2014-10-20 08:40:41

Ushirikiano wa kiteknolojia usaidie kudumisha amani na usalama!


Askofu mkuu Bernadito Auza, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa, hivi karibuni akichangia mada kwenye mkutano mkuu wa Umoja wa Mataiafa kuhusu ushirikiano wa kimataifa anabainisha kwamba, imani inaweza kuisaidia sayansi kutambua na kuthamini kazi kubwa ya uumbaji ambayo mwanadamu amekabidhiwa kutunza na kuiendeleza kwa ajili ya mafao ya wengi, lakini kwa kuwa na mtazamo wa pekee kwa ajili ya maskini, ili nao waweze kufaidika na vitega uchumi vinavyofanywa sehemu mbali mbali za dunia.

Askofu mkuu Bernadito Auza anasema, ushirikiano wa kimataifa unagusa haki miliki ya kiakili, leseni na matumizi sahihi ya anga la kimataifa, linalohifadhi teknolojia kubwa ya mawasiliano duniani, kikolezo muhimu sana katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kijamii, lakini hadi sasa eneo hili limekuwa ni chanzo cha kinzani za kiuchumi na kijamii badala ya kujikita katika mafao ya wengi pamoja na amani duniani. Kanuni maadili ya Jumuiya ya Kimataifa katika matumizi anga la kimataifa ni muhimu sana katika mchakato unaopania kukuza na kudumisha amani kwa kudhibiti biashara haramu ya silaha, inayotishia amani na usalama wa Jumuiya ya Kimataifa.

Ujumbe wa Vatican kwenye mkutano huu, unaipongeza Jumuiya ya Kimataifa kwa kucharuka katika mikakati ya kuifahamu sayari dunia na mazingira yake na kwamba, ufahamu na maarifa haya yawajengee watu uwezo wa kulinda na kutunza mazingira kwa kubadili mfumo wa maisha, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Teknolojia isaidie kupambana na ujinga, maradhi na umaskini na kamwe teknolojia hii isiwakandamize watu kwa kulazimisha kufuata tamaduni na tunu msingi za maisha kutoka kwa Jamii nyingine, kwa kisingizio cha kuwa na nguvu ya kiteknojia. Anga linapaswa kutambulika kuwa ni sehemu ya urithi wa Jumuiya ya Kimataifa. Watu wazingatie kanuni maadili, ili urithi huu uweze kuwafaidisha watu wengine kwa siku za usoni.







All the contents on this site are copyrighted ©.