2013-06-29 09:55:01

Vitendo vya kigaidi vinapaswa kudhibitiwa, ili kudumisha misingi ya haki, amani, utulivu na maendeleo!


Ifuatayo ni hotuba ya Mizengo Pinda, Waziri mkuu wa Tanzania, wakati wa kuhitimisha shughuli za mkutano wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tarehe 28 Juni 2013.

UTANGULIZI

a) Masuala ya Jumla
Mheshimiwa Spika,
    Tarehe 9 Aprili, 2013 tulianza Kikao cha Kwanza cha Mkutano wa 11 wa Bunge lako Tukufu. Ni jambo la kumshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa Rehema kwamba leo tunahitimisha shughuli zote zilizopangwa kwa amani na salama. Mkutano huu ulikuwa mahsusi kwa ajili ya kuwasilisha, kujadili na hatimaye kupitisha Bajeti ya Serikali na Makadirio ya Matumizi ya Fedha kwa Wizara, Mikoa na Taasisi mbalimbali.


Mheshimiwa Spika,
    Pamoja na kupitisha Bajeti ya Serikali, katika Mkutano huu Waheshimiwa Wabunge walipata fursa ya kufanya uchaguzi wa Wajumbe kwenye Taasisi na Vyuo vya Elimu ya Juu. Napenda nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Murtaza Ally Mangungu, Mbunge wa Kilwa Kaskazini kuwa Mjumbe wa Bunge hili katika Chuo Kikuu cha Dodoma; Mheshimiwa Jitu Vrajilal Soni, Mbunge wa Babati Vijijini kuwa Mjumbe katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo; Mheshimiwa Dkt. Pindi Hazara Chana, Mbunge wa Viti Maalum, kuwa Mjumbe wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Taknolojia – Mbeya na Mheshimiwa Selemani Said Jafo, Mbunge wa Kisarawe kuwa Mjumbe wa Jukwaa la Kibunge la Nchi Wanachama Kusini mwa Afrika (SADC – PF). Aidha, nawapongeza Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum na Mheshimiwa Mohamed Habib Mnyaa, Mbunge wa Mkanyageni kwa kuchaguliwa kuwa Wawakilishi wetu katika Baraza la Chuo Kikuu cha Mzumbe. Matarajio yetu ni kwamba, wote waliochaguliwa watatuwakilisha vyema katika Taasisi hizo muhimu.


Mheshimiwa Spika,
    Kipekee, napenda nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Yussuf Salimu Hussein kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge Mpya wa Jimbo la Chambani kupitia Chama cha Wananchi – CUF. Ni dhahiri kwamba kuchaguliwa kwake ni kutokana na matumaini makubwa waliyonayo Wananchi wa Jimbo la Chambani na kwamba atawawakilisha vyema ndani na nje ya Bunge katika kusukuma shughuli za Maendeleo Jimboni mwao.


    Vilevile, nitumie nafasi hii kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. Dalali Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga na Mheshimiwa Aeshi Hilaly, Mbunge wa Sumbawanga Mjini kwa kufanikiwa kurejea tena Bungeni baada ya kushinda rufaa za kesi zao za uchaguzi katika Majimbo yao.


Mheshimiwa Spika,
    Napenda kuchukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uongozi wake makini ambao umeendelea kuipatia sifa Tanzania katika ngazi za Kanda na Kimataifa. Hali hiyo imejidhihirisha wazi kwa matukio ya Kimataifa ambayo yamefanyika hapa Nchini. Miongoni mwa matukio hayo ni Ziara ya Rais Xi Jinping wa China alipotembelea Tanzania tarehe 24 Machi, 2013, na kuhutubia Bara la Afrika akitumia Jukwaa la Tanzania. Hivi sasa pia tunajiandaa kumpokea Mheshimiwa Barack Obama, Rais wa Marekani atakayekuwepo hapa Nchini kuanzia tarehe 1 Julai, 2013. Vilevile, Tanzania itakuwa Mwenyeji wa Mkutano wa Kimataifa wa Majadiliano ya Ushirikiano kwa Manufaa ya Wote wa Mwaka 2013 (Global 2013 Smart Partnership Dialogue) ambao utafanyika kuanzia tarehe 28 Juni, 2013. Matukio yote haya siyo tu yametokea hivi kwa bahati tu, bali ni muonekano wa Tanzania Nchi za nje na jinsi ambavyo inaonekana kwa wenzetu tunaoshirikiana nao. Hili ni jambo la kujivunia!


Mheshimiwa Spika,
    Sote tunakumbuka kuwa, wakati tukiendelea na Mkutano huu hapa Bungeni, matukio matatu makubwa ya kusikitisha yalitokea hapa Nchini. Moja ni tukio la Mlipuko wa Bomu katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi la Olasiti, Arusha lililotokea tarehe 05 Mei, 2013. Pili ni tukio la vurugu za tarehe 22 Mei, 2013 zilizotokea Mkoani Mtwara baada ya baadhi ya Wananchi wa Mtwara kutopenda kujengwa kwa Bomba la Kusafirishia Gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam. Tatu ni tukio la mlipuko wa Bomu lililotokea tarehe 15 Juni, 2013 katika Mkutano wa Kampeni za Uchaguzi wa Madiwani katika Kata ya Soweto katika Jiji la Arusha. Wote tunakumbuka kwamba katika matukio yote haya matatu, Watu wapatao 10 walipoteza maisha na wengine wapatao 155 kupata majeraha, na mali za Raia kuharibiwa au kupotea kabisa. Kwa masikitiko natoa pole wale wote waliopotelewa na Ndugu, Jamaa na Marafiki katika matukio hayo. Aidha, nawapa pole Majeruhi wote pamoja na Wananchi wote waliopoteza mali ikiwemo kuchomewa nyumba na hivyo kuathirika kiuchumi na kisaikolojia.


Mheshimiwa Spika,
    Uzoefu tunaoupata katika matukio yote haya ni kwamba hakuna raia mwema anayeipenda Nchi yake anayetamani matukio haya yatokee ndani ya Nchi yetu. Wananchi wengi wamesikitishwa sana na matukio hayo ambayo yamepoteza maisha na mali za ndugu zetu. Tunamwomba Mwenyezi Mungu atuepushe na hila zozote zenye nia mbaya ya kufanya matukio kama hayo kutokea tena kwenye Nchi yetu. Wito wangu kwa Watanzania wote ni kuwaomba tuwe Wamoja katika kukemea na kulaani matukio hayo. Ni muhimu tuendelee kuishi kwa Upendo, Amani na mshikamano, kwa maana huo ndio utamaduni wa Mtanzania.


Mheshimiwa Spika,
    Wakati wa Mkutano huu, wapo Waheshimiwa Wabunge wenzetu waliopoteza Ndugu, Jamaa na Marafiki, ikijumuisha Wapendwa wao, Wazazi, na Watoto. Wote kwa ujumla wao nawapa pole kwa yote yaliyowafika.


b) Maswali
Mheshimiwa Spika,
    Tangu tulipoanza Mkutano huu tarehe 9 Aprili, 2013 hadi leo, jumla ya Maswali 489 ya Msingi pamoja na 1,327 ya Nyongeza yaliulizwa na Waheshimiwa Wabunge na kujibiwa na Serikali. Vilevile, Maswali 31 ya Msingi na 27 ya Nyongeza yalijibiwa kwa utaratibu wa Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu. Nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote waliouliza Maswali ya Msingi na ya Nyongeza. Aidha, nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri waliojibu Maswali hayo na kutoa ufafanuzi kwa ufasaha mkubwa.


c) Miswada
Mheshimiwa Spika,
    Katika Mkutano huu, pia Waheshimiwa Wabunge walipata fursa ya kujadili, kurekebisha na kupitisha Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali wa mwaka 2013, [The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Bill, 2013]. Kupitishwa kwa Muswada huo kutatusaidia kama Taifa kuboresha matumizi ya Sheria husika ikiwemo Sheria ya Uchaguzi wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria, na Sheria ya Utumishi wa Umma. Aidha, Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2013 (The Finance Bill 2013) na Muswada wa Sheria wa Kuidhinisha Matumizi ya Fedha za Serikali wa Mwaka 2013 (Appropriation Bill) yote ilisomwa kwa mara ya Kwanza na kupitia ngazi zake zote na hivyo kuidhinisha Matumizi ya Serikali ya Mwaka 2013/2014.


