2014-07-23 11:08:52

Yataka moyo kweli kweli kuwa Mkristo!


Askofu Giorgio Bertin wa Jimbo Katoliki la Djibouti na Msimamizi wa kitume wa Jimbo kuu la Mogadisho, Somalia anasema, yataka moyo kweli kweli kuwa Mkristo nchini Somalia na kusimama kidete ili kuwa ni sauti ya wanyonge, kwa kutetea utu na heshima ya binadamu. Ukijifanya kutekeleza dhamana ya Kanisa kwamba ni sauti ya wanyonge, ukafumbwa mdomo na kuamriwa kuondoka nchini Somalia kwa mwendo wa kunyakua!

Askofu Bertin ambaye tangu mwaka 2001 anaishi na kutekeleza utume wake Jimboni Djibouti anasema, hali ni shwari kwa kiasi fulani. Serikali inaonekana kutekeleza wajibu wake wa ulinzi na usalama na kwamba, wananchi wa Djibout wanaliheshimu na kulipenda Kanisa. Kutokana na woga uliofichika katika mioyo ya watu, kunaonekana kana kwamba, kuna amani na utulivu, lakini ukweli wa mambo unaonesha kwamba, watu ni waoga kudai haki zao msingi, kwani wanahofia kufungwa mdomo na kutoweka katika uso wa dunia.

Takwimu zinaonesha kwamba, Wakristo ni asilimia 6% ya idadi ya wananchi wa Djibouti na wengine wote ni waamini wa dini ya Kiislam, changamoto kubwa ni kuendeleza majadiliano ya kidini, ili kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na udugu kati ya watu.

Umaarufu wa Kanisa unatokana na huduma makini zinazotolewa na Kanisa katika sekta ya elimu, afya na maendeleo ya watu: kiroho na kimwili. Serikali imeridhishwa na mchango wa Kanisa katika sekta ya elimu kiasi kwamba, imeridhia kulipa mishahara ya walimu kwa shule nne zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa kama alama ya shukrani kwa mchango wa Kanisa katika maendeleo ya wananchi wa Djibouti. Inasikitisha kuona kwamba, kiwango cha miito ni duni sana, kiasi kwamba, Jimbo linahudumiwa kwa kiasi kikubwa na Mapadre kutoka nje ya nchi.







All the contents on this site are copyrighted ©.