2014-08-22 12:25:55

Mabadiliko katika sekta ya afya Nigeria hayalengi kudumisha zawadi ya uhai


Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria halikuridhishwa sana na muswada wa sheria uliopitishwa Bungeni hivi karibuni kuhusiana na masuala ya afya hata baada ya kufanyiwa marekebisho ya msingi, ili kuhakikisha kwamba, wananchi wote wa Nigeria wanapata tiba makini hospitalini bila ubaguzi.

Maaskofu Katoliki Nigeria wanasema muswada huu wa sheria licha ya uzito wake kwa masihai ya wengi, lakini bado kuna vipengele vinavyotishia usalama wa haki ya maisha. Kardinali John Olorunfemi Onaiyekan wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria, akizungumzia kuhusu muswada huu anasema vipengele namba 50, 51 na 52 vinahusika zaidi.

Wafanyakazi katika sekta ya afya pia wameonesha wasi wasi wao kuhusiana na kipengele namba 50 kinachogusia utoaji wa viini tete na masuala mengine ya kimaadili, yanayoweza kupelekea baadhi ya watu kuanza kujiingiza katika biashara haramu ya viungo vya binadamu. Maaskofu wanamshauri Rais Goodluck Jonathan kutia sahihi muswada huu baada ya kufanyiwa marekebisho msingi.

Mabadiliko katika sekta ya afya ni mambo ambayo yamejadiliwa kwa miaka mingi bila mafanikio. Takwimu za Shirika la Afya Duniani zinazonesha kwamba, umri wa wastani wa mtu kuishi nchini Nigeria ni miaka 54. Vifo vya watoto wadogo na wanawake wajawazito bado viko juu sana. NI wanawake asimilia 3% wenye virusi vya Ukimwi ambao wanapata dawa za kurefusha maisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.