2014-07-18 09:10:49

Pasi na familia hakuna ustawi wala maendeleo!


Utamaduni unaosimikwa katika ubinafsi na uchoyo ni kati ya mambo yanayochangia kuporomoka kwa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Kumbe, kuna haja kwa Mama Kanisa kujifunga kibwebwe kuhakikisha kwamba, Familia inapewa kipaumbele cha kwanza katika mikakati, maisha na utume wa Kanisa.

Hii ni changamoto ambayo imetolewa hivi karibuni na Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la familia wakati wa maadhimisho ya mkutano mkuu wa kumi wa Shirikisho la Mabaraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kati, ACERAC lililokuwa linakutana huko Brazzaville, Congo.

Askofu mkuu Paglia anasema, Bara la Afrika linakabiliwa na changamoto nyingi kuhusiana na maisha na utume wa Familia, kiasi cha kupindisha hata mpango na utashi wa Mungu katika maisha ya mwanadamu. Hii ni changamoto ya kiimani na kimaadili inayopaswa kufanyiwa kazi kwa kina na mapana, ili kujikita katika maendeleo ya kweli yanayoheshimu misingi ya utu na heshima ya binadamu.

Kuna mmong'onyoko mkubwa wa tunu bora za kimaadili na utu wema; umoja, upendo na mshikamano katika maisha ya ndoa kwa sasa uko mashakani kutokana na ubinafsi na kwamba, ule mshikamano wa kifamilia uliokuwepo Barani Afrika kwa miaka mingi unaendelea kuyeyuka kwa kasi kubwa.

Tatizo jingine linaloibuka kwa sasa ni ukosefu wa uaminifu katika maisha ya ndoa na familia, kiasi kwamba, kuna baadhi ya wanandoa wanadhani "kuchepuka" ni suluhu ya matatizo wanayokabiliwana nayo katika ndoa zao, kumbe, hapa wanaendelea kujichumia majanga binafsi na kwa ajili ya familia zao. Umaskini na ukosefu wa fursa za ajira ni changamoto kubwa kwa familia nyingi Barani Afrika, kiasi cha kuwafanya wazazi na walezi kushindwa kutekeleza dhamana kwa familia zao.

Ikumbukwe kwamba, Familia Barani Afrika daima imekuwa ni shule ya kwanza katika kurithisha tunu msingi za maisha ya imani, maadili na utu wema, lakini kwa sasa dhamana hii iko hatarini kupokwa na vyombo vya mawasiliano ya kijamii!

Askofu mkuu Paglia anasema, umefika wakati kwa familia kujenga na kuimarisha misingi ya ndoa na familia; kwa kukuza mahusiano bora ndani ya Jamii, ili kujenga mshikamano wa upendo kati ya wazee, vijana na watoto. Hii ni changamoto ya Kanisa zima na wala si tu kwa ajili ya Kanisa Barani Afrika.

Baba Mtakatifu Francisko kwa kutambua fursa, changamoto na kinzani zinazoendelea kuiandama Familia, ameamua kuitisha Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia itakayoadhimishwa mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014. Kutakuwepo na awamu ya pili ya maadhimisho haya itakayofanyika mwaka 2015.

Hii ni changamoto kwa Serikali, taasisi, wanasiasa, wachumi na watunga sera kufuata mfano wa Kanisa Katoliki katika kulinda, kutetea na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Familia iwe ni kiini cha mawazo na sera makini kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.