2014-10-20 11:24:33

Jumuiya ya Kimataifa inashuhudia vitendo vya kigaidi ambavyo havijawahi kutokea hata kidogo!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 20 Oktoba 2014 ameongoza mkutano wa Makardinali, ili kutafakari maombi yaliyowasilishwa kwake na Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu, ili Mwenyeheri Giseppe Vaz na Maria Christina wa Bikira Maria Mkingiwa dhambi ya asili waweze kutangazwa na Mama Kanisa kuwa ni watakatifu. Papa Francisko ametumia fursa hii pia kuzungumzia kuhusu hali Mashariki ya Kati, lakini zaidi kuhusu dhuluma na nyanyaso wanazokabiliana nazo Wakristo huko Mashariki ya Kati.

Baba Mtakatifu anasema, watu wengi wana kiu ya kutaka kuona amani inatawala tena huko Mashariki ya Kati pamoja na utashi wa kutaka suluhu ya kudumu iweze kupatikana ili kumaliza mapambano ya vita kwa kujikita katika majadiliano, upatanisho na utekelezaji wa mikakati ya kisiasa inayoamriwa. Kanisa linapenda kutoa msaada wake kwa Jumuiya za Kikristo huko Mashariki ya Kati, ili kusaidia mchakato wa kuendelea kubaki katika maeneo yao ya asili.

Baba Mtakatifu anasema, haiwezekani kufikiri Mashariki ya Kati bila ya uwepo wa Wakristo, ambao kwa takaribani miaka elfu mbili wameendelea kuungama imani juu ya Yesu Kristo. Matukio ya hivi karibuni huko Iraq na Syria yanasikitisha sana, kwani Jumuiya ya Kimataifa inashuhudia kwa macho makavu vitendo vya kigaidi ambavyo havijawahi kutokea.

Kuna maelfu ya watu wanaodhulumiwa, kiasi kwamba, wanalazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha yao. Hapa inaonekana kana kwamba, utu na heshima ya binadamu havina thamani tena, kiasi hata cha kuwatoa watu wengine sadaka kwa ajili ya mafao binafsi na jambo la kushangaza ni kuona kwamba, watu wengi hawaguswi na mahangaiko ya watu hao.

Baba Mtakatifu anasema hali hii inahitaji waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuendelea kujikita katika sala na kwamba, Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kutoa majibu muafaka. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, mkutano wa Makardinali utasaidia kupata mawazo na majibu yatakayoliwezesha Kanisa kutoa msaada unaohitajika kwa ajili ya Jumuiya za Kikristo huko Mashariki ya Kati, chimbuko la Ukristo!







All the contents on this site are copyrighted ©.