Ndoa za shuruti na ukeketaji ni nyanyaso kwa wasichana na wanawake!
Shirika la kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF linaonesha kwamba, kuna wanawake
millioni 700 wamelazimika kufunga ndoa za shuruti, wakiwa katika umri mdogo na kati
yao kuna wanawake millioni 250 waliofunga ndoa wakiwa na umri chini ya miaka kumi
na mitano. Hii ni sawa na asilimia 35%.
UNICEF imeyasema haya katika maadhimisho
ya mkutano wa watoto unaoendelea Jijini London kwa kusema kwamba, wasichana wanaoolewa
chini ya umri wa miaka kumi na minane wako hatarini ya kukumbana na nyanyaso katika
familia zao. Wasichana katika umri huu, wengi wao hupoteza maisha wakati wa kujifungua,
kuliko wanawake wanaoamua kuolewa wakiwa na umri zaidi ya miaka ishirini. UNICEF inasema
kwamba, kuna wanawake zaidi millioni 130 katika nchi 29 kutoka Barani Afrika na Mashariki
ya Kati ambao wamekeketwa.
UNICEF inapenda kuwasaidia wanawake kulinda na
kutetea utu na heshima yao kwa kupinga ndoa za utotoni pamoja na kukomesha vitendo
vya ukeketaji ambavyo wataalam wa afya wanasema vina madhara makubwa kwa wanawake.