2014-07-31 08:59:37

Ni mjumbe wa amani, upendo na upatanisho!


Baba Mtakatifu Francisko anasubiriwa nchini Korea kama mjumbe wa amani na wananchi wa Korea ambao kwa takribani miaka hamsini wameendelea kuteseka kutokana na kinzani na mgawanyiko, changamoto ya kuanza mchakato wa kuponya madonda ya utengano kati ya Korea hizi mbili, tayari kujikita katika mchakato wa uponyaji na upatanisho. RealAudioMP3

Ni matumaini yanayooneshwa na Professa Thomas Hong-soon Han wa masuala ya siasa za uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Hankuk, ambaye amewahi pia kuwa Balozi wa Korea mjini Vatican, katika mahojiano maalum na Jarida la “La Gregoriana” linalochapishwa na Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregoriani, kilichoko mjini Roma.

Profesa Thomas anasema, wananchi wa Bara la Asia wanamsubiri kwa hamu kubwa Baba Mtakatifu Francisko, ili kushirikishana ile Furaha ya Injili. Kutokana na ushawishi wake mkubwa katika masuala ya Mafundisho Jamii ya Kanisa, Professa Thomas alifaulu kuanzisha Chuo cha Mfundisho Jamii ya Kanisa nchini Korea, chuo ambacho kinachngia kwa kina katika demokrasia na maendeleo ya wananchi wote wa Korea.

Anasema, Mafundisho Jamii ya Kanisa ni mchango mkubwa unaotolewa na Mama Kanisa kwa ajili ya kutafuta mafao ya wengi, utu na heshima ya binadamu pamoja na maendeleo endelevu ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Bara la Asia lina kiu ya haki na amani, upendo na mshikamano wa kweli. Katika miaka ya hivi karibuni, Bara la Asia limeendelea kucharuka katika uchumi na maendeleo ya vitu, lakini limeendelea kutopea katika uvunjaji wa haki msingi za binadamu.

Ni sehemu ambayo ina kinzani kubwa za kidini kutokana na baadhi ya waamini kuwa na misimamo mikali ya kidini ambayo haina tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya watu husika. Bara la Asia linakabiliwa na uchafuzi mkubwa sana wa mazingira, hali inayopelekea pia uwepo mkubwa wa maskini na watu wanaoshambuliwa na magonjwa.

Professa Thomas anasema, Mafundisho Jamii ya Kanisa yanawasaidia waamini na wananchi katika ujumla wao kutolea ushuhuda wa tunu msingi za maisha ya mwanadamu na kwamba, Imani kwa Kristo na Kanisa lake si jambo linalotishia ustawi na maendeleo ya wananchi wa Bara la Asia, bali ni kikolezo kikuu cha utu na heshima ya binadamu pamoja na mafao ya wengi.

Korea na Vatican, Desemba 2013 wameadhimisha Jubiulee ya Miaka 50 ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya pande hizi mbili. Katika kipindi chote hiki, Vatican imeendelea kushirikiana na Korea katika medani mbali mbali za maisha, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wanachi wa Korea. Kazi kubwa kwa sasa ni kusaidia utekelezaji wa mchakato wa upatanisho kati ya Korea ya Kusini na Korea ya Kaskazini, ili wote waweze kujisikia kuwa ni watu wa taifa moja








All the contents on this site are copyrighted ©.