2014-07-31 15:19:53

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 18 ya Mwaka A wa Kanisa


Tunakuletea tafakari ya Neno la Mungu Dominika ya 18 ya mwaka A wa Kanisa. Unaalikwa leo kushiriki furaha ya milele ambayo katika neno la leo inalinganishwa na sherehe iliyo kubwa, nzuri na iliyosheheni vyakula vya aina zote. Kwa kushiriki sherehe hii Nabii Isaya anasema hakuna malipo zaidi ya kuwa na mambo mawili yaani njaa na kiu. RealAudioMP3

Kwa jinsi hii mimi mwenyewe lazima nitashiriki kwa maana nimepunguziwa gharama ya malipo isipokuwa nadaiwa kupiga mwendo na kufika kwenye mazingira inapofanyika.

Hata hivyo tunapaswa kujiuliza, hivi leo hii kuna sherehe katika miji, mitaa na vijiji vyetu isiyokuwa na gharama? Kwa hakika naona ni kama hakuna! Kwa maana hiyo huyu anayetualika amepata wapi fedha ya kufadhili sherehe nzima? Tena cha ajabu hakuna idadi kamili ya watu inayohitajika, kwa jinsi hiyo sherehe hii inao uwezo wa kuwakirimu watu wote watakaofika.

Mpendwa unayesafiri pamoja nasi leo, tunakualika sasa upate majibu ya maswali haya katika injili. Tunamwona Mwana wa Mungu anayewalisha watu elfu tano wanaume pasipo kuhesabu wanawake na watoto. Anawalisha kwa mikate mitano na samaki wawili! Hili ni jambo la ajabu machoni petu, limefanywa na Mungu. Katika hali ya kawaida mikate mitano na visamaki viwili visingeweza kutosheleza watu wote, kumbe kuna nguvu ya Mungu toka juu iliyojaa upendo unaoshibisha wana wa Mungu.

Mpendwa msikilizaji, wanapokula wanasaza na vikapu kumi na viwili vinakusanywa, ndiyo kusema kama Mungu akiwa katika maisha yetu daima hatutatindikiwa na kitu chochote. Leo hii, zawadi hii tunapewa kwa njia ya Ekaristi Takatifu mkate wa uzima wa mbinguni, usioisha wala kupungua kwa vizazi vyote. Wajibu wetu si kupeleka pesa kununua bali kuwa na mapendo kwa wenzetu, imani thabiti na maandalizi tafiti moyo yanayokagua uwepo wa neema ya utakaso mioyoni mwetu na matamanio makamilifu mbele ya mkate huu wa uzima wa mbinguni. Matamanio yetu, imani yetu na mapendo kwa wenzetu ndiyo njaa na kiu anayotuambia nabii Isaya.

Mtume Paulo akiona utajiri wa Ekaristi Takatifu, utajiri usiodai gharama ya kifedha bali gharama ya upendo, anaweka mbele yako swali lenye kugusa moyo wako na unapaswa kulijibu kadiri ya mazingira yako. Je, kipi chaweza kututenga na upendo wa Kristu? Kipi chaweza kututenga na Ekaristia? Mtume anatoa mwelekeo, je ni njaa, vishawishi? Hapana.

Natumai wewe ni Baba, Mama, mtoto, mwanafunzi, afisa katika serkali, Kasisi. Je, yepi katika mazingira yako yaonesha kukuvuta ili ujitenge na upendo wa Kristu? Yaone mapema na uanze kujitenga nayo ili uunganike na Kristu aliyemwaga damu pale msalabani kwa ajili yako.

Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwenu na Pd Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.