2014-04-23 10:04:06

Jiepusheni na utumwa mamboleo!


Kardinali Thèodoro Adrien Sarr, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dakar, Senegal katika ujumbe wake kwa Kipindi cha Pasaka kwa Mwaka 2014 anasema kwamba: uchu wa mali na madaraka; matumizi haramu ya dawa za kulevya; ulevi wa kupindukia, ukahaba na ngono ni kati ya mambo makuu yanayowatumbukiza watu wengi katika biashara ya utumwa mamboleo. Nyakati za Siku kuu si muda wa kutenda dhambi kwa kujiachia ili kumezwa na malimwengu.

Kardinali Sarr anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujitahidi kuishi maisha yanayoongozwa na kanuni msingi za maadili na utu wema; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi; umoja, upendo na mshikamano wa kitaifa. Anawaalika watu kuondokana na imani za kishirikina na nguvu za giza zinazowasababishia hofu na mashaka katika maisha; uchu wa mali na madaraka unaowatumbukiza wengi katika vita na migongano ya kiuchumi na kijamii.

Pasaka kiwe ni kipindi muafaka cha waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema kujiondoa kabisa katika utumwa mamboleo unaowatmbukiza katika majanga ya maisha, ukosefu wa haki msingi za binadamu na matokeo yake ni watu kutokomea katika upweke hasi unaoweza kuwasababishia kifo. Wakristo wanachangamotishwa kuhakikisha kwamba, wanaziishi katika ukamilifu ahadi zao za Ubatizo, kwa kumpatia Mwenyezi Mungu kipaumbele cha kwanza sanjari na kupendana wao kwa wao badala ya kuangaliana kwa "macho ya makengeza".







All the contents on this site are copyrighted ©.