Mheshimiwa Spika,
    Vilevile, Miswada ifuatayo ilisomwa kwa mara ya Kwanza:


    Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, 2013 [The Constitutional Review (Amendments) Act, 2013];


    Muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni wa Mwaka 2013 [The Referendum Act, 2013];


    Muswada wa Sheria ya Mfuko wa Akiba kwa Wafanyakazi wa Mwaka 2013 [GEPF Retirement Benefits Fund Act, 2013];


    Muswada wa Sheria ya Taifa ya Umwagiliaji, 2013 [The National Irrigation Act, 2013]; na


    Muswada wa Sheria ya Takwimu wa Mwaka 2013 [The Statistics Act, 2013].


Mheshimiwa Spika,
    Napenda kwa dhati kabisa kuwashukuru tena Waheshimiwa Wabunge kwa kutumia muda wote wa Mkutano huu kwa ufanisi mkubwa. Wote mtakumbuka tulianza Mkutano huu kwa changamoto kubwa ya Mabadiliko ya Mzunguko mpya wa kuwasilisha Bajeti ya Serikali (New Budget Cycle) na pengine kuwepo hoja na mashaka kuhusu ufanisi wake. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba tumefanya vizuri sana!! Wote ni mashahidi kwamba Waheshimiwa Wabunge wameweza kujadili kwa kina na kutoa ushauri wao ambao kwa kiasi kikubwa umezingatiwa na Serikali. Tunajivuna kwa kupitisha Bajeti ya Serikali kwa kutumia utaratibu mpya na kwa kuzingatia Kanuni na Taratibu za Bunge lako Tukufu.


Mheshimiwa Spika,
    Nitumie fursa hii ya kipekee kukupongeza wewe binafsi kwa kubuni na kuridhia utekelezaji wa utaratibu huu. Aidha, nirudie kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa kazi nzuri mliyoifanya kwa ajili ya maendeleo ya Taifa hili. Lakini kipekee kabisa nimpongeze Waziri wa Fedha na Wataalam wake kwa kazi nzuri ambayo imeiwezesha Serikali sikivu inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kukamilisha Bajeti hii baada ya kuzingatia ushauri na maoni ya Waheshimiwa Wabunge. Ni kweli kwamba haikuwa kazi nyepesi, lakini wote ni mashahidi kwamba kwa mara ya kwanza tumepata Bajeti nzuri ya Serikali na ya aina yake. Changamoto iliyoko mbele yetu ni kujipanga vizuri kusimamia utekelezaji wake kwa kukusanya Mapato yatakayotosheleza mahitaji yaliyoorodheshwa kwenye bajeti hiyo.





II UTARATIBU MPYA WA MZUNGUKO WA BAJETI (NEW BUDGET CYCLE)

Mheshimiwa Spika,
    Tumefanikiwa kukamilisha mchakato wa kuandaa, kuchambua, kujadili na hatimaye kuidhinisha Bajeti za Mafungu ya Wizara zote, zikiwemo Idara zinazojitegemea, Taasisi na Wakala mbalimbali za Serikali, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa mwaka 2013/2014. Hatua hii itatuwezesha kuanza utekelezaji wa Bajeti ya Serikali ifikapo tarehe 1 Julai, 2013. Wakati wa mchakato huu tumejifunza mambo mengi lakini pia tumeona zipo changamoto mbalimbali ambazo zinahitaji kupatiwa ufumbuzi. Aidha, tumepata maoni na ushauri mbalimbali kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge na Wadau mbalimbali kuhusu namna ya kuboresha Bajeti zijazo ili ziwe bora zaidi na zenye maslahi makubwa kwa Wananchi wetu na Taifa kwa ujumla. Tutazingatia maoni na ushauri huo tuliopata kutoka kwa Wadau wote.

Mheshimiwa Spika,
    Miongoni mwa mafanikio ya utaratibu huu mpya ni pamoja na; Kwanza: Kuwezesha Serikali kuanza kutekeleza Mpango na Bajeti mapema kuanzia tarehe 1 Julai 2013; na Pili kutoa fursa kwa Serikali kufanya majadiliano mapana na ya kina na Waheshimiwa Wabunge na kuwezesha kuzingatia maeneo muhimu yanayopaswa kuingizwa kwenye Mpango na Bajeti katika mwaka mpya wa fedha kabla Bajeti mwaka haijapitishwa.


Mheshimiwa Spika,
    Kufuatia mafanikio hayo, kwa utaratibu huu mpya tumeweza kutenga fedha zaidi katika Sekta za Maji, Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Umeme Vijijini na kutunisha Mifuko ya Mendeleo ya Wanawake na Vijana. Ni faraja kwamba Serikali imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kufanya maboresho zaidi katika Kodi na Tozo mbalimbali ili kupata fedha za kugharamia mahitaji hayo yaliyojitokeza. Serikali inapongeza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Kamati zote za Bunge za Kisekta na Wadau wengine kwa mchango wao wa mawazo wa namna ya kuongeza Mapato ya Serikali ili kukidhi mahitaji hayo ya fedha yaliyojitokeza wakati wa majadiliano ya Bajeti.


III UFUATILIAJI NA TATHMINI YA UTEKELEZAJI WA VIPAUMBELE VYA MPANGO WA MAENDELEO NA BAJETI YA 2013/2014

Mheshimiwa Spika,
    Katika mwaka ujao wa fedha wa 2013/2014, Serikali imejizatiti kutekeleza kwa dhati Mpango wa Maendeleo na Bajeti ya Serikali tuliyoipitisha katika Mkutano huu. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu) Mheshimiwa Stephen Wasira (Mb.) pamoja na Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. William Augustao Mgimwa (Mb.) katika hotuba zao na kwenye majumuisho wameeleza kwa kina na kutoa ufafanuzi wa hatua zitakazochukuliwa na Serikali katika maeneo hayo.


Mheshimiwa Spika,
    Pamoja na maelezo hayo mazuri ya Waheshimiwa Mawaziri, napenda kutumia fursa hii kutoa msisitizo katika maeneo mawili muhimu. Eneo la Kwanza ni kuhusu utekelezaji wa Vipaumbele vya Mpango wa Maendeleo na utaratibu mpya wa kusimamia na kufuatilia Miradi ya Maendeleo chini ya President’s Delivery Bureau. Eneo la Pili ni Kuimarisha Usimamizi wa Ukusanyaji Mapato na Matumizi ya Serikali.


    Utekelezaji wa Vipaumbele vya Mpango wa Maendeleo na utaratibu mpya wa kusimamia na kufuatilia Miradi ya Maendeleo chini ya President’s Delivery Bureau.

Mheshimiwa Spika,
    Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Mwaka 2013/2014 umetayarishwa kwa mantiki kwamba ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa mwaka 2011/2012 - 2015/2016. Hivyo, malengo yake yamezingatia utekelezaji wa vipaumbele vya msingi vya Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, ambavyo ni:


    Kuongeza uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme;


    Kuimarisha shughuli za Usafirishaji na Uchukuzi hususan katika Ukanda wa Kati. Hii inajumuisha kupanua Bandari ya Dar es Salaam na kuboresha usafiri wa barabara na Reli ya Kati;


    Kuongeza uzalishaji na tija katika Sekta ya Kilimo, hususan, katika uzalishaji wa mazao makuu ya chakula ili kutosheleza mahitaji ya ndani na kupata ziada kwa ajili ya kuuza nje ya Nchi;


    Kuchochea uwekezaji katika Sekta ya Viwanda, hususan, vile vinavyotumia au kuongeza thamani ya mazao ghafi yanayopatikana hapa Nchini;


    Kuendeleza Rasilimali Watu na Ujuzi ikiwa ni pamoja na kuimarisha ufundishaji wa Masomo ya Sayansi, Ufundi Stadi na Teknolojia;


    Kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za jamii; na


    Kuboresha huduma za utalii, biashara na fedha.

Mheshimiwa Spika,
    Ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa Mipango yetu ya Maendeleo, imeonekana kuna umuhimu wa kuimarisha Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini. Katika kuhakikisha kwamba azma hii inatekelezwa, Serikali imefikia uamuzi wa kuanzisha Mfumo mpya wa ufuatiliaji na tathmini unaojulikana kama “Matokeo Makubwa Sasa” (Big Results Now) ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/2012 - 2015/2016). Msingi wa Mfumo huu ni uwazi katika kupanga shughuli za utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo inayokusudiwa. Kwa ujumla, Miradi ya Maendeleo na utekelezaji wake inatakiwa isiwe siri kwa Wananchi au jamii inayolengwa. Hivyo, pamoja na kuainisha shughuli zitakazotekelezwa, Mfumo huu unabainisha muda, mhusika, rasilimali zinazohitajika, vigezo vya kupimia mafanikio ya utekelezaji na ni shirikishi.


