Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II wanashiriki utakatifu mmoja!
Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanabainisha kwamba, utakatifu ni wito na
changamoto kwa kila mwamini na kwamba, wote wanaitwa kuwa wakamilifu kama Baba yao
wa mbinguni alivyo mkamilifu. Wenyeheri Yohane wa XXIII na Yohane Paulo II ni viongozi
wa Kanisa waliojitahidi kutekeleza utakatifu mmoja, kwa njia ya nyajibu zao, huku
wakiongozwa na Roho wa Mungu, kwa njia ya utii na ibada katika roho na kweli!
Miamba
hawa wa Kanisa walijitahidi kumfuasa Yesu Kristo: mtii,fukara na mnyenyekevu aliyeonesha
njia ya utakatifu wa maisha kwa Fumbo la Msalaba, ili aweze kuwastahilisha kushiriki
utukufu wake. Hawa ni watu ambao kwa njia ya ushuhuda wa imani hai na tendaji, walionesha
imani, matumani na mapendo kwa Kristo na Kanisa lake.
Askofu mkuu Vincenzo
Bertolone wa Jimbo kuu la Cantanzaro- Squillace, Italia ndivyo anavyochambua utakatifu
wa Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II; viongozi wakuu wa Kanisa waliojitahidi
kusoma alama za nyakati na hivyo kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa
katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Ni viongozi waliojitahidi kudumisha
majadiliano na walimwengu kwa njia ya mwanga na kweli za Kiinjili, ili kumpeleka Kristo
kati ya watu na watu kwa Kristo.
Watu mbali mbali walishuhudia na kuonja utakatifu
wa maisha ya Mwenyeheri Yohane Paulo II katika maisha na utume wake. Ni kiongozi aliyesimama
kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; uhuru wa kweli; haki, amani
na maendeleo ya binadamu. Alivunjilia mbali kuta za utengano kati ya watu na leo hii
anakumbukwa kuwa ni kati ya viongozi waliosambaratisha ukomunisti duniani.
Mwenyeheri
Yohane Paulo II alilitaka Kanisa kujikita katika Uinjilishaji Mpya, ili watu wanaotembea
katika mwanga na kweli za Kiinjili waweze kutolea ushuhuda wao kwa Kristo na Kanisa
lake. Alikazia na kusisitiza umuhimu wa Mafundisho Jamii ya Kanisa kama njia ya kuyatakatifuza
malimwengu. Alionesha kwamba, hakuna ukinzani wala mpasuko kati ya imani na uwezo
wa mwanadamu wa kufikiri na kutenda, bali jambo la msingi ni kutambua na kukiri uwepo
wa Mungu ambaye ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho wa yote!
Mwenyeheri Yohane
Paulo wa Pili, anakumbukwa na wengi kwa kuhimiza utakatifu wa maisha ya ndoa na familia
na kwamba, Familia za Kikristo zinapaswa kuwa kweli ni shule ya utakatifu, haki na
amani; upendo na mshikamano. Hapa ni mahali pa kwanza ambapo mwanadamu anajifunza
tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema
wakizingatia dhamana na utume wa Familia, wanaweza kukabiliana na changamoto za maisha
ya ndoa na familia kwa ujasiri na moyo mkuu!