2014-07-25 10:08:26

Utu na utakatifu wa maisha ya binadamu ni mambo nyeti!


Kardinali Timothy Michael Dolan wa Jimbo kuu la New York, Marekani katika tafakari yake kuhusu mateso na mahangaiko ya wahamiaji na wakimbizi nchini Marekani anasema kwamba, kuna haja ya Jamii kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu. Hivi karibuni ameshuhudia umati mkubwa wa wananchi waliokuwa na hasira wamezunguka Bus lililokuwa limewabeba wahamiaji, wakimbizi na omba omba wa mjini Calfornia, wakipiga kelele kutaka waondolewe mara moja kutoka mjini humo!

Jambo hili limemfadhaisha sana Kardinali Dolan kwani ni kitendo ambacho ni kinyume kabisa cha utu na heshima ya binadamu; ni kitendo kinachosigana na Maandiko Matakatifu. Wananchi waliokuwa na hasira walifanikiwa kwani Madreva waliokuwa wanaendesha Mabus hayo, waliogopa na kutafuta hifadhi sehemu nyingine. Kwa watu wenye umri mkubwa wanakumbuka unyama kama huu waliotendewa wahamiaji na wageni waliokuwa wanatafuta hifadhi nchini Marekani.

Wananchi wengi wa Marekani wanasahau kwamba, wengi wao ni wahamiaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia, waliofika nchini humo wakiwa wamegubikwa na baa la njaa na umaskini, lakini wakiwa na tumaini la maisha bora zaidi.

Mjini Texas, Marekani hali ni tofauti kabisa, wananchi wanaonesha upendo na ukarimu kwa wahamiaji na wageni waliofika kwenye Parokia ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Wafanyakazi wa Serikali walitekeleza wajibu wao kwa utaratibu pasi na makelele, jambo ambalo anasema Kardinali Dolan, limemfurahisha na kumpatia faraja. Hapa inaonesha umuhimu wa kusimama kidete kulinda, kutetea utu, heshima na utakatifu wa maisha ya binadamu. Ni jambo la fedhehesha sana kuwashambulia watu wenye shida wanaohitaji kuonjeshwa huruma na upendo!







All the contents on this site are copyrighted ©.