2014-10-25 08:11:15

Kanisa linapenda kuhamasisha mchakato wa mabadiliko ya kweli katika jamii yanayosimikwa katika haki


Baraza la Kipapa la haki na amani kwa kushirikiana na Taasisi ya Kipapa ya Sayansi Jamii pamoja viongozi wa vyama vinavyotetea utu na heshima ya binadamu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kwa pamoja wameandaa mkutano unaojadili kwa kina haki msingi za binadamu, hususan kwa watu wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; watu ambao utu na heshima yao vinaendelea kuwekwa rehani. Mkutano huu unaanza kutimua vumbi mjini Roma kuanzia siku ya Jumatatu, tarehe 27 hadi tarehe 29 Oktoba, 2014.

Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani anasema, kuna watu wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, hawa ni wale wanaotambulikana kutoka katika dunia au maskini, "akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi". Hawa ni matokeo ya utandawazi usioguswa na mahangaiko ya watu, wengi wao wakiwa ni vijana ambao hawana tena fursa za ajira na wazee wanaoonekana kuwa kama kero kubwa kwa jamii kiasi cha kuizuia jamii "kula kuku kwa mrija".

Hizi ni baadhi ya changamoto zinazojitokeza katika ulimwengu wa utandawazi usioguswa na mateso wala mahangaiko ya watu, changamoto kwa Mama Kanisa kusikiliza kwa makini kilio cha haki na kujibu kilio hiki kwa nguvu. Ni mwaliko wa kuwakumbatia na kuwashirikisha wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Huu ni wajibu wa Kanisa na Jamii husika, ili kila mtu aweze kujisikia kuwa ni mdau na mtu muhimu sana katika ujenzi wa jamii, ustawi na maendeleo ya watu katika medani mbali mbali za maisha.

Kardinali Turkson anasema, jambo la msingi ni kusikiliza kwa makini, sio tu mahangaiko na mateso ya watu hawa, bali pia matarajio na matumaini yao pamoja na mikakati ambayo watu hawa wanatamani ifanyiwe kazi, kwa kutambua kwamba, wao ni wadau wa kwanza katika utekelezaji wa mikakati hii katika maisha yao na wala si watazamaji katika mchakato huu wa maendeleo. Ni watu wanaohitaji mabadiliko ya dhati katika masuala ya kiuchumi, kijamii, kisiasa na kitamaduni, ili waweze kujiunga na kuunda makundi au vikundi vya kutekeleza mikakati hii.

Mkutano huu pamoja na mambo mengine anasema Kardinali Turkson unajadili mambo makuu matano yaani: changamoto zinazoendelea kujitokeza katika masuala ya makazi ya watu, fursa za ajira, ardhi, uhalifu na mazingira. Mama Kanisa kwa upande wake, anapenda kuzimilisha changamoto hizi kama sehemu ya utume wake kwa Watu wa Mataifa, ili kuhamasisha mabadiliko ya kweli katika jamii, ili kujenga ulimwengu unaosimikwa katika haki.

Watu nao kwa upande wao wanataka kushirikiana na Kanisa ili kuyachachua malimwengu katika ngazi mbali mbali kwa kuwashirikisha watu ile nguvu ya upendo unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu na huruma iliyodhihirishwa na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kulihamasisha Kanisa kushikamana na kuwasaidia maskini ili waweze kukabiliana na changamoto mbali mbali za maisha. Huu ni mchakato endelevu wa mawasiliano yanayojikita katika majadiliano, ushirikiano na uratibu katika ngazi mbali mbali. Huu ni mwaliko kwa watu kushiriki kikamilifu katika mustakabali wa maisha yao kwa siku za usoni.







All the contents on this site are copyrighted ©.