Mheshimiwa Spika,
    Vilevile, Mfumo huu umeanzishwa ili kumwezesha Mheshimiwa Rais na Serikali kwa ujumla, kusimamia ipasavyo utekelezaji wa programu na miradi ya kipaumbele ili kuharakisha maendeleo. Hivyo, kazi za utendaji na uratibu zitakuwa chini ya Ofisi ya Rais, Ikulu, na kusimamiwa na chombo kitakachojulikana kama “President’s Delivery Bureau-PDB”. Majukumu ya chombo hicho ni:


    Kuchambua kwa utaratibu wa Kimaabara wa Miradi ya kipaumbele iliyobainishwa katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na kuainisha shughuli zinazopaswa kutekelezwa, muda wa kuanza na kukamilika kwake, malengo yanayotarajiwa, na kiasi cha fedha kinachohitajika kwa utekelezaji;


    Kutayarisha na kusimamia mikataba ya uwajibikaji wa Mawaziri;


    Kutoa ushauri na kusaidia kutatua vikwazo vya utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo; na


    Kufanya tathmini ya utekelezaji na kuishauri Serikali juu ya hatua zinazopaswa kuchukuliwa na kuwezesha Wizara husika kufikia malengo yaliyowekwa.


Mheshimiwa Spika,
    Napenda kubainisha kuwa “Tekeleza kwa Matokeo Makubwa Sasa” si Mpango, bali ni Mfumo. Mfumo huu utawezesha kusimamia vizuri zaidi utekelezaji wa miradi ya maendeleo na majukumu ya Serikali yaliyobainishwa kuwa ni ya kipaumbele katika kufikia malengo ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Mfumo huu, pamoja na mambo mengine, unakusudiwa pia kuimarisha Mfumo wa Upimaji wa Wazi wa Utendaji Kazi Serikalini unaojulikana kama “Open Performance Review and Appraisal System - OPRAS”, ambao kwa sasa umekuwa hautekelezwi kama ilivyokusudiwa. Kwa kutumia Mfumo huu mpya, sasa Waheshimiwa Mawaziri watakuwa wanawekeana Mikataba ya Utendaji (Performance Contracts) na Watendaji walio chini yao. Kwa kuanzia, “President’s Delivery Bureau” itasimamia utekelezaji wa Awamu ya Kwanza katika maeneo sita (6) yaliyofanyiwa uchambuzi wa kina wa Kimaabara (Labs) ambao umekamilika hivi karibuni. Maeneo hayo ni Nishati ya Umeme; Uchukuzi na Usafirishaji; Kilimo; Elimu; Maji; na Ukusanyaji Mapato.


    Kuimarisha usimamizi wa ukusanyaji wa Mapato na Matumizi ya Serikali

Mheshimiwa Spika,
    Pamoja na kuanzishwa kwa utaratibu huu Mpya wa kufuatilia Miradi, kipengele muhimu kilichozungumziwa katika Mkutano huu ni kuhusu kuimarisha usimamizi wa ukusanyaji wa Mapato na Matumizi ya Serikali. Michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge iliyotolewa imesisitiza kwamba Bajeti ya Serikali ya Mwaka 2013/2014 iliyoidhinishwa na Bunge lako Tukufu inahitaji usimamizi makini na mahiri ili kufikia malengo tuliyojiwekea. Kwa mantiki hiyo, Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi wa ukusanyaji wa Mapato na kuhakikisha kwamba kuna uwajibikaji mkubwa wa matumizi ya Serikali. Miongoni mwa hatua zitakazochukuliwa na Serikali katika mwaka 2013/2014 ili kufikia azma hiyo ni pamoja na zifuatazo:

Kwanza: Kuimarisha uwezo wa Serikali wa kukusanya Mapato ya ndani ili kupunguza utegemezi wa misaada kutoka nje na kutegemea zaidi kodi za biashara za Kimataifa na Kikanda. Hatua hizo zitaambatana na kusimamia ipasavyo ukusanyanyaji wa mapato yatokanayo na rasilimali muhimu za Taifa kama vile Madini, Gesi Asilia, Wanyamapori, Misitu, Uvuvi, Ardhi, Vivutio vya Utalii pamoja na kutumia vizuri fursa za kijiografia zinazotokana na Nchi yetu kupakana na Nchi Nane jirani zisizokuwa na bahari;

Pili: Sambamba na hatua hiyo, Serikali itayafanyia kazi mapendekezo ya Kamati yako Maalum uliyoiunda inayoongozwa na Mheshimiwa Andrew Chenge, Mbunge wa Bariadi Magharibi ambayo umeipa jukumu la kuangalia vyanzo vipya vya Mapato ya Serikali. Aidha, Serikali itakamilisha utafiti wake unaoendelea wa kubaini vyanzo vipya na endelevu vya kupata mapato mengi ya ndani. Vilevile, itakamilisha utafiti wa uchambuzi wa misamaha ya kodi ili kuleta mapendekezo mahsusi ya kupunguza misamaha isiyo na tija;

Tatu: Serikali itaimarisha usimamizi na udhibiti wa mifumo yake ya ndani hasa katika eneo la Manunuzi ya Umma. Maafisa Masuuli wa Wizara, Idara za Serikali zinazojitegemea, Wakala na Taasisi za Umma, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa zote Nchini wanakumbushwa tena kuzingatia ipasavyo Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo ya kifedha na kiuhasibu iliyopo kuhusiana na Matumizi ya Fedha za Umma. Hii ni pamoja na kudhibiti matumizi yasiyo ya lazima kama vile kugharamia Semina na Makongamano, Ununuzi wa fulana na Kofia za Sherehe mbalimbali, ununuzi wa magari ya kifahari, posho mbalimbali, mafuta na matengenezo
ya magari ya Serikali kwa gharama kubwa zisizoendana na ubora uliopatikana. Hatua za Kinidhamu zitachukuliwa kwa watakaokiuka maelekezo yaliyotolewa;

Nne: Ili kuongeza uwazi na uwajibikaji wa Serikali kwa Bunge na Wananchi, Serikali imeandaa mfumo imara na endelevu wa kuhakikisha kuwa Taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na Taarifa za Kamati za Kudumu za Bunge zinazosimamia Fedha za Umma yaani Public Accounts Committee - PAC na Local Authorities Accounts Committee-LAAC zinapewa umuhimu wa hali ya juu na kushughulikiwa kikamilifu. Tayari, Katibu Mkuu Kiongozi ameunda Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu yenye wajibu wa kuhakikisha kuwa Taarifa hizo zote zinachambuliwa vizuri na majibu sahihi yanatolewa kwa wakati. Kamati hii inasaidiwa na Kamati Ndogo ya Wataalam ambayo pamoja na mambo mengine inafanya uchambuzi wa awali, na pia kupendekeza kwa Kamati ya Makatibu Wakuu namna bora ya kupunguza uzalishaji wa hoja mpya za ukaguzi;

Tano: Ili kuimarisha usimamizi wa rasilimali za Umma pamoja na kuongeza ufanisi wa utendaji kazi Serikalini, Serikali itaendelea kuhimiza uzingatiaji wa Maadili katika Utumishi wa Umma pamoja na kuteua na kupanga safu ya Viongozi na Watendaji hodari, makini na wenye sifa stahiki za kitaaluma katika Wizara, Taasisi na Idara za Serikali, Mikoa na Halmashauri. Watumishi wasio na sifa na wababaishaji hawatapewa nafasi.

IV LISHE

Mheshimiwa Spika,
    Mara kwa mara nimekuwa nikilitaarifu Bunge lako Tukufu kuhusu hali ya Lishe Nchini na athari zake kwa Wananchi hasa kwa Watoto chini ya miaka mitano na uchumi kwa ujumla. Nimeeleza pia juhudi za Serikali katika kukabiliana na hali ya Lishe Duni. Nichukue nafasi hii kulitaarifu Bunge kuwa Serikali ya Awamu ya Nne imeendelea na juhudi zake za kuboresha lishe na kipekee Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amekuwa mstari wa mbele katika kuongoza juhudi hizo.



Mheshimiwa Spika
    Kutokana na juhudi hizo, Tarehe 15 Mei 2013, Mheshimiwa Rais alizindua Mpango wa Kuongeza Virutubisho kwenye Vyakula kwa kuanzia na mafuta ya kupikia na unga wa ngano. Mpango huo utachangia kwa kiasi kikubwa sana kupunguza utapiamlo kwa Watoto walio chini ya miaka mitano. Aidha, tarehe 16 Mei 2013 Mheshimiwa Rais alizindua Kampeni ya Kitaifa ya Kuongeza Uwajibikaji Katika Lishe Nchini. Uzinduzi huo ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, Sekta Binafsi, Washirika wa Maendeleo pamoja na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Viongozi hao walipata nafasi ya kutoa na kuthibitisha ahadi zao za kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha Lishe Nchini.


