Afrika inahitaji miaka 60 ili kufutilia mbali baa la umaskini wa kutupwa!
Pengo kati ya matajiri wanaokula na kusaza na maskini, yaani "akina yakhe pangu pakavu
tia mchuzi" linaendelea kuongezeka kila kukicha na ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa
haitaweza kulivalia njuga baa la umaskini duniani, inakadiriwa kwamba, itawachukua
watu takribani miaka sitini ili kuweza kutokomeza baa la umaskini duniani, kadiri
ya taarifa iliyotolewa na Shirika la Misaada kutoka Uingereza, OXFAM, linalofanya
kazi zake sehemu mbali mbali duniani.
Taarifa ya OXFAM inaonesha pengo kubwa
kati ya matajiri na maskini duniani, ikilinganishwa na hali ilivyokuwa miaka thelathini
iliyopita. Kuanzia mwaka 2009 idadi ya matajiri duniani imeongezeka maradufu, lakini
bado kuna watu millioni 805 wanaoteseka kwa baa la njaa. Inakadiriwa kwamba, kuna
watu millioni 358 kutoka Kusini mwa Jangwa la Sahara wanaosumbuliwa kwa baa umaskini,
baa la njaa na utapiamlo wa kutisha.
Kwa mtindo huu, Bara la Afrika litahitaji
walau si pungufu ya miaka sitini ili kuweza kudhibiti baa la umaskini kwa asilimia
tatu. Upembuzi huu unaweza pia kuwa ni kielelezo hata katika sehemu nyingine za dunia.