2014-04-23 15:04:43

Kwa nini mnamtafuta aliye hai katika wafu?


Maelfu ya waamini pamoja na mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia, asubuhi na mapema siku ya Jumatano tarehe 23 Aprili 2014, waliwahi kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ili kusikiliza katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko wakati huu wa Kipindi cha Pasaka. Baba Mtakatifu katika katekesi yake ameuliza swali la msingi "kwa nini mnamtafuta aliye hai katika wafu?

Baba Mtakatifu Francisko anasema, furaha ya Siku kuu ya Pasaka inapata chimbuko lake katika imani kwa Ufufuko wa Yesu Kristo sanjari na uwepo wake endelevu ndani ya Kanisa na katika Ulimwengu. Kwa njia ya Ufufuko, yote yamefanywa kuwa upya. Swali ambalo wanawake waliulizwa siku ile ya Pasaka ni swali ambalo Mama Kanisa anapenda kuwaswalisha watoto wake, kwa nini mna mtafuta aliye hai katika wafu?

Baba Mtakatifu anasema, Injili inatoa mifano mitatu ya watu waliokutana na Yesu, wakaonja mabadiliko katika maisha yao ya kiroho, mwaliko na changamoto hata kwa waamini wa nyakati hizi. Kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Toma, waamini wana shauku ya kutaka kuona ukweli wa maisha mapya yanayobubujika kutoka kwa Kristo mfufuka. Kama ilivyokuwa kwa Maria Madgalena, waamini wanapenda kusikia sauti ya Yesu Mfufuka ikiwaita kwa majina yao!

Baba Mtakatifu Francisko anasema kama ilivyokuwa kwa wanafunzi wa Emmaus waliokuwa wanasafiri, waamini pia wanataka kuonja furaha na matumaini mapya kwa kutambua kwamba, Yesu anaendelea kutembea pamoja nao. Wafuasi wa Emmaus walikuwa wanafikiri uwepo wa Yesu kati ya wafu, akawaongoza kwa njia tofauti katika imani na nguvu yake ya ufufuko.

Leo hii, waamini wanachangamotishwa kumtafuta Yesu aliyefufuka kutoka katika wafu kwa kuachana na mambo yote ambayo ni kizingiti cha kutaka kukutana na Yesu, ili kupata maisha mapya, uhuru wa kweli unaoweza kutolewa na Yesu mwenyewe.

Baba Mtakatifu ametambua uwepo wa Mashemasi wapya kutoka Chuo Kikuu cha Kipapa cha Ireland waliokuwa wameambatana na wazazi, ndugu na jamaa zao. Amewaambia waamini kwamba, Kristo ndiye aliyeshinda dhambi na mauti, anayewaalika waamini kujiachilia mikononi mwake, ili awawezeshe kupata matumaini na ukamilifu wa maisha!

Baba Mtakatifu Francisko ametumia fursa hii kuwashukuru wote waliomtumia salam na matashi mema kwa Siku kuu ya Pasaka na siku ya Jumatano tarehe 23 Aprili 2014 anapofanya kumbu kumbu ya Mtakatifu somo wake. Anawashukuru wote wanaoendelea kumsindikiza kwa sala na sadaka zao katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, Jumapili ijayo, Jimboni Alba, Kaskazini mwa Italia, Kanisa litamtangaza Mtumishi wa Mungu Padre Giuseppe Giroti kuwa Mwenyeheri. Aliuwawa na Jeshi la Wanazi kutokana na chuki za kiimani. Mfano wa maisha ya Mwenyeheri Giuseppe Giroti ulete mwamko na ari miongoni mwa waamini kutaka kujishikamanisha na Kristo pamoja na Injili yake. Ametambua uwepo wa vijana kutoka Jimbo kuu la Milano ambao wako mjini Roma kwa ajili ya kukiri imani yao kwa miamba ya imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.