Mheshimiwa Spika,
    Kampeni kama hizo zitaendelea kufanyika katika ngazi za Mikoa, Wilaya hadi Vijijini ili Elimu ya Lishe Bora ienezwe kwa kasi katika ngazi zote. Napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuwa mstari wa mbele katika kuongoza mapambano dhidi ya utapiamlo Nchini. Aidha, nitumie fursa hii kuwaagiza Wakuu wa Mikoa kuhakikisha wanaendeleza Kampeni za Elimu ya Lishe katika Mikoa yao na kusimamia kwa karibu kuhakikisha kwamba kampeni hizo zinaendelezwa hadi kwenye ngazi za Wilaya na Vijiji.


Mheshimiwa Spika,
    Vilevile, nitumie fursa kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, tarehe 8 Juni, 2013 nilihudhuria Mkutano Maalum ulioandaliwa na Nchi Tajiri na zenye Viwanda vingi Dunani (G8) kuhusu Lishe Bora na Ukuaji wa Uchumi uliofanyika Jijini London-Uingereza na kuhudhuriwa na Viongozi kutoka Mataifa mbalimbali. Katika Mkutano huo, nilipata nafasi ya kuelezea hatua ambazo Serikali imechukua katika kupambana na utapiamlo hapa Nchini. Aidha, nilieleza bayana malengo tuliyoyaweka ya kupunguza utapiamlo kwa Watoto na akina Mama kama ilivyobainishwa katika Mkakati wa Lishe wa Kitaifa 2011/2012 - 2015/2016. Malengo hayo tuliojiwekea ni pamoja na kupunguza udumavu kwa Watoto chini ya miaka 5 kutoka Asilimia 42 hadi Asilimia 27, kupunguza ukosefu wa madini joto kwa Wanawake wajawazito kutoka Asilimia 48.5 hadi Asilimia 35 na kuongeza unyonyeshaji pekee wa maziwa ya mama kwa Watoto wadogo bila kuwapa chakula chochote ndani ya miezi sita kutoka Asilimia 50 hadi Asilimia 60.


Mheshimiwa Spika,
    Imani yangu ni kwamba, malengo tuliyojiwekea yatafikiwa iwapo sote tutashirikiana kwa karibu katika utoaji wa Elimu ya Lishe kwa Wananchi wetu katika ngazi zote. Kwa maana hiyo, ninawasihi Waheshimiwa Wabunge kuendelea kushirikiana na Serikali kutoa elimu hiyo katika maeneo yenu ili kutokomeza janga hili la utapiamlo Nchini. Nitumie nafasi hii kupitia Bunge lako Tukufu kuwashukuru kwa dhati Wadau wote wa Maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika jitihada za kupambana na utapiamlo Nchini.

V SEKTA YA KILIMO

    Hali ya Chakula

Mheshimiwa Spika,
    Tathmini ya awali ya uzalishaji wa mazao ya chakula katika msimu wa 2012/2013 na upatikanaji wa chakula katika mwaka 2013/2014 inaonesha kuwa uzalishaji katika mikoa 19 kati ya 25 utakuwa wa kuridhisha na kuna dalili za kuwepo kwa chakula cha ziada katika Mikoa hiyo. Hivi sasa bei za Wastani za chakula hasa mchele na mahindi katika masoko mengi Nchini zimeshuka kufuatia uvunaji wa mazao hayo katika maeneo yanayopata mvua za msimu. Kwa mfano, bei ya mahindi imeshuka kutoka bei ya Wastani ya Taifa ya Shilingi 774 mwezi Februari 2013 hadi kufikia Shilingi 545 katika mwezi Mei 2013 na mchele kutoka Shilingi 1,825 hadi 1,413 katika kipindi hicho. Matarajio ni kwamba bei hizo zitashuka kadri chakula kitakavyoingizwa Sokoni. Ili kujihakikishia kuwa Nchi inakuwa na chakula cha kutosha, Wakala wa Taifa wa Uhifadhi wa Chakula (NFRA) itaanza ununuzi wa Tani 235,000 za mahindi na Tani 15,000 za mtama Mwezi Julai 2013.


Mheshimiwa Spika,
    Aidha, Serikali kupitia NFRA itaendelea na usambazaji wa chakula cha msaada kiasi cha Tani 69,451 kilichoidhinishwa na kutengwa kwa ajili ya kusambazwa kwa watu wenye upungufu wa chakula katika Mikoa na Halmashauri zenye upungufu. Nitumie fursa hii kuwaagiza tena Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuwahimiza Wakulima kuhifadhi Chakula cha kutosha kwa mahitaji ya Kaya zao badala ya kuuza Chakula chote na kusubiri Serikali kuwapelekea Chakula. Aidha, Halmashauri za Wilaya muda wote ziweke Mikakati madhubuti ya kuzuia ununuzi holela wa Chakula kutoka mashambani mwa Wakulima.


    Uamuzi wa Serikali kuhusu Muundo utakaotumika kutoa Pembejeo za Ruzuku

Mheshimiwa Spika,
    Katika mwaka 2012/2013, Serikali iliendelea kutoa ruzuku za Pembejeo za Kilimo kwa nia ya kumpunguzia Mkulima gharama za uzalishaji. Ruzuku ya pembejeo imekuwa ikitolewa kwa kutumia Vocha ambapo Mawakala walichaguliwa na Makampuni ya pembejeo. Hata hivyo, utaratibu huo uligubikwa na changamoto nyingi zikiwemo za Vocha kuchelewa kuwafikia Wakulima kutokana na kutowajibika kikamilifu na baadhi Watendaji wasio waaminifu kuwarubuni Wakulima, na baadhi ya Makampuni kutofikisha pembejeo kwa wakati. Changamoto hii zimelalamikiwa na Wabunge wengi wakati wanachangia hotuba ya Wizara ya Kilimo na Chakula na Ushirika.


    Ili kuondokana na changamoto hizo, Serikali imeamua kutumia Mifumo miwili katika utoaji wa ruzuku ya pembejeo za kilimo katika msimu wa kilimo wa 2013/2014. Mifumo hiyo itahusisha kuendelea na utaratibu wa Vocha na kuanzisha Mfumo wa mikopo kwa uwiano wa Asilimia 80 Vocha na Asilimia 20 mikopo. Aidha, Serikali imeidhinisha Bajeti ya Shilingi Bilioni 112.46 zikiwemo Shilingi Bilioni 19.972 za ufadhili wa Benki ya Dunia na Shilingi Bilioni 92.49 za Serikali kwa ajili hiyo.


Mheshimiwa Spika,
    Katika mwaka 2013/2014 Serikali itaendelea kufuatilia kwa karibu upatikanaji wa Tani 400,000 za mbolea, Tani 40,000 za mbegu bora, Miche Milioni 40 ya Chai na Kahawa, Tani 2,000 na lita 870,000 za madawa ya pamba na korosho kupitia ruzuku ya pembejeo. Napenda kuwakumbusha Wakuu wa Mikoa na Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri, kusimamia kwa karibu upatikanaji na usambazaji wa Mbegu na Mbolea ili kuwasaidia Wakulima kupata pembejeo hizo mapema. Aidha, nahimiza Sekta Binafsi nayo kuendelea kuingiza Mbolea, Mbegu bora na Madawa mbalimbali kwa ajili ya kuendeleza Kilimo Nchini.





    Mkakati wa Kuimarisha Mfumo Wa Stakabadhi za Mazao Ghalani Zao la Korosho


Mheshimiwa Spika,
    Katika Mkutano huu, Waheshimiwa Wabunge pia, walizungumzia kwa hisia tofauti Mfumo wa Stakabadhi wa mazao Ghalani. Mfumo wa Stakabadhi za Mazao Ghalani Maghala umeanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Stakabadhi Ghalani Na. 10 ya mwaka 2005 kwa lengo la kuwasaidia Wakulima wakiwa katika vikundi au ushirika kuwa na nguvu ya soko, kupata bei nzuri katika mazao ya biashara na kuingia katika soko la ushindani ambalo ingekuwa vigumu kutokana na kukosekana kwa mitaji. Pia, ulianzishwa ili kusaidia kuzuia upotevu wa mazao unaotokana na uhifadhi dhaifu, na pia kuongezea bidhaa thamani kabla ya kuziuza. Mfumo huu ulianza vizuri ambapo Wakulima walipata malipo ya kwanza, ya pili na ya tatu (Majaliwa). Hata hivyo, kwa sasa Mfumo huo unakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazotokana na upotoshaji unaofanywa na walanguzi na madalali wanaojinufaisha na ununuzi wa mazao kutoka kwa wakulima kwa kutumia mfumo usio rasmi. Vilevile, wapo Watendaji wasio waaminifu wa Vyama vya Ushirika, wasimamizi wa maghala na Taasisi za fedha wamechangia kudhoofisha mfumo huo.


