2014-04-21 10:24:38

Simameni kidete kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya haki na amani!


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anasema ujumbe ambao angependa kuipatia Familia ya Mungu Afrika Mashariki ni kutaka kuwakumbusha kwamba, Pasaka ni kipindi cha mpito kutoka katika hali duni na kuingia katika hali bora zaidi ya maisha, kama vile Kristo alivyojinyemnyekeza na kujishusha, akawa binadamu na kujitwalia hali ya utumishi, akateswa na kufa Msalabani. RealAudioMP3

Yesu kwa njia ya utii kwa Baba yake wa mbinguni, Mwenyezi Mungu amemkirimia jina linalopita majina yote. Kristo ameshinda mauti na kifo, amefufuka ni mtukufu. Hivyo basi, Pasaka ya Kristo iwe ni Pasaka ya waamini wote kwa kuondokana na uzembe wa maisha ili kuanza kuzingatia kweli za Kiinjili kama sehemu ya mchakato wa mwendelezo wa kazi ya ukombozi iliyoanzishwa na Kristo mwenyewe.

Upya huu wa maisha unapaswa kujikita katika ushuhuda wa maisha yenye mvuto wa Kimungu, ili watu wamkimbilie Mungu kupata baraka, faraja na neema zitakazowasaidia kuwa watu wapya kweli kweli!

Naye Askofu Augustino Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar katika mahojiano na Radio Vatican anasema ujumbe wa Pasaka kwa Mwaka 2014 ni amani inayobubujika kutoka kwa Kristo aliyeshinda kifo, dhambi na ubaya, ili kumkirimia mwanadamu mwanga mpya na utimilifu wa maisha ya binadamu. Ufufuko wa Kristo ni chemchemi ya amani kwa binadamu wote. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanachangamotishwa na Mama Kanisa: kulinda, kutetea na kudumisha msingi ya haki na amani duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.