, kwa kuonesha upendo na mshikamano wa dhati.







All the contents on this site are copyrighted ©.