Chama cha Sheria Kimataifa kimeendelea kujipambanua kwa kutoa huduma makini kwa Jamii,
ili kujenga na kudumisha misingi ya haki inayoheshimu utu na haki msingi za binadamu
bila ubaguzi na kwamba, Kanisa linatekeleza dhamana na utume wake kwa njia ya Uinjilishaji
wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Kanisa bado linajishughulisha
sana katika mchakato wa kutafuta, kulinda na kudumisha misingi ya haki na amani sehemu
mbali mbali duniani.
Hii ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Baba Mtakatifu
Francisko wakati alipokutana na kuzungumza na wajumbe wa Chama cha Sheria Kimataifa,
waliomtembelea mjini Vatican siku ya Alhamisi, tarehe 23 Oktoba 2014. Baba Mtakatifu
amegusia mambo yanayopelekea watu kutaka kulipizana kisasi kuwa ni pamoja na: vyombo
vya sheria na kisiasa kushindwa kutatua migogoro na kinzani zinazojitokeza ndani ya
Jamii.
Kuna baadhi ya wanasiasa na vyombo vya mawasiliano ya kijamii vimekuwa
vikijihusisha katika kuchochea vurugu kati ya watu na kwamba, watu wengi wamepoteza
imani katika mfumo katika vyombo vya kisheria, kiasi cha baadhi ya watu kubebeshwa
mizigo ya kijamii.
Baba Mtakatifu amewaambia wanachama hawa kwamba, kuna miundo
ya sheria ambayo imeshindwa kudhibitiwa, kumbe ni wajibu na dhamana ya wanasheria
kurekebisha hali hii kama inavyojionesha kwenye adhabu ya kifo, ambayo inakiuka haki
msingi za binadamu. Tatizo hili limechangia kuibuka kwa mjadala mkubwa unaotaka Jumuiya
ya Kimataifa kufuta adhabu ya kifo, mwaliko kwa wanasheria kutekeleza wajibu wao kikamilifu
bila ya kushinikizwa na vyombo vya mawasiliano ya jamii, kwa kuheshimu zawadi ya maisha
sanjari na kuleta mabadiliko ya kina ndani ya Jamii kwa njia ya mifumo ya adhabu zinazotolewa.
Baba Mtakatifu Francisko kwa namna ya pekee kabisa anasema, Sheria haina budi
kusimama kidete kulinda na kutetea maisha, utu na heshima ya binadamu, changamoto
ya kutoa adhabu mbadala badala ya kuendelea kuendekeza adhabu ya kifo. Hii inatokana
na ukweli, Serikali nyingi zina uwezo wa kuzuia na kudhibiti uhalifu kwa aliyetenda
kosa kama hili ili asiweze kuleta madhara, bila ya kumpatia adhabu ya kifo.
Baba
Mtakatifu anasema adhabu ya kifo imepitwa na wakati kwani takwimu zinaonesha kwamba,
kati ya mataifa 60 yanayotoa adhabu ya kifo, ni mataifa 35 tu ambayo yanatekeleza
adhabu hii katika kipindi cha miaka kumi iliyopita. Kanisa linasema kwamba, adhabu
ya kifo inayotolewa kwa watu ni kinyume cha haki msingi za binadamu, changamoto kwa
waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kupinga adhabu ya kifo, ili
zawadi ya maisha iweze kuheshimiwa na kuthaminiwa.
Baba Mtakatifu anasema wafungwa
magerezani wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha hata kabla ya kuhukumiwa, kiasi cha
kuyafanya magereza kufurika kupita kiasi na kwamba, wakati mwingine askari wametumia
vibaya magereza kwa kuwanyanyasa na kuwadhulumu wafungwa. Kumbe, kuna haja kwa Jamii
kuhakikisha kwamba, inarekebisha na kuheshimu mfumo wake wa sheria ili uhuru wa watu
na haki zao msingi ziweze kuheshimiwa.
