2014-04-23 08:21:45

Hija ya kichungaji ya Papa Francisko, nchini Korea


Maandalizi ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko Korea ya Kusini kuanzia tarehe 14 hadi tarehe 18 Julai 2014 yanayoongozwa na kauli mbiu “Ondoka, uangaze kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa Bwana umekuzukia” sanjari na Siku ya sita ya Vijana Barani Asia yanaendelea vyema. Itakumbukwa kwamba, Papa Yohane Paulo II alifanya hija ya kichungaji Korea ya Kusini, yapata miaka ishirini na mitano iliyopita. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika wananchi wa Korea katika ujumla wao, kusimama kifua mbele kama mawimbi na kuangaka kama miale ya moto! Hija ya kichungaji pamoja na mambo mengine ni changamoto ya kudumisha mchakato wa upatanisho kati ya Korea ya Kaskazini na Korea ya Kusini, ili kweli amani na utulivu viweze kutawala.

Nembo la hija ya hija hii ya kichungaji inaviashiria vya sadaka kubwa iliyotolewa na Mashahidi 124 wa Korea waliomimina maisha yao kwa ajili ya imani kwa Kristo na Kanisa lake kati ya Mwaka 1791 na Mwaka 1888. Kimsingi, hija ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Korea ya Kusini, Jimboni Daejeon ni kushiriki katika maadhimisho ya Siku ya sita ya Vijana Barani Asia, inayowataka vijana kuondoka na kuangaza, kwani utukufu wa Mashahidi utawang’aria pamoja na kuwatangaza watumishi wa Mungu 124 kuwa ni Wenyeheri.

Papa Yohane Paulo II alipotembelea nchini Korea, alipata fursa ya kuwatangaza wenyeheri 103 kuwa ni Watakatifu na Mashahidi wa Kanisa. Kati yao kuna Mtakatifu Andrea Kim Tae-gon, Padre wa kwanza mzalendo kutoka Korea. Katika miaka ya hivi karibuni, Kanisa Barani Asia limeendelea kukua na kuongezeka maradufu, ingawa bado lina idadi ya waamini wachache ikilinganishwa na dini kubwa Barani Asia.

Kanisa nchini Korea linaendelea kukua na kupanuka na kwa sasa takwimu zinaonesha kwamba, lina jumla ya waamini wapatao millioni tano, sawa na asilimia 10% ya idadi ya wananchi wote wa Korea.








All the contents on this site are copyrighted ©.