Mheshimiwa Spika,
    Upo ukweli kwamba, mafanikio mengi yamepatikana baada ya kuanzishwa kwa Mfumo huo. Kwa mfano, kumekuwepo na ongezeko la uzalishaji wa Zao la Korosho ikilinganishwa na miaka mitano kabla ya kuanzishwa kwa Mfumo huu kutoka Tani 71.918 katika msimu wa 2001/2002 hadi kufikia Tani 158,439 katika msimu wa 2011/2012.

Aidha, bei ya Korosho iliongezeka kutoka Shilingi 360 kwa kilo katika msimu wa 2003/2004 hadi kufikia Wastani wa Shilingi 1,500 katika msimu wa 2010/2011.

Mheshimiwa Spika,
    Mfumo huu pia umesaidia Wakulima kuuza mazao yao kwa kutumia Mizani zinazokaguliwa na Wataalamu na kupatiwa bei Dira kwa kilo, tofauti na vipimo visivyo rasmi vinavyotumika nje ya Mfumo wa Stakabadhi Ghalani. Wakulima katika maeneo yanayozalisha Korosho wanafahamu sana vipimo batili vinavyojulikana kama “Kangomba” ambapo licha ya kipimo hiki kutofautiana kutoka eneo moja hadi jingine; kwa kutumia “Kangomba” Wakulima wanalipwa bei Dira ya ujazo mkubwa kuliko ujazo wa Kilo moja ya kawaida au kulipwa kidogo kulingana na bei Dira iliyopo. Aidha, matumizi ya “Kangomba” yanamkosesha Mkulima malipo ya majaliwa na hata pembejeo za mkopo, maana kipimo hiki hakipo katika Mfumo wa kukopesha Wakulima Pembejeo.


Mheshimiwa Spika,
    Chini ya Mfumo huu, Mikopo kutoka Mabenki kupitia kwa Vyama vya Ushirika vya Msingi imeongezeka kutoka Shilingi Bilioni 36.2 katika msimu wa 2007/2008 hadi kufikia Shilingi Bilioni 134.6 katika msimu wa 2011/2012. Kwa upande wa mapato, kumekuwepo na ongezeko la Mapato yatokanayo na Korosho Ghafi kutoka Tani 99,106 msimu wa 2007/2008 hadi Tani 158,439 msimu wa 2011/2012. Thamani ya mauzo imeongezeka kutoka Shilingi Bilioni 43.1 msimu wa 2007/2008 hadi Shilingi Bilioni 236.1 msimu wa 2011/2012.


    Aidha, Mapato yatokanayo na ushuru kwa kuuza nje ya Nchi yameongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka Shilingi Bilioni 6.4 msimu wa 2007/2008 hadi kufikia Shilingi Bilioni 35.4 katika msimu wa 2011/2012. Vilevile, Mfumo huu umewezesha upatikanaji wa takwimu sahihi za kiasi cha Korosho kilichozalishwa, kilichouzwa nje ya Nchi na kilichobanguliwa hapa Nchini.


Mheshimiwa Spika,
    Kutokana na mifano hiyo michache ya mafanikio, napenda kuchukua fursa hii kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, Wakulima na Wananchi kwa ujumla kuwa, Serikali ina imani na Mfumo huu wa Stakabadhi za Mazao Ghalani, na hivyo hautaondolewa kwa sasa bali Serikali inajipanga vizuri kuondoa vikwazo vilivyofanya Mfumo huu kufanya vibaya. Tutaimarisha usimamizi ili kutoa matokeo yaliyolengwa. Aidha, uamuzi huu wa Serikali unatokana na ukweli kuwa Mfumo huu upo kwa mujibu wa Sheria ya Stakabadhi za Mazao Gahalani Na. 10 ya mwaka 2005.


Mheshimiwa Spika,
    Vilevile, katika mwaka huu Serikali kwa kushirikiana na Wamiliki na wenye Viwanda vya Kubangulia Korosho, itafanya uchambuzi wa kina wa matatizo yanayokabili Viwanda hivi ili viweze kutumika kwa ajili ya kununua Korosho kutoka kwa Wakulima na kuzibangua. Lengo letu ni kuhakikisha kuwa Korosho zote zinazozalishwa hapa Nchini zinabanguliwa na kuongezwa thamani ili Mkulima aweze kupata bei nzuri zaidi.


    Mikakati ya Kuimarisha zao la Pamba.

Mheshimiwa Spika,
    Katika miaka ya hivi karibuni, uzalishaji wa zao la Pamba umekuwa ukidhoofika kutokana na kukumbwa na changamoto nyingi. Kwa mfano, katika msimu wa Kilimo wa 2012/2013 Kanda ya Magharibi ililenga kulima wa Hekta 660,000 lakini iliweza kulima Hekta 420,000 tu sawa na Asilimia 64 ya lengo. Upungufu huu ni sawa na Asilimia 26 ikilinganishwa na Hekta 568,000 zilizolimwa msimu wa kilimo 2011/2012.


Mheshimiwa Spika,

    Changamoto zinazokabili zao la Pamba kwa sasa ni pamoja na matumizi madogo ya pembejeo zikiwemo mbegu bora na viuatilifu visivyokidhi mahitaji; na wakati mwingine vimekuwa hafifu kutokana na mfumo wa kusambaza pembejeo hizi kutosimamiwa vyema. Aidha, katika Mfumo wa Kilimo cha Pamba cha Mkataba ambao unapaswa kumwezesha Mkulima kupata pembejeo kwa njia ya mkopo nao umeingia dosari nyingi kutokana na kuwepo kwa baadhi ya Viongozi na Wafanyabiashara katika maeneo yanayolimwa pamba kuwashawishi Wakulima kuukataa Mfumo huo. Imebainika kwamba baadhi ya Viongozi hao wana maslahi binafsi katika biashara ya pamba.


    Aidha, Taasisi zinazotakiwa kusimamia Zao la Pamba zimekuwa hazifanyi kazi zake ipasavyo, Wakulima kukosa imani na Mfuko wa Kuendeleza Zao la Pamba na Vikundi vya Wakulima kutoandikishwa kisheria hivyo kukosa dhamana ya kufidia wanunuzi endapo watashindwa kurejesha fedha za pembejeo na mikopo mingine waliyopewa ndani ya Mkataba.

Mheshimiwa Spika,
    Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba tayari, Mikutano ya Wadau inayoshirikisha Wakuu wa Mikoa, Wenyeviti wa Halmashauri, Maafisa Kilimo, Waheshimiwa Wabunge, Wafanyabiashara wa Pamba, Wakulima, Viongozi wa Bodi ya Pamba, Wawakilishi wa Wafadhili na Serikali imeshaanza katika Mikoa ya Mara, Simiyu, Geita na Mwanza. Lengo la mikutano hiyo ni kujadili Changamoto zinazokabili Sekta hii ya Pamba na kuweka mikakati ya kukabiliana nayo. Mikutano kama hiyo inatarajiwa kuendelea katika Mikoa yote inayozalisha Zao la Pamba.

Hatimaye tarehe 4 - 5 Julai, 2013 utafanyika Mkutano wa Wadau wote wa Pamba ambao utajadili changamoto na utatuzi wake.

VI VYAMA VYA USHIRIKA

    Mikakati ya kuimarisha Ushirika Nchini

Mheshimiwa Spika,
    Vyama vya Ushirika vimeendelea kutoa mchango mkubwa katika Maendeleo ya Wananchi katika Sekta mbalimbali za uchumi. Aidha, idadi ya Vyama imeendelea kuongezeka kutoka 5,424 mwezi Machi 2012 hadi 5,559 mwezi Machi 2013. Idadi ya wanachama nayo imeongezeka kutoka 917,889 hadi 1,153,248 katika kipindi hicho. Hisa, Akiba na Amana za Wanachama zimeongezeka pia kutoka Shilingi Bilioni 236.8 hadi Shilingi Bilioni 463.5 katika kipindi hicho. Kadhalika mikopo iliyotolewa na SACCOS kwa Wanachama wake imeongezeka kutoka Shilingi Bilioni 703.3 hadi Shilingi Bilioni 893.7.


