2014-10-18 16:20:36

Ujumbe wa Mababa wa Sinodi kwa Watu wa Mungu!


Baada ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia yaliyoanza hapo tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014, yakiongozwa na kauli mbiu "Changamoto za kichungaji kuhusu familia mintarafu Uinjilishaji, Mababa wa Sinodi wametoa ujumbe kwa Familia ya Mungu sehemu mbali mbali duniani wakionesha umoja na mshikamano wao wa dhati na Baba Mtakatifu Francisko wakati wote wa maadhimisho ya Sinodi, kwa kutambua kwamba, Yesu Kristo ni njia, ukweli na uzima. Mababa wa Sinodi wanazishukuru familia zote zinazoendelea kuonesha uaminifu, imani, matumaini na mapendo. RealAudioMP3

Mababa wa Sinodi wanasema hata wao, wamezaliwa na kukulia katika familia, huku wakiwa na historia na makando kando mbali mbali. Kama viongozi wa Kanisa wamekutana na kuishi na na familia ambazo zimesimulia na kuonesha kwa njia ya ushuhuda wa matendo uzuri na matatizo ya familia. Maandalizi ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu yalianza kwa kutuma maswali dodoso kwa watu sehemu mbali mbali za dunia, ili kusikiliza kwa makini uzoefu na mang'amuzi mbali mbali ya kifamilia.

Majadiliano kati ya Mababa wa Sinodi, yamekuwa ni utajiri mkubwa kati yao katika mchakato wa kutambua ukweli kuhusu maisha ya kifamilia. Mababa wa Sinodi wanaziambia Familia kwamba, Yesu anasimama mlangoni pao huku akibisha hodi, ikiwa kama watasikiliza sauti yake, atakuja na kula pamoja nao. Yesu hadi leo hii anaendelea kupiga hodi katika barabara na mitaa ya miji na majiji mbali mbali kama alivyofanya alipokuwa akiishi katika Nchi Takatifu.

Mababa wa Sinodi wanakiri kwamba, katika nyumba za waamini kuna mwanga na giza; kuna changamoto kubwa, wakati mwingine za kukatisha tamaa. Giza hili limekuwa nene kiasi kwamba, linawatendea vibaya na kusababisha wanafamilia kutenda dhambi. Changamoto kubwa ni uaminifu miongoni mwa wanandoa. Hii inatokana na kumong'onyoka kwa imani na tunu msingi za kimaadili; ubinafsi, mahusiano tenge, msongo wa mawazo na ukosefu wa tafakari ya kina; haya ni mambo yanayozikumba familia. Kuna baadhi ya wanandoa wamekosa uvumilivu, hawana uhakika wa mambo; hawana tena moyo wa kusamehe, upatanisho na sadaka. Huu ndio mwanzo wa kuporomoka kwa ndoa na hivyo kusababisha kuibuka kwa mahusiano mapya, wanandoa wapya pamoja na ndoa mpya, kiasi cha kugumisha maisha ya kifamilia mintarafu Ukristo.

Mababa wa Sinodi wanakiri kwamba, kuna hali ngumu kwa wanandoa kuishi kwa pamoja kutokana na magonjwa yanayowaandama watoto, magonjwa makubwa, uzee au kifo cha wapendwa ndani ya familia. Pamoja na changamoto zote hizi, bado hata hivyo kuna familia ambazo zimedumu katika uaminifu na kuendelea kuishi katika majaribu haya kwa ujasiri, imani na mapendo, kwa kutambua kwamba, hivi si vikwazo vinavyoweza kusababisha kinzani, bali ni zawadi inayowasaidia kumwona Yesu Kristo mteseka katika hali kama zile.

Mababa wa Sinodi wanasema kwamba, kuna familia ambazo zinakumbana na athari za mtikisiko wa uchumi kimataifa, hali ambayo inadhalilisha utu na heshima ya binadamu; ukosefu wa fursa za ajira jambo linalowanyima uwezo wa kuhudumia familia zao hata kwa mambo msingi; kundi kubwa la vijana wasiokuwa na kazi, vijana ambao wanaweza kutumbukia kwa urahisi katika matumizi haramu ya dawa za kulevya na makosa ya jinai.

Mababa wa Sinodi wanaona mbele yao familia maskini za watu wanaolazimika kuzikimbia nchi zao ili kutafuta hali nzuri zaidi ya kuishi; familia zinazoteseka na kudhulumiwa kutokana na imani yao, tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu; familia ambazo zimeathirika kutokana na vita na kinzani za kijamii. Kuna wanawake wanaodhulumiwa na kunyanyaswa utu na heshima yao kutokana na: vipigo, biashara haramu ya binadamu bila kusahau nyanyaso za kijinsia zinazofanywa na watu ambao wamekabidhiwa dhamana ya malezi na makuzi; wanazikumbuka familia zote zinazonyanyasika na ambazo zinakabiliwa na matatizo makubwa.

Mambo yote yanayonesha ile hamu ya kutaka kuwa na utamaduni wa maisha bora, lakini watu hawaguswi na mahangaiko haya. Mababa wa Sinodi wakiwa wameguswa na mahangaiko ya familia zote hizi, wanazitaka Serikali husika na Mashirika ya Kimataifa kusimama kidete kulinda na kutetea haki za familia kwa ajili ya ustawi na mafao ya wengi.

