Silaha na nishati ya nyuklia bado ni tishio kwa usalama wa binadamu!
Baraza la Makanisa Ulimwenguni, WCC linaendelea kuihamasisha Jumuiya ya Kimataifa
kusitisha utengenezaji, ulimbikizaji na matumaini ya silaha za kinyuklia ili kuiokoa
dunia kutokana na hofu ya maafa makubwa yanayoweza kujitokeza kutokana na matumizi
ya silaha za kinyuklia.
Ushuhuda
unaoendelea kutolewa na wahanga wa mashambulizi ya silaha za kinyuklia Nagasaki na
Hiroshima kunako mwaka 1945 na kuvuja kwa mtambo wa nyuklia wa Fukushima kunako mwaka
2011 unaoendelea kuongeza hofu na wasi wasi kwa Jumuiya ya Kimataifa.
Baraza
la Makanisa Ulimwenguni linayataka Makanisa wanachama kuendesha kampeni dhidi ya utengenezaji
wa silaha za kinyuklia inayoongozwa na kauli mbiu “Ulimwengu pasi na silaha za Kinyuklia”.
Makanisa yanapaswa kupambanua kwa kina na mapana, kimaadili na kitaalimungu athari
za matumizi ya silaha na nishati za kinyuklia.
Waoneshe ushuhuda unaotolewa
na wadau mbali mbali kuhusiana na matumizi ya nishati ya kinyuklia pamoja na kuendelea
kutoa ushawishi wa kuridhia upigaji rufuku wa utengenezaji, matumizi na ulimbikizaji
wa silaha za kinyuklia duniani. Baraza la Makanisa Ulimwenguni linayahimiza Makanisa
wanachama kufanya mabadiliko ya ndani katika maisha yao, kwa kutumia nishati rafiki
ili kulinda na kutunza mazingira.
Baraza la Makanisa ulimwenguni linabainisha
kwamba, matumizi ya nishati ya kinyuklia ni hatari kwa usalama na maisha pamoja na
maendeleo ya binadamu. Serikali mbali mbali zinazoendeleza sera ya matumizi ya nishati
ya kinyuklia zinahatarisha ustawi wa wengi kwa kutumia rasilimali fedha ya umma kwa
ajili ya kuendeleza sekta binafsi.