Mheshimiwa Spika,
    Pamoja na mafanikio hayo, pamekuwepo na changamoto mbalimbali zinazokwamisha kasi ya ukuaji wa Ushirika Nchini. Baadhi ya changamoto hizo zimeongelewa sana ndani ya Bunge na Waheshimiwa Wabunge. Changamoto hizo ni pamoja na kuwepo kwa Viongozi wanaodhoofisha ushirika kwa kukosa ubunifu na kutowajibika katika kutekeleza majukumu yao. Kwa mfano, katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2010 hadi Juni 2012, jumla ya Vyama vya Ushirika vya Akiba na Mikopo (SACCOS) 1,844 na Vyama vya Ushirika wa Kilimo na Masoko (AMCOS) 2,544 vilikaguliwa. Matokeo ya ukaguzi huo yalionesha kukithiri kwa wizi, ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka kwenye Vyama vya Ushirika. Vitendo hivyo vimefanywa na Viongozi na Watendaji wa Vyama husika. Kutokana na tabia hiyo, baadhi ya vyama vimeingia katika migogoro na madeni makubwa na hivyo kusababisha hasara za mara kwa mara na kuchangia kukatisha tamaa Wanachama kuhusu Ushirika.


Mheshimiwa Spika,
    Katika kukabiliana na changamoto hizi, hatua kadhaa zimechukuliwa ambapo Viongozi wabadhirifu wameondolewa katika Vyama vya Ushirika vya CORECU (Pwani), CETCU (Singida), MLIMANI SACCOS (Dar es Salaam), AIRPORT TAX DRIVERS (Dar es Salaam), TUCOPROCOS (Turiani), UWAWAKUDA (Mvomero), MOCEMA (Morogoro), TINGATINGA ARTS SOCIETY LTD (Dar es Salaam), LUICHE SACCOS (Dar es Salaam), WAZALENDO SACCOS (Moshi) na WETCU (Tabora).


    Pamoja na hatua ya kuwaengua katika nafasi za uongozi, hatua za kuwatoza fidia (SURCHARGE) pia zimechukuliwa ili kurejesha fedha zilizofujwa. Aidha, utaratibu wa kuwachukulia hatua zaidi za kijinai unaandaliwa. Ili kuimarisha ukaguzi na usimamizi, Serikali itaunda timu imara ya ukaguzi zikihusisha Wakaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya mbalimbali zitakazoweza kufanya kazi kwa pamoja. Hatua hii itasaidia kupunguza uhaba wa Wakaguzi waliopo sasa na kuongeza kasi ya kufanya ukaguzi.




Mheshimiwa Spika,
    Vilevile, pamoja na mipango kadhaa ya kukabiliana na changamoto zilizojitokeza, Serikali itaendelea kuchambua na kutathmini mienendo ya kiuchumi ya Vyama vya Ushirika katika ngazi zote za Vyama vya Ushirika vya Msingi, Vyama Vikuu, Vyama vya kilele na Shirikisho la Vyama vya Ushirika ili kubaini hali halisi ya Vyama hivyo na uwezo wake. Hatua hii itaiwezesha Serikali kutoa ushauri kuhusiana na wimbi la utitiri wa Vyama vidogo vidogo ambavyo kimsingi havina tija.


Mheshimiwa Spika,
    Napenda kusisitiza kuwa, Serikali imebaini kuwa matatizo ya Ushirika yanasababishwa na udhaifu katika usimamizi na kwamba tatizo hili pia limetokana na utaratibu wa Maafisa wa Serikali kuwajibika katika Mamlaka mbili tofauti yaani Serikali Kuu na TAMISEMI. Hivyo, Serikali imefanya marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Ushirika ya mwaka 2003 ili kuongeza mbinu za usimamizi. Pia, Serikali itaanzisha Tume ya Maendeleo ya Ushirika na kuweka Mamlaka ya Usimamizi wa Vyama vya Ushirika katika ngazi zote, chini ya Mamlaka ya Tume.


Muswada huo tayari umesomwa kwa mara ya Kwanza na unatarajiwa kusomwa kwa mara ya Pili katika Bunge la Mwezi Agosti 2013.

    VICOBA

Mheshimiwa Spika,
    Pamoja na changamoto za Ushirika, yapo maeneo ambayo tumeweza kufanya vizuri na ninaamini tukiyapatia msukumo tunaweza kubadili maisha ya Wananchi wetu. Moja ya maeneo hayo ni katika VICOBA. Mfumo wa VICOBA umeendelea kushamiri na kuenea katika maeneo mbalimbali Nchini. Wananchi wengi hasa wa kipato cha chini wamejiunga na kunufaika na Mfumo huu. Inakadiriwa kuwa takriba Asilimia 35 ya Wananchi wanatumia huduma za fedha zisizo rasmi ambazo ni pamoja na VICOBA. Aidha, taarifa zilizopo zinaonesha kuwa tangu mwaka 2000 hadi sasa, inakadiriwa kuwa VICOBA vimefikisha Mtaji wa zaidi ya Shilingi Bilioni 300. Kwa sasa kasi ya kukua kwa mtaji imekuwa kubwa ambapo mtaji unakua kwa Shilingi Bilioni 100 kwa mwaka, tofauti na vilipoanza. Serikali inatambua hali hiyo na imejipanga vizuri kusaidia uendelezaji wa VICOBA nchini kwani mfumo huu ni rahisi na unasaidia sana upatikanaji wa huduma za fedha kwa watu wakipato cha chini hasa Wananchi wanaoishi Vijijini.


Mheshimiwa Spika,
    Ili kutoa msukumo katika suala zima la kuendeleza VICOBA, tayari Serikali imeshafanya mambo yafuatayo ili kuimarisha VICOBA Nchini:


Kwanza: Serikali imeshaanzisha Dawati maalum la kushughulikia VICOBA katika Baraza la Uwezeshaji wa Wananchi kwa kumteua Ofisa maalum wa kusimamia VICOBA;

Pili: Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imemteua Mtaalam Mwelekezi (Consultancy), Kampuni ya DAI Johannesburg ya Afika ya Kusini ili kufanya Utafiti (Study) na kuishauri Serikali namna bora ya kuendeleza VICOBA Nchini; na

Tatu: Wizara ya Fedha inaanzisha Idara ya Huduma Ndogondogo za Fedha (Microfinance Deptartiment) ili kusimamia maendeleo ya Sekta ya Fedha na Idara hiyo ndio itakuwa Mlezi wa VICOBA.

Mheshimiwa Spika,
    Pamoja na hatua hizo nilizozitaja, Serikali itaendelea kushirikiana na Wadau mbalimbali ili kuhakikisha huduma za fedha zinapatikana hadi Vijijini. Kila Halmashauri, ihakikishe kwamba, mafunzo yanatolewa kwa Vikundi vya VICOBA na vile vinavyoendeshwa vizuri vipewe fursa zaidi ya kujiendeleza. Kipekee kabisa napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Devota Mkuwa Likokola (Mb.) kwa jitihada zake kubwa za kuendeleza VICOBA Nchini. Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi hizo pamoja na Wadau wote wa VICOBA hapa Nchini.

VII AJIRA KWA VIJANA

Mheshimiwa Spika,
    Katika Mkutano huu, suala la ajira ya Vijana limezungumzwa sana. Tatizo la ajira bado ni changamoto kubwa inayowakabili Vijana Nchini. Kwa mujibu wa Sera ya Maendeleo ya Vijana (2007) umri wa Kijana ni miaka 15 - 35 Kutokana na Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, idadi ya Vijana Nchini ni 16,195,370 (Bara na Zanzibar). Idadi hii ni sawa na Asilimia 35.1 ya Watanzania wote. Vijana walioajiriwa katika Sekta ya Umma ni 188,087, waliajiriwa katika Sekta Binafsi ni 1,028,634 na waliojiajiri wenyewe ni 1,102,742. Kwa mantiki hii Vijana waliobaki wapatao 13,200,000 wengi wao wanajishughulisha na Kilimo. Hata hivyo, kwa vile Vijana hao waliopo kwenye kilimo hawafanyi kilimo cha kisasa na chenye tija, wengi wao hawafanyi Kilimo cha kibiashara hivyo wako chini ya kiwango cha ajira kamili kinachofahamika Kimataifa.