Yesu alitamani kuliona Kanisa lake likiwa na malango wazi kwa ajili ya kuwapokea wote wanaotaka kuingia humo bila ya kumtenga au kumbagua mtu awaye yote. Mababa wa Sinodi wanawashukuru kwa namna ya pekee, wachungaji, waamini na Jumuiya ambazo ziko tayari kuwasindikiza pamoja na kujitwika mzigo wa matatizo ya ndani na yale ya kijamii yanayowakabili wanandoa na familia zao.

Pamoja na mambo yote haya bado kuna mwanga wa matumaini wanasema Mababa wa Sinodi, mwanga unaoendelea kung'ara katika medani mbali mbali za maisha, ili kuupatia moyo joto; ni mwanga unaojionesha kwa wachumba wanapoamua kufunga ndoa ili kushirikishana upendo kati ya bwana na bibi kama unavyosimuliwa kwenye Maandiko Matakatifu, hawa ni watu wanaokamilishana na kusaidiana licha ya tofauti zao msingi.

Hapa ni mwanzo wa safari ya uchumba, kipindi cha kusubiri na kujiandaa kwa makini na kukamilishwa katika maagano ya ndoa yanayotiwa muhuri kwa uwepo na neema ya Mungu. Ni safari inayotambua tendo la ndoa, wema na uzuri unaovuka hata umri wa ujana kwa kutambua kwamba, upendo kwa asili ni jambo linalodumu kiasi hata cha kujisadaka maisha kwa yule anayependwa. Kwa mwanga huu, upendo wa maisha ya ndoa ni wa pekee na usiofutika; unaendelea kudumu licha ya matatizo na mapungufu ya kibinadamu; huu ni muujiza wa pekee na unaogusa watu wengi.

Mababa wa Sinodi wanasema kwamba, upendo huu unadumishwa kwa njia ya mwendelezo wa kizazi kwa kutoa maisha mapya ya Kimungu katika Sakramenti ya Ubatizo; elimu na malezi ya watoto. Ni upendo wenye nguvu ya kutoa maisha, hisia, tunu msingi na mang'amuzi mapana hata kwa wale ambao hawakubahatika kupata watoto. Familia zinazoishi katika ushuhuda wa mwanga huu ni ushuhuda tosha kabisa kwa wengi na hasa zaidi miongoni mwa vijana.

Katika safari hii ya maisha kuna wakati ambapo wanandoa wanajisikia kuchoka na hata wakati mwingine kuanguka chini, lakini watambue kwamba, Mwenyezi Mungu bado anawasindikiza, hali inayojionesha katika majadiliano kati ya wanandoa; kati ya wazazi na watoto wao; kati ya ndugu na jamaa. Uwepo wa Mungu unajidhihirisha kwa kuishi na kutafakari kwa pamoja Neno la Mungu; Sala za familia, pamoja na kufurahia maisha pale nafasi inapopatikana katika siku.

Hapa kuna dhamana endelevu ya kufundana katika imani, maisha mema ya Kiinjili na utakatifu. Utume huu wakati mwingine wanashiriki mabibi na mababu, kiasi cha kuonesha Familia kama Kanisa dogo la nyumbani, inayoendelea na kupanuka kwa kushirikiana na familia nyingine zinazounda Jumuiya ya Kikanisa. Wanandoa Wakristo wanaalikwa kuwa kweli ni walimu wa imani na mapendo kwa wanandoa vijana.

Mababa wa Sinodi wanasema kwamba, kuna umoja na mshikamano wa kidugu unaojikita katika upendo, sadaka na ujirani mwema, kwa kuwajali maskini; wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; wapweke, wagonjwa, wageni na familia ambazo zinajikuta zikikabiliana na kinzani pamoja na migogoro mbali mbali, kwa kusukumwa na Neno la Mungu kwamba, kuna faraja kubwa kutoa kuliko kupokea. Hii ni zawadi kubwa, ni ujirani, ni upendo na huruma na kwamba, ni ushuhuda wa ukweli, mwanga na maana ya maisha.

Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu linaloadhimishwa kila Jumapili ni kusanyiko linalowaunganisha watoto wote na Mungu pamoja na jirani zao ndani ya Kanisa kama Familia ili kwa pamoja kuweza kushiriki meza ya Bwana. Yeye anajisadaka kwa ajili ya wote, mahujaji wanaotembea katika historia ili hatimaye kuweza kukutana na Yesu Kristo atakapokuwa yote katika yote.

Mababa wa Sinodi katika awamu hii ya kwanza wamejadili pamoja na mambo mengine jinsi ya kuzisindikiza familia katika shughuli za kichungaji na maisha ya Kisakramenti kwa wana ndoa walioachana na kuoa au kuolewa tena. Waamini wanaombwa na Mababa wa Sinodi kuendelea kuwasindikiza katika maadhimisho ya Sinodi ya kawaida ya Maaskofu itakayoadhimishwa mwaka 2015.

Mababa wa Sinodi wanaziombea familia zote ulinzi wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu nao wanapenda kusali kwa ajili ya kuwaombea nguvu na hekima ili kweli familia ziweze kuwa na uhuru na umoja; wazazi waweze kupata nyumba ambamo kuna amani na watoto wakiwa kweli ni kielelezo cha imani na matumaini na kwamba, vijana waoneshe ujasiri, uwajibikaji na uaminifu.

Mababa wa Sinodi wanawaombea watu wote ili waweze kupata riziki kwa jasho lao wenyewe; waonje utulivu wa maisha ya kiroho, huku wakiwa na mwanga angavu wakati wa giza la maisha. Mwishoni, Mababa wa Sinodi wanawaombea watu wote kuona Kanisa linalostawi daima likiwa aiminifu na lenye kuaminika; mji wenye haki na utu; dunia inayopenda ukweli, haki na huruma.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.