2014-03-11 12:15:39

Mh. sana Padre Placide Lubamba Ndjibu ateuliwa kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Kasongo, DRC


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Mheshimiwa sana Padre Placide Lubamba Ndjibu, kutoka katika Shirika la Wamissionari wa Afrika kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Kasongo, DRC. Askofu mteule alizaliwa tarehe 26 Oktoba 1959, Jimboni Lubumbashi. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapadrishwa tarehe 27 Julai 1991.

Hadi kuteuliwa kwake alikuwa ni Padre mkuu wa Kanda ya Wamissionari wa Afrika inayounganisha nchi ya Burundi, DRC na Rwanda. Tangu Mwaka 1991 hadi mwaka 1994 alifanya kazi nchini Burkina Faso. Mwaka 1994 hadi mwaka 1996 akaenda kusomea Uandishi wa Habari Chuo Kikuu cha Friburg, nchini Uswiss. Kati ya Mwaka 1996 hadi mwaka 1998 alitoa huduma za kuhariri Gazeti la Wamissionari wa Afrika lijulikanalo kama Vivant Universr huko Ubelgiji.

Askofu mteule Ndjibu kati ya Mwaka 1998 hadi mwaka 2002 alikuwa anafanya utume wake Parokiani Manzese, Jimbo kuu la Dar es Salaam, Tanzania. Mwaka 2002 hadi Mwaka 2007 alikuwa ni Mhariri mkuu wa jarida la KARIBU linalochapishwa mjini Bukavu.

Mwaka 2007 hadi mwaka 2010 aliteuliwa kuwa Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Bernadetta, Jimbo Katoliki la Lubumbashi. Kuanzia tarehe 1 Septemba 2010 alikuwa anaishi kwenye Makao Makuu ya Kanda ya Shirika la Wamissionari wa Afrika kwa ajili ya Burundi, DRC na Rwanda.







All the contents on this site are copyrighted ©.