2014-04-22 09:58:13

Miaka 20 ya uhuru na demokrasia ya kweli Afrika ya Kusini


Wananchi wa Afrika ya Kusini wanaendelea kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa kuadhimisha kumbu kumbu ya Miaka 20 tangu walipojipatia uhuru na demokrasia kamili, kwa ajili ya mafao, ustawi na maendeleo ya wananchi wote wa Afrika ya Kusini pasi na chachu ya ubaguzi wa rangi. Haya ni mafanikio ambayo yamegharimu maisha ya wananchi wengi wa Afrika ya Kusini.

Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini kwa namna ya pekee, linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuunganika pamoja na kusali, hapo tarehe 27 Aprili 2014 kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kuwapatia demokrasia ya kweli katika kipindi cha miaka 20 iliyopita. Wanapenda kumwomba, ili awasaidie kuimarisha haki, uhuru, upendo na mshikamano wa kitaifa

Wananchi wa Afrika ya Kusini wamwombe Mwenyezi Mungu, huruma na msamaha kwa mapungufu yote yaliyojitokeza katika kipindi hiki sanjari na kuomba neema na mapendo ya Mungu kwa wananchi wote wa Afrika ya Kusini. Wanaposali na kuomba, wananchi pia wajibidishe zaidi na zaidi katika kukuza na kudumisha uzalendo, umoja na udugu kwa kutekeleza nyajibu zao kama raia wema, hasa nyakati za uchaguzi, ili kweli Afrika ya Kusini iweze kupata viongozi wema na waadilifu, watakaosimamia misingi ya ukweli, haki, amani na mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.