2014-09-02 08:53:35

Kanisa la Nyumbani: uaminifu


Tumsifu Yesu Kristo! Kwa mara nyingine tena karibu katika makala yetu pendevu tuendelee kuhekimishana, na hasa kwa kipindi hiki ambapo tunaitazama familia kama shule ya fadhila na maadili kwa ujumla wake. Nyakati zote, Kanisa linatoa wito kwa wazazi na wote wanaoshika dhamana ya malezi ya watoto kuhakikisha kwamba watoto wanapatiwa malezi stahiki. Hilo ni katika kuchangia kumuunda mtu mwenye kufaa katika jamii ya watu.
Kwa nafasi hii mpendwa msikilizaji, tunakualika tutafakari juu ya fadhila ya uaminifu. Maandiko matakatifu yanausifu uaminifu na mtu mwaminifu anajazwa baraka tele. Mzaburi anatuambia “Mtumishi mwaminifu atasitawi kama mtende, atasitawi vema kama mwerezi wa Lebanoni” anaendelea kusema, “waliopandwa katika nyumba ya Bwana watasitawi katika nyua za Mungu wetu, watajaa utomvu na ubichi, na kuzaa matunda hadi wakati wa uzee” (rej. Zab.92:12-15).
Uaminifu ni nini? Twaweza kusema ni vigumu sana kupata tafanusi sahihi ya uaminifu. Kwa vile ni sanaa inayohusu maisha ya watu, basi tunaweza kuielewa tu katika uwanda wa maisha ya kawaida. Hivyo twaweza kusema kwamba, uaminifu ni sanaa ya maisha ya unyoofu wa akili, moyo na matendo ya kila siku.
Kwa nini hayo matatu yaunganishwe katika uaminifu? Kwa maana chanya, sisi wanadamu wenye akili na utashi, ni kwa akili zetu tunatambua nini tunapaswa kutenda na tunatenda namna gani. Kwa moyo wetu, tunapenda kile tunachokitenda na wale tunaowatendea. Na katika matendo ya maisha yetu, tunadhihirisha kile tunachokijua na tunachokipenda.
Hivyo, ule unyoofu katika fikra (akili), unyoofu katika hisia na unyoofu katika matendo ndiyo uaminifu. Kwa mantiki hiyo tunaweza kusema kwamba kuushi kiaminifu ni kuishi katika ukweli, kuishi katika uhalisia wenye haki. Ni kuenenda pasipo kuleta wasiwasi au mashaka. Uaminifu ni moja ya nguzo muhimu sana za maisha adilifu.
Zamani za wazee wetu, watu walinidhamishwa kwa nguvu sana kuuambata uaminifu kwa sababu waliamini kwa dhati kwamba, uaminifu ni tunu bora kwa maisha ya amani na furaha; uaminifu ni msingi wa mafanikio na maendeleo binafsi na maendeleo ya jamii nzima. Na zaidi sana waliamini kwamba uaminifu ni msingi wa mahusiano mema kati ya jamii ya mwanadamu inayoishi na ulimwengu wa roho.
Ndiyo maana tukichunguza kwa undani jamii zetu mbalimbali, tutakuta kuna aina za viapo vikali ambavyo vilimlazimu mtu kuwa mwaminifu kwa agano au kwa wajibu, ili tu kuweza kuleta mustakhabali wa maisha ya watu. Mtu aliapishwa ili aseme na atende katika unyoofu, aishi katika ukweli wa moyo. Na kuliwekwa adhabu za kisaikolojia na za kimwili ili kumnidhamisha mtu kutunza uaminifu. Adhabu za kisaikolojia ni pamoja na aina ya vitisho juu ya madhara mabaya ya kuvunja uaminifu. Adhabu za kimwili ilikuwa ni pamoja na kutengwa na jamii, mapigo makali au hata kuuawa kwa namna mbalimbali. Hayo yote yalilenga katika kujenga uzito wa tunu ya uaminifu na kuwafanya wote waiambate.
Leo nasi tunahitaji sana fadhila hii ya uaminifu katika jamii zetu. Kwa sababu ya kupuuzia kwa makusudi tunu za kiroho, jamii yetu inateseka sana kwa sababu ya watu kukosa uaminifu katika nyanja zote. Tumejitamadunisha kwa kuishi kijanja-kijanja, huku tulilinda maslahi binafsi zaidi bila kujali mafaa ya jamii. Kukosa uaminifu inaelekea kuwa ndiyo utaratibu sahihi wa maisha. Tazama sasa watu wanavyoteseka, jamii inavyoangamia kwa kupuuza tunu ya uaminifu.
Katika makala hii, tunataka tutafakari na tuiambate tunu hii ya uaminifu katika mapana yake. Sehemu ya kwanza tunataka tuone juu ya uaminifu katika fikra, uaminifu katika maneno (yaani ukweli), uaminifu katika mahusiano, uaminifu katika kazi: kazi binafsi na kazi za umma na uaminifu kwa maisha binafsi. Na sehemu ya pili tutaona pia uaminifu kwa katika mambo ya Kiroho na mambo yamhusuyo Mungu.
Kwa ujumla wake tunaona kwamba, ni kukosa uaminifu ndio kunatufanya tuvunje amri za Mungu, za Kanisa, tukiuke sheria za kiasili, tupuuze miongozo sahihi ya jamii zetu na hata tukiuke kanuni za kazi na kanuni za maisha kwa ujumla. Na matokeo ya kukosa uaminifu ni mahangaiko na mateso. Tukitaka tuwe salama, na tujibidishe katika uaminifu. Na uaminifu huo ujengwe katika mioyo ya watu kuanzia katika familia zetu, mashuleni na kila moja wetu aendelee kujilea katika uaminifu.
Sehemu kubwa ya kushindwa kwetu, kuteseka kwa familia ya mwanadamu, uharibifu wa mazingira ni kwa sababu tu ya kukosa uaminifu. Katika kipindi kijacho tutaendelea kuchambua uaminifu katika nyanja mbalimbali. Kutoka katika Studio za Radio Vaticani, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB









All the contents on this site are copyrighted ©.