Kardinali Angelo Scola, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Milano, Kaskazini mwa Italia anapenda
kuungana na Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini kuwatakia kheri na baraka waamini
wa dini ya Kiislam wanapoadhimisha Siku kuu ya Id Al Fitr inayokuja mara baada ya
Mfungo mkutukufu wa Mwezi wa Ramadhani, kipindi cha kufunga, swala na msaada kwa maskini.
Kardinali
Scola anasema Wayahudi, Wakristo na Waislam wote ni watoto wa Mwenyezi Mungu na kwamba,
wanapaswa kujitambua kuwa wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, kumbe ni ndugu
wamoja, wanawajibika kujisadaka kwa ajili ya Jumuiya zao za Kidini na Jamii katika
ujumla wake.
Ni matumaini ya Kardinali Scola kwamba, waamini wa dini mbali
mbali wataendelea kushirikiana, kushikamana, kufahamiana na kusaidiana ili kukabiliana
na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika ulimwengu mamboleo. Kwa namna ya pekee,
anapenda kuwakumbuka waamini wa dini ya Kiislam kutoka nchi mbali mbali wanaoishi
na kufanya kazi Jimbo kuu la Milano.
Anakumbuka nchi walikotoka waamini hao,
lakini zaidi katika nchi zile ambazo amani inateteleka, kuna kinzani za kijamii, kisiasa
na kiuchumi na kwamba, watu wana kiu ya kuona kwamba, haki inatendeka; nyanyaso na
dhuluma zinatoweka katika uso wa dunia. Kwa namna ya pekee, Kardinali Scola anaungana
na Baba Mtakatifu Francisko kusema tena kwamba, amani inaweza kupatikana tu kwa njia
ya majadiliano na wala si kwa njia ya mtutu wa bunduki kama wanavyodhani watu wengi
kwa sasa.
Ufuatao ni ujumbe wa Id Al Fitri kutoka kwa Baraza la Kipapa la
Majadiliano ya kidini ambao utasambazwa kwa waamini wa dini ya Kiislam katika nyumba
za Ibada wakati wa Siku kuu ya Id Al Fitri.
Itakumbukwa kwamba, kunako Mwaka
2013, Baba Mtakatifu Francisko alipokuwa anaanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu
Petro aliandika ujumbe wa matashi mema kwa waamini wa dini ya Kiislam katika maadhimisho
ya Siku kuu ya Id Al Fitr kuonesha upendo na mshikamano wake kwa waamini wa dini ya
Kiislam kama ndugu, maneno ambayo yana maana sana! Hii inatokana na ukweli kwamba,
Waislam na Wakristo ni ndugu wamoja wanaounda Familia moja ya binadamu iliyoumbwa
na Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo.
Waamini wa dini hizi mbili
kwa pamoja wanaungama imani kwa Mungu mmoja Muumbaji wa binadamu na kwamba, wanautukuza
ukuu wa Mungu kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu. Wanamwabudu
na kujiweka miguuni pa Mwenyezi Mungu, kiasi hata cha kuthubutu kuitana ndugu katika
imani kwa Mungu mmoja. Ni maneno yaliyotolewa na Mtakatifu Yohane Paulo II kunako
mwaka 1982 alipokutana na viongozi wa kidini mjini Kaduna, Nigeria.
Baraza
la Kipapa la majadiliano ya kidini linasema, kwa pamoja waamini wa dini hizi mbili
wanamwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa mambo yale yanayowaunganisha
pamoja na kutambua tofauti zao msingi. Kuna haja ya kuendeleza majadiliano ya kidini
yanayojikita katika hali ya kuheshimiana pamoja na urafiki; kwa kusimamia tunu msingi
za udugu, ili kwa pamoja waweze kufanya kazi ya kuendeleza haki na amani; kwa kuheshimu
utu na haki msingi za kila binadamu.
Wakristo na Waislam wanatambua kwamba,
kimsingi wanawajibika kuwasaidia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii:
wagonjwa, yatima, wahamiaji, wahanga wa biashara haramu ya binadamu, waathirika wa
matumizi haramu ya dawa za kulevya na ulevi wa kupindukia. Masuala yote haya ni changamoto
kubwa katika kujenga na kudumisha mshikamano miongoni mwa watu wenye mapenzi mema.
Ni changamoto inayotishia uharibifu wa mazingira, myumbo wa uchumi kimataifa na ukosefu
wa fursa za ajira na hasa zaidi miongoni mwa vijana wa kizazi kipya.
Mambo
haya yanawafanya watu kunyong'onyea kiasi cha kukosa matumaini kwa kesho iliyo bora
zaidi. Waamini hawawezi kamwe kusahau matatizo yanayoziandamana familia kwa kutengana
na kuwaacha watoto wadogo katika shida na mahangaiko makubwa. Kumbe, kuna haja ya
kufanya kazi kwa pamoja, ili kujenga madaraja ya amani na upatanisho hasa katika maeneo
ambayo Waislam na Wakristo ni wahanga wa vita. Urafiki kati ya waamini wa dini hizi
mbili usaidie mchakato wa ushirikiano ili kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali
kwa ajili ya mafao ya wengi.
Upatanisho, haki, amani na maendeleo ni kati
ya vipaumbele vya waamini wa dini hizi mbili kwa ajili ya mafao ya Familia ya binadamu.
Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini, likiwa limeungana na Baba Mtakatifu Francisko
linapenda kuwapatia salam na matashi mema waamini wote wa dini ya Kiislam katika Siku
kuu ya Id al Fitr; heri, fanaka na amani.