2014-07-28 10:30:10

Miaka 45 tangu kuanzishwa kwa SECAM


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, tarehe 27 Julai 2014 limeadhimisha kumbu kumbu ya miaka 45 tangu SECAM ilipoanzishwa kwa mara ya kwanza wakati Mtumishi wa Mungu Paulo VI alipotembelea Uganda kunako mwaka 1969. Hili lilikuwa ni tukio la kihistoria kwani ni kwa mara ya kwanza kabisa Khalifa wa Mtakatifu Petro alikuwa anatembelea Bara la Afrika.

Leo hii SECAM inaundwa na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki kitaifa yapatayo 37 yanayowakilishwa na Mashirikisho ya Mabaraza ya Maaskofu Kikanda yapatayo 8, kati yake ni AMECEA, lililohitimisha mkutano wake wa kumi na nane uliokuwa unafanyika mjini Lilongwe, nchini Malawi.

Kwa mara ya kwanza katika historia, Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, limeadhimisha kumbu kumbu ya miaka 45 tangu kuanzishwa kwake, kwa kusali kwa ajili ya kuliombea Kanisa la Kiulimwengu, lakini zaidi kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa Barani Afrika. SECAM pamoja na mambo mengine inapania kuwa na mwono wa pamoja kuhusu Kanisa Barani Afrika, dhana ambayo imekuwa na kukomaa kutokana na changamoto zilizotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Bara la Afrika linatambua utajiri mkubwa unaofumbatwa katika lugha, mila, desturi na tamaduni mbali mbali zinazopatikana Barani Afrika, lakini hata hivyo bado linahamasishwa kujenga na kudumisha umoja na mshikamano wa Kanisa Barani Afrika, ili kwa pamoja Familia ya Mungu inayowajibika Barani Afrika iweze kujikita katika mchakato wa Uinjilishaji mpya unaojikita katika utamadunisho, upatanisho, haki na amani, mambo ambayo Kanisa Barani Afrika linapenda kuyavalia njuga kama sehemu ya mikakati yake ya Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kanisa Barani Afrika linatambua umuhimu wa kuendeleza majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kweli amani na maendeleo ya watu yaweze kupatikana. Kanisa Barani Afrika litaendelea kujielekeza zaidi na zaidi katika Uinjilishaji wa awali kwani bado kuna umati mkubwa wa watu ambao bado haujabahatika kusikiliza Injili ya Furaha.

Dhamana hii inapaswa kutekelezwa kwa njia ya ushuhuda wa imani inayomwilishwa katika matendo, ili kweli Ukristo uweze kuwa na mashiko na mvuto kwa watu wa nyakati hizi sanjari na kuimarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia na kwamba Bara la Afrika si dodoki linalokusanya kila aina ya takataka zinazotolewa na vyombo vya habari. Bara la Afrika lina mila, tamaduni na maadili yake yanayopaswa kulindwa na kuendelezwa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa Barani Afrika.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.