Mheshimiwa Spika,
    Kwa kutambua umuhimu wa Vijana katika Nchi yetu, ndiyo maana Mfuko wa Maendeleo ya Vijana umeboreshwa kwa kuongezewa fedha Bilioni Tatu (3) ili kukuza uwezo wa kutoa Mikopo yenye masharti nafuu kwa Vijana na kuwajengea uwezo wa kuanzisha shughuli za uzalishaji mali au kuziimarisha zile wanazoziendesha. Kiasi hicho cha fedha ni nyongeza kwa Bajeti iliyotengwa kwa mwaka huu wa fedha. Fedha hizi zitatumika kwa Vikundi vya Vijana waliomaliza Vyuo na Vijana wengine watakaokuwa tayari kuanzisha miradi mizuri inayokopesheka. Fedha hizi zitaendelea kutolewa kupitia SACCOS za Vijana za Wilaya. Mwongozo mpya wa Matumizi ya Mfuko wa Maendeleo ya Vijana umesambazwa kwa Halmashauri zote 151 Tanzania Bara na kwamba Miradi ya Vijana sasa itahakikiwa kwenye ngazi ya Halmashauri, Mkoa na Wizara kabla ya mkopo kutolewa. Natoa wito kwa Vijana hasa wakiwa katika Ushirika kuchangamkia fursa hii ili waweze kujiajiri. Nawasihi wafike katika Mamlaka husika kupata maelezo na kuwasilisha michanganuo ya kazi zao ili waweze kusaidiwa.

VIII MIGOGORO YA ARDHI

    Mgogoro wa Ardhi kwenye eneo la Pori Tengefu Loliondo

Mheshimiwa Spika,
    Tarehe 19 Machi 2013, Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii, ilitoa Taarifa kwa Umma kuhusu kusudio la kupunguza ukubwa wa eneo la Pori Tengefu la Loliondo, kutoka Kilomita za Mraba 4,000 hadi 1,500. Lengo la Serikali lilikuwa ni kulinda mazalia ya Wanyamapori, Mapito na Vyanzo vya Maji kwa ajili ya ustawi wa Hifadhi katika eneo la Kilometa za Mraba 1,500 lililopendekezwa. Vilevile, ni kuhakikisha kuwa usimamizi endelevu wa Hifadhi za Serengeti, Ngorongoro na Pori Tengefu la Loliondo kwa ajili ya Kizazi cha sasa na kijacho.

Mheshimiwa Spika,

    Kutokana na taarifa hiyo, Wananchi wanaoishi katika Vijiji vilivyomo ndani ya eneo la Pori Tengefu Loliondo na ambao wamekuwa wakiishi katika eneo hilo kwa muda mrefu, hususan katika eneo la Kilomita za Mraba 1,500 ambazo Serikali iliamua ziendelee kubaki na hadhi ya Pori Tengefu, wamepata hofu ya kuhamishwa na hivyo walituma Wawakilishi mbalimbali kufika Dodoma na Arusha kuniona ili kupata ufafanuzi wa Tamko hilo.


Mheshimiwa Spika,
    Kimsingi, Sheria ya Uhifadhi wa aina mbalimbali za Wanyama (Fauna Conservation Ordinance) Sura ya 302 ya Mwaka 1951 ndiyo iliyoanzisha Mapori ya Akiba na Mapori Tengefu Nchini. Sheria hii ilianzisha Mapori Tengefu 49 Nchini kwa Tangazo la Serikali.


    Mwaka 1974, Sheria ya Hifadhi ya Wanyamapori ilianzishwa na kufuta Sheria ya awali ya Fauna Conservation Sura ya 302. Chini ya Sheria hizo mbili, masuala ya malisho na makazi hayakukatazwa katika maeneo ya Mapori Tengefu ikiwemo Pori Tengefu la Loliondo. Sheria hiyo ya Hifadhi ya Wanyamapori iliendelea kutumika hadi mwaka 2009 ambapo Sheria mpya ya Uhifadhi wa Wanyamapori (The Wildlife Conservation Act) Namba 5 ya Mwaka 2009 ilipoanzishwa na kufuta ile ya awali ya mwaka 1974.


    Chini ya Sheria hii mpya ya Mwaka 2009, masuala ya malisho na makazi katika maeneo ya Mapori Tengefu yamezuiliwa, mpaka kwa kibali kutoka kwa Mkurugenzi wa Wanyamapori. Kutokana na masharti hayo ya Kisheria, Vijiji ambavyo awali vilianzishwa katika maeneo ya Mapori Tengefu vimejikuta katika hali ya kuvunja Sheria hiyo ya Mwaka 2009.


Mheshimiwa Spika,
    Ndani ya eneo la Loliondo ambalo Serikali inapendekeza liendelee kubaki na hadhi ya Pori Tengefu la Kilomita za Mraba 1,500 kutokana na umuhimu wake kiuhifadhi, kuna Vijiji sita (6) vilivyosajiliwa na Serikali. Kutokana na Tamko lililotolewa, ni dhahiri kuwa Wananchi waliopo katika Vijiji hivyo watatakiwa kuhama katika maeneo hayo. Hata hivyo, changamoto iliyopo ni kwamba, Vijiji vyote hivi vimeanzishwa na Serikali na kupewa hadhi ya kuwa Vijiji, ingawa kwa mujibu wa Sheria ilibidi ardhi hiyo iondolewe kwenye hadhi ya Pori Tengefu kwanza kabla ya kuanzisha Vijiji hivyo. Vijiji hivi vimekuwa ni makazi ya Watu na vina miundombinu ya kudumu ya kutoa huduma kwa Jamii.


Mheshimiwa Spika,
    Wananchi waishio katika Vijiji ndani ya Pori Tengefu la Loliondo wana hofu ya kukosa eneo la malisho ya mifugo na eneo la kuishi baada ya kuishi hapo kwa miaka mingi kabla na tangu kuanzishwa rasmi kwa Vijiji hivyo. Hofu ya kuharibiwa kwa hifadhi hiyo ipo pia kwa upande wa Serikali, na ndio maana Wizara ya Maliasili na Utalii imekuja na Mpango huu wa kuondoa eneo la Kilomita za Mraba 2,500 ili liwe nje ya Hifadhi na kusimamiwa na Wananchi wenyewe kwa kuzingatia Mpango endelevu wa Matumizi Bora ya Ardhi.

Mheshimiwa Spika,
    Napenda kuchukua nafasi hii kulijulisha Bunge lako Tukufu na Wananchi wa Loliondo kuwa, pamoja na kwamba Tamko la Serikali lilitolewa kwa nia njema ya kuendeleza uhifadhi endelevu, kumejitokeza malalamiko mengi dhidi ya Tamko hilo. Serikali imepokea malalamiko hayo kutoka kwa Wadau na Makundi mbalimbali ya Wananchi kutoka Loliondo wakiwemo Viongozi wa Wilaya, Halmashauri, Wazee wa Kimila, Akina Mama na Vijana.


Mheshimiwa Spika,
    Uko ukweli kwamba, suala hili limeleta changamoto kubwa ambayo inahitaji tafakuri kubwa. Kwa kuzingatia changamoto hizo Serikali kwa sasa inafanya mambo yafuatayo:


    Kupitia upya Tamko lililotolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuzingatia Sheria zilizopo za Wanyamapori pamoja na zile za Ardhi;


    Kubaini miundombinu iliyopo katika eneo linalopendekezwa kubaki na hadhi ya Pori Tengefu;


    Kuangalia changamoto zilizojitokeza kwa pande zote mbili (Wananchi na Serikali) kuhusu eneo hilo la Kilomita za Mraba 1,500 kuendelea kubaki na hadhi ya Pori Tengefu; na


    Kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa kuendeleza uhifadhi katika Pori la Loliondo kwa kuwashirikisha Wananchi.


Mheshimiwa Spika,
    Wakati Serikali ikiendelea na hatua hizo, ninawaomba Wananchi waliomo ndani ya Pori hilo la eneo la Loliondo waendelee kuvuta subira wakati Serikali ikiendelea kutafuta suluhu ya kudumu ya suala hili. Aidha, nimekwisha toa maelekezo ya awali kuhusu namna ya kushughulikia ufafanunuzi wa suala hili kwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha ili kutoa ufafanuzi stahiki kwa Wananchi wanaoishi ndani ya Pori Tengefu Loliondo. Nawaomba Wananchi wa Loliondo waelewe nia hii njema ya Serikali ya kuwaondolea wasiwasi uliopo.


    Mwisho niwaombe Viongozi wa kisiasa wakiwemo, Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro, Waheshimiwa Madiwani wa Kata za Loliondo na Sale na Viongozi wa Serikali wa Wilaya ya Ngorongoro na Mkoa wa Arusha watusaidie kusimamia suala hili ili lishughulikiwe kwa manufaa ya Taifa na Wananchi wa eneo hilo kwa ujumla. Aidha, tuendelee kuhifadhi mazingira ya eneo hili ambalo limepata sifa kubwa Duniani kutokana na kuwa na vyanzo vya maji na mapito ya Wanyama Pori wahamao katika Mfumo wa Ekolojia ya Serengeti. Kwa sasa Dunia inatambua eneo hili kama “Urithi wa Dunia” (World Heritage) na mojawapo ya Maajabu Saba ya Asili katika Bara la Afrika.






