2014-10-25 08:37:58

Baba Mtakatifu Francisko kukutana na wadau wa huduma kwa watu wenye matatizo ya afya ya akili


Baraza la Kipapa la Wafanyakazi katika sekta ya afya, kuanzia tarehe 20 hadi tarehe 22 Novemba 2014 litafanya mkutano wake wa ishirini na tisa wa kimataifa mjini Vatican, utakaoongozwa na kauli mbiu "Watu wenye matatizo ya afya ya akili". Watu wenye matatizo ya afya ya akili na wale wanaowahudumia ndio walengwa wakuu wa mkutano huu wa kimataifa, ili kubainisha mbinu na mikakati itakayoimarisha na kukoleza matumaini kwa watu wenye matatizo ya afya ya akili pamoja na ndugu na jamaa zao wanaowahudumia.

Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la Wafanyakazi katika sekta ya afya anabainisha kwamba, huu ni mkutano utakaowashirikisha mabingwa na watalaam wa afya ya akili kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ili kukabiliana na changamoto hizi katika sekta ya afya. NI mkutano utakaozingatia masuala ya kisayansi, tiba, familia, taasisi za elimu na huduma pamoja na kuwa na mwelekeo wa jumla kwa Serikali na Jamii husika.

Wawezeshaji wa mkutano huu watashirikisha pamoja na mambo mengine masuala ya kijamii na kidini yanayolenga kupata ufumbuzi wa matatizo na changamoto zinazoendelea kuwakumba watu wenye matatizo ya afya ya akili. Mkutano huu utafunguliwa kwa Ibada ya Misa Takatifu itakayoongozwa na Kardinali George Pell, Mwenyekiti wa Sekretarieti ya Uchumi mjini Vatican.

Wajumbe wa mkutano huu watapata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko pamoja na kuwashirikisha wafanyakazi mbali mbali kutoka katika sekta ya afya, taasisi na vyama vinavyowahudumia wagonjwa. Kwa mara ya kwanza, Baba Mtakatifu Francisko ataweza kukutana ana kwa ana na hali halisi ya watu wanaoteseka kutokana na kudorora kwa afya ya akili katika mwelekeo wa kimataifa.

Kwa kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu wadau mbali mbali wataweza kushirikisha na kujipatia matumaini na imani kwamba, Kanisa bado lina wajali na wala katika mahangaiko yao, hawako pweke, bali kuna kundi kubwa la wadau wanaopenda kuwashirikisha na kuwamegea mshikamano wa upendo unaojikita katika kanuni maadili na utu wema.







All the contents on this site are copyrighted ©.