2014-10-23 07:55:09

Tafakari ya neno la Mungu Jumapili ya 30 ya Kipindi cha Mwaka A wa Kanisa


Mpendwa mwana wa Mungu, msikilizaji wa Radio Vatican kipindi tafakari Neno la Mungu, karibu tutafakari pamoja masomo Dominika ya 30 ya mwaka A wa Kanisa. Leo Neno la Mungu linatualika kutafsiri na kuona katika kila siku ya maisha yetu mpango wa Mungu unaotualika kukuza upendo kwake yeye na kwa jirani. Kwa kifupi ni mwaliko wa upendo ulio wa dhati. RealAudioMP3

Katika Somo la kwanza toka kitabu cha Kutoka tunapata wajibu wa kwanza wa kutenda katika mpango uleule wa upendo nao ni kuwaheshimu na kuwatunza maskini yaani watoto yatima, wajane na wageni. Hawa kwa hakika ni kundi ambalo lahitaji msaada wa daima kwa maana, yatima hawana wazazi, wajane hawana wenzi wao wa ndoa na wageni hawako nyumbani walikozaliwa au wanakoishi na hivi wako safarini, ni mahujaji.

Mwandishi anakazia jambo hili kwa maana kulikuwepo na hila na fitina dhidi ya kundi hili lisilo na nguvu katika jamii. Anawakumbusha wana wa Israeli kuwa hata wao walikuwa wageni huko Misri na hivi wakumbuke mateso waliyoyapata na kwa namna hiyo wataweza kuwasaidia wanaoteseka katikati yao. Mwandishi anaweka mbele yetu onyo kali kuwa ni chukizo kwa Mungu kuwatesa na kuwanyonya maskini.

Mpendwa mwana wa Mungu, leo hii hali ni ngumu katika jamii yetu, yaani mateso kwa wajane yameongezeka kupita kiasi, watoto yatima wamekuwa ni vichokoo katika jamii na hata wengine kuwa chanzo cha mtaji wa biashara. Wageni wakati fulani hatuwapi huduma ya kufaa. Hili ndugu zangu ni chukizo kwa Mungu. Vilio vyao ni vilio vya damu kwa Mungu kama damu ya Abeli. Mpendwa unayenisikiliza, naomba uache kabisa jambo hili ni kinyume na Injili ya upendo.

Mtume Paulo anapowaandikia Watesalonike akiendeleza shukrani zake kwao kwa sababu ya imani yao thabiti kwa Mungu kiasi kwamba imekuwa kielelezo cha mapendo ya Mungu kwa jumuiya zinazozunguka jumuiya yao, ni msaada kwetu wa kutuwezesha kugundua kuwa Injili ni kurudisha shukrani kwa Mungu na kushirikishana mapaji kati yetu na majirani na si kuleta manyanyaso kwa walio maskini.

Mtume anawashukuru Watesalonike kwa imani yao iliyojaa moyo wa kimisionari, ulio upanuzi wa himaya ya Mungu inayozidi kueleweka na kufunuliwa wazi zaidi kwa njia ya utume wao. Katika wajibu huo wa imani, matendo ya upendo ndiyo msingi wa maisha ya kikristu. Mtume Paulo anatupa mwanga pia wa kuelewa kuwa katika utume wetu wa upendo kwa vyovyote vile kutakuwa na upinzani kama walioupata watu wa Tesalonike, kumbe, yatupasa kutumaini daima.

Mpendwa mwanatafakari, katika somo la Injili fundisho msingi ni lile la amri ya upendo, yaani wajibu wa kila mmoja wetu kumpenda Mungu kwa moyo, akili na roho na kisha kuwekeza upendo huu katika kiumbe kilichoumbwa katika sura na mfano wa Mungu, yaani mwanadamu. Katika jamii ya kiyahudi zilikuwepo amri 613 na kati ya hizi 365 zilikuwa zinazuia watu wasifanye mambo mbalimbali katika jamii yao na 248 zilikuwa zinaelekeza kipi cha kufanya katika jumuiya.

Sheria hizi zilionekana kuwa na uzito sawa, ingawaje kulikuwa na kutokukubaliana katika hili. Baadhi ya walimu walisisitiza kuwa kumpenda Mungu na jirani ndiyo iliyokuwa ya kwanza. Tokana na shida hii Mafarisayo wanamwuliza Bwana, ipi ni amri kuu?

Bwana akijua nini maana ya swali lao ambalo msingi wake ni usawa wa amri 613 na majaribu kwake, anawaambia iliyo kuu ni kumpenda Mungu na jirani. Ndiyo kusema amri hii ni ufupisho wa mafundisho ya amri zote, ni ufupisho wa mafundisho ya Bwana. Na hivi Bwana anakazia njia ya kumpenda Mungu ni kwa njia ya jirani. Anaweka machoni pao kiumbe kitukufu yaani mwanadamu, kilicho sura na mfano wake kielelezo cha mapendo yake kwa ulimwengu na hivi njia ya kumpenda yeye. Jirani kama tulivyosikia katika kitabu cha kutoka ni yatima, mgeni na mjane na mwanadamu kwa ujumla kiumbe cha Mungu.

Mpendwa, ni wajibu wetu sasa kutambua kuwa kila siku tutafakaripo amri za Mungu mwisho wa tafakari yetu unapaswa kuwa ni kumpenda Mungu na Jirani. Pamoja na hilo moyo, roho na akili vinapaswa kujionesha katika imani na tumaini katika Mungu mmoja. Kumbe imani thabiti inakusanya akili, moyo na roho zetu na kuziweka machoni pa Bwana mwabudiwa daima, na yeye hutoa mwanga ambao huzaa upendo na sadaka kwa jirani. Tumsifu Yesu Kristo na Maria.

Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.