2014-04-15 08:07:17

Usawa, unyofu na mshikamano ni kanuni msingi katika mapambano dhidi ya baa la njaa duniani


Kardinali Oscar Rodriguez Maradiaga, Rais wa Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis anasikitika kusema kwamba, takwimu zinaonesha kuwa matajiri 85 duniani wanamiliki nusu ya utajiri wote wa dunia, changamoto kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea mambo makuu matatu: usawa, unyofu na mshikamano. RealAudioMP3

Mambo haya yakizingatiwa kikamilifu kwa kutambua kwamba, binadamu wote wanaunda Familia moja ya binadamu, baa la njaa na utapiamlo wa kutisha unaweza kupewa kisogo, ufikapo Mwaka 2025, kama inavyojionesha kwenye Kampeni ya Caritas Internationalis katika kupambana na baa la njaa duniani. Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Kwaresima, aliwaomba waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuunga mkono juhudi zinazotekelezwa na Caritas Internationalis katika kupambana na baa la njaa duniani.

Kardinali Maradiaga anasema, ikiwa kama: mali, madaraka na utajiri wa kutupwa kwa baadhi ya watu ungetumika kikamilifu kwa ajili ya mafao na ustawi wa wengi, leo hii umaskini, ujinga na maradhi yangekuwa ni mambo yaliyopitwa na wakati. Lakini mambo ni tofauti kabisa, kumbe kuna haja kwa Jamii kuchunguza dhamiri zao, tayari kubadili mwelekeo kwa kukazia haki, usawa, unyofu na mshikamani wa upendo na udugu miongoni mwa Watu wa Mataifa, ili asiwepo tena mtu anayekufa kwa baa la njaa duniani.

Kila mtu anapaswa kujiuliza haki inayotiliwa mkazo na Baba Mtakatifu Francisko ina maana gani katika maisha ya mtu mmoja mmoja na Jamii katika ujumla wake? Ni mahali gani ambako haki na usawa vimetoweka katika maisha ya mwanadamu. Je, ninawezaje kujenga maisha yangu katika fadhila ya unyofu? Ni nani ninayeona anahitaji zaidi msaada wangu kwa wakati huu.

Kutokana na tafakari hii ya kina, inawezekana kabisa kwamba, Kampeni ya Caritas Internationalis dhidi ya baa la njaa duniani inaweza kuwa ni sehemu ya utekelezaji wa changamoto zinazotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Caritas Internationalis inasema, si haki kabisa kwa watu millioni 800 kuteseka kwa baa la njaa wakati ambapo kuna baadhi ya watu wanakula na kusaza bila hata ya kuguswa na shida pamoja na mahangaiko ya jirani zao wanaokufa kwa baa la njaa sehemu mbali mbali za dunia. Kuna haja kwa watu kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya watu kama anavyokazia Baba Mtaktifu Francisko.
Dunia imebahatika kuwa na rasilimali ya kutosha, jambo la msingi ni kuwa na ugavi bora na sahihi unaozingatia mafao na maendeleo ya wengi. Watu wanaweza kuwa na maisha manyofu, kwa kuwa na matumizi ya wastani pamoja na kujenga utamaduni wa kutunza chakula kwa kuzingatia vipaumbele vya mtu katika maisha.

Kipindi cha Kwaresima na hasa Juma kuu kiwe ni fursa ya kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo na udugu kati ya watu: kwa kugawana muda, rasilimali, chakula kama kielelezo cha ushuhuda wa imani tendaji katika mchakato wa kupambana na baa la njaa na utapiamlo duniani. Ni muda muafaka wa kushikamana ili kupambana na umaskini unaoendelea kuwanyanyasa watu zaidi ya billioni 3. 5.

Kila mtu akipenda anaweza kuchangia katika kupambana na baa la umaskini duniani, anasema Kardinali Oscar Rodriguez Maradiaga, Rais wa Caritas Internationalis katika kuhamasisha Kampeni ya mapambano dhidi ya baa la njaa duniani.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.