IX MATOKEO YA UCHAGUZI

    Uchaguzi Mdogo

Mheshimiwa Spika,
    Tume ya Taifa ya Uchaguzi imefanikiwa kusimamia Uchaguzi Mdogo wa Ubunge Jimbo la Chambani, Pemba na Chaguzi Ndogo za Madiwani katika Kata 26 za Halmashauri mbalimbali Nchini. Vyama vilivyoshiriki katika Chaguzi hizo Ndogo ni CCM, CHADEMA, ADC na CUF. Matokeo yanaonesha kwamba, Wagombea wa Chama cha Mapinduzi wamefanikiwa kushinda katika Kata 16 na CHADEMA walipata Kata sita (6) katika Kata 22 ambako uchaguzi ulifanyika. Chama cha ADC na Chama cha CUF vyote havikupata kura. Kwa upande wa Ubunge katika Jimbo la Chambani, wote tumeshuhudia kuapishwa kwa Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein kuwa Mbunge Mpya wa Jimbo hilo kwa tiketi ya Chama cha CUF. Nitumie nafasi hii tena kupongeza Vyama vyote vilivyoshiriki na hasa vile vilivyopata ushindi.


    Maandalizi ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Ngazi ya Vijiji, Mitaa na Vitongoji Mwezi Oktoba 2014

Mheshimiwa Spika,
    Tarehe 10 Aprili, 2013 nilitoa tarifa hapa Bungeni kwamba, uchaguzi wa Viongozi katika ngazi za Vijiji, Mitaa na Vitongoji unatarajiwa kufanyika mwezi Oktoba, 2014. Ofisi yangu inaendelea kuratibu maandalizi ya awali ya Uchaguzi huo ili kuwezesha uchaguzi huo kufanyika Kidemokrasia zaidi, kwa uhuru na haki. Kwa mujibu wa Kifungu cha 56 (3) cha Sheria za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura 287 na vifungu vya 4 na 70(c) vya Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka ya Miji) Sura 288 matoleo ya 2002, jukumu la msingi la Ofisi yangu ni kuandaa Kanuni za uendeshaji Uchaguzi huo ili kuhakikisha demokrasia inakuwepo.


Mheshimiwa Spika,
    Maandalizi yanayoendelea hivi sasa ni pamoja na kupokea michango na maoni ya awali kutoka kwa Wadau mbalimbali hususan Vyama vya Siasa kuhusu namna ya kuboresha Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Kanuni hizo zinatarajiwa kutangazwa katika Gazeti la Serikali mwaka 2014. Maoni yanayokusanywa yatachambuliwa na kisha kujadiliwa katika Vikao vya Wadau vitakavyoitishwa. Aidha, mapendekezo ya Kanuni hizo yatatangazwa kwenye magazeti ili Wananchi waweze kuzisoma na kutoa maoni yao. Wito wangu ni kuwataka Viongozi wa Vyama vya Siasa, Vyama Visivyo vya Kiserikali na Wananchi kwa ujumla kujitokeza kwa wingi katika kutoa maoni ili hatimaye kuwa na Kanuni za Uchaguzi zitakazosaidia kuwa na Uchaguzi Huru na wa haki.


Mheshimiwa Spika,
    Maandalizi mengine yanayofanywa na Ofisi yangu ni kuhakiki Vijiji na kuvisajili. Kabla ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ngazi za Vijiji, Vitongoji na Mitaa wa mwaka 2009 kufanyika, Vijiji na Mitaa mipya ilianzishwa. Maeneo mapya ya Vijiji yalihakikiwa na kutolewa hati za usajili kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa. Kwa sasa, Ofisi yangu imekuwa ikipokea maombi mbalimbali ya kuanzisha Vijiji vipya. Tayari nimetoa maelekezo kwamba mwisho wa kupokea maombi kwa ajili ya maeneo mapya ya Vijiji ni tarehe 31 Desemba, 2013. Natoa wito kwa Halmashauri zote zinazotaka kuomba Vijiji vipya kuzingatia Sheria, na tarehe ya mwisho ya kupokea maombi hayo. Aidha, nawaomba kuwashirikisha Wananchi na Wadau mbalimbali kupitia Vikao vya Ushauri vya Wilaya (DCC) na Mkoa (RCC) ili tuweze kufanikisha maandalizi ya Chaguzi hizo.

X HIFADHI YA MAZINGIRA

    Wiki ya Mazingira Duniani

Mheshimiwa Spika,
    Tarehe 1 - 6 Juni, 2013 Nchi yetu iliungana na Nchi nyingine Duniani kuadhimisha wiki ya mazingira Duniani. Maadhimisho hayo yalifanyika Kitaifa katika Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa. Ujumbe wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka huu ni: “Fikiri, Kula: Hifadhi Mazingira” au kwa Lugha ya Kiingereza “Think - Eat - Save”. Ujumbe huu unamaanisha kwamba shughuli zote zinazofanyika za uzalishaji mali na utoaji wa huduma zizingatie kuhifadhi Mazingira badala ya kuwa chanzo cha uharibifu wake.


Mheshimiwa Spika,
    Juhudi za kukabiliana na uharibifu wa mazingira zinakabiliwa na Changamoto mbalimbali. Baadhi ya Changamoto hizo ni: Ukataji miti kwa ajili ya kuni, mkaa, mbao/ujenzi pamoja na uchomaji moto ovyo. Utafiti unaonesha kuwa takriban Hekta 400,000 zinapotea kila mwaka kutokana na ukataji miti.


    Changamoto nyingine inayotukabili ni kuwa na Idadi kubwa ya Mifugo ambayo haiwiani na uwezo wa eneo la malisho hasa katika Mikoa ya Shinyanga, Rukwa Mwanza, Morogoro n.k. Hali hiyo inasababisha Wafugaji kuvamia maeneo ya vyanzo vya maji pamoja na maeneo ya hifadhi, na kuleta mmomonyoko wa udongo na hivyo kusababisha uharibifu mkubwa wa mazingira. Uchafuzi wa Mazingira ya Makazi kumekuwepo na mazingira ya uchafu katika makazi ya Watu na hasa maeneo ya Miji kutokana na kukosekana kwa namna nzuri ya uondoshaji wa taka ngumu na laini.

Mheshimiwa Spika,
    Serikali kwa kushirikana na Wananchi imeendelea na juhudi za kupambana na uharibifu wa mazingira kwa kuchukua hatua mbalimbali. Hatua hizo ni pamoja na kuhimiza na kusimamia zoezi la upandaji wa miti kila mwaka; kupanua mashamba ya miti ya Serikali kila mwaka, kusimamia Sheria zinazozuia ukataji miti ovyo, kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wanaochoma moto ovyo, kuweka Vituo vya Maliwato kwenye Vituo vya Mabasi na kwenye Barabara Kuu, kutenga maeneo ya kukusanyia taka ngumu na Vimiminika Mijini, kuweka mazingira ya Miji kuwa safi na kuhimiza uchimbaji na matumizi ya vyoo n.k. Napenda kuchukua fursa hii kupongeza Mikoa na Halmashauri mbalimbali ambazo wamekuwa wakifanya juhudi kubwa kuhimiza na kusimamia usafi katika maeneo yao. Nimekuwa nikishuhudia ubunifu mkubwa katika suala hili la usafi wa Miji.


    Nawaomba Viongozi kwa kushirikiana na Wananchi kusimamia suala la kutunza Mazingira katika maeneo yao. Tuzidi kuimarisha usafi wa mazingira, tusimamie zoezi la upandaji miti kuanzia kwenye nyumba tunazoishi, Barabara, mashamba, Viwanja n.k. Tutunze vyanzo vya maji, tuzuie uchomaji moto ovyo, tuwaelimishe Wafugaji kupunguza idadi ya mifugo ili iendane na maeneo yao ya kulishia na tuchukue hatua zozote zinazoboresha mazingira ili tuwe na maendeleo endelevu.


    Mradi wa Uendelezaji na Kuboresha Miji Nchini (Tanzania Strategic Cities Program (TSCP)

Mheshimiwa Spika,
    Tarehe 18 Juni, 2013 nilipata fursa ya kuzindua mradi wa kuboresha Miji Nchini katika hafla iliyofanyika Mjini