Serikali hazina budi kudhibiti adhabu
kali na za kinyama wanazopewa wafungwa, kiasi cha kudhalilisha utu na heshima ya binadamu,
mambo yanayotendeka hasa kwenye magereza yenye ulinzi mkali, hospitali za wagonjwa
wa afya ya akili au vizuizi maalum. Baba Mtakatifu anasema, Jumuiya ya Kimataifa haina
budi kutoa kipaumbele cha kwanza kwa kusimama kidete kulinda na kudumisha utu na heshima
ya binadamu wakati wa kutekeleza adhabu mbali mbali. Wazee wasaidie kuelimisha umma
kwa kusimulia mapungufu yao na fundisho walilolipata wakiwa gerezani.
Baba
Mtakatifu anakiri kwamba, kuna uhalifu mwingine ambao unafanywa na watu binafsi lakini
una madhara makubwa kwa utu wa binadamu na mafao ya wengi. Haya ni matukio ambayo
wakati mwingine yanawahusisha watu mbali mbali. Kwa mfano: biashara haramu ya binadamu
na utumwa mamboleo. Ikiwa kama Serikali na Jumuiya ya Kimataifa zitawajibika barabara,
dhuluma hii inaweza kufutika katika uso wa dunia.
Chanzo kikuu cha biashara
haramu ya binadamu ni umaskini wa kutupwa, kwani takwimu zinaonesha kwamba, kuna watu
billioni moja wanaishi katika umaskini mkubwa na wengine billioni moja wanaishi katika
mazingira hatarishi bila kupata huduma msingi kama vile maji safi na salama, umeme,
elimu na afya. Kinzani za kivita na migogoro ya kijamii ni kati ya mambo ambayo yanaendelea
kuwatumbukiza watu katika baa la njaa, umaskini, ujinga na maradhi pamoja na kuongezeka
kwa idadi kubwa ya wakimbizi na wahamiaji.
Baba Mtakatifu Francisko amegusia
pia tatizo la rushwa ambayo kwa sasa ni "janga la kimataifa" kwani linaendekezwa na
baadhi ya viongozi wa kijamii wenye uchu wa mali na madaraka. Mafisadi kutoka sehemu
mbali mbali za dunia wanaonekana kustawi na kushamiri kama "mtende wa Lebanon" na
hivyo kuonekana kuwa ni watu wanaopaswa kuigwa; dhamiri za watu zimekufa.
Watu
watambue kwamba, rushwa ni dhambi kubwa yenye mwelekeo wa kutaka kumeza watu wengi,
lakini ikumbukwe kwamba, rushwa ni kielelezo cha ukosefu wa matumaini. Sheria nyingi
zimekuwa hafifu katika kupambana na rushwa ulimwenguni. Hata wala na watoa rushwa
bado wanahimizwa na Kristo mwenyewe kutubu na kumwongokea, ili waweze kupata maisha
bora zaidi.
Adhabu inayotolewa kwa wala rushwa inaonesha ubaguzi kwani mafisadi
wadogo wadogo ndio wanaokamata na kutangazwa sana, lakini mafisadi na wala rushwa
wakuu, wanaendelea "kutesa kwa zamu". Viongozi wa Serikali wakati mwingine wanakuwa
ni kizingiti katika utekelezaji wa sheria.
Mwishoni, Baba Mtakatifu anasema,
utekelezaji wa sheria uongozwe na kanuni inayozingatia kwanza kabisa maisha ya mwanadamu;
utu na heshima yake. Amewaambia wajumbe wa Chama cha Sheria Kimataifa kwamba, ataendelea
kuwaenzi katika utume wao kwa njia ya sala na sadaka yake, ili utekelezaji wa sheria
uwe ni kwa ajili ya huduma kwa binadamu katika sekta ya haki. Kwa waamini wanapaswa
kuonesha mfano bora, kwa kushiriki katika mchakato wa Uinjilishaji, huku wakikimbilia
msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu, chimbuko la uwezo wa kufikiri na haki.