Mshikamano wa Maaskofu na waathirika wa machafuko ya kisiasa nchini Misri
Marekani haina budi kushirikiana na Jumuiya ya Kimataifa ili kuuunga mkono juhudi
zinazofanywa na wananchi wa Misri ili kumaliza migogoro na malumbano ya kivita na
kurejesha amani na utawala wa kisheria nchini Misri.
Ni maneno ya Askofu Richard
Pates, Mwenyekiti wa kamati ya Haki na Amani Kimataifa ya Baraza la Maaskofu Katoliki
Marekani kwenye barua aliyomwandikia Katibu wa Serikali ya Marekani Bwana John Kerry
hivi karibuni. Kuna haja ya kujenga na kudumisha utamaduni wa majadiliano na msamaha
ili kudumisha misingi ya haki, amani na uhuru wa kidini nchini Misri.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Marekani linasikitishwa na hali ya Misri na pia linalaani mwelekeo
uliochukuliwa na baadhi ya wananchi wa Misri kushambulia Makanisa na miundo mbinu
ya huduma za kijamii. Maaskofu wanaungana na Baba Mtakatifu Francisko ili kuiombea
Misri, waathirika na familia zao na watu wote wanaoendelea kuteseka kutokana na misukosuko
nchini Misri.
Maaskofu wanawashukuru na kuwapongeza wananchi wa Misri walionesha
uungwana kwa kutetea mali ya Kanisa dhidi ya mashambulizi. Waathirika wakuu wa machafuko
na migogoro kama hii ni maskini, wanawake na watoto!
Shirika la Misaada la
Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, CRS linashirikiana na Kanisa la Misri katika
jitihada za kuwasaidia waathirika wa vurugu na kinzani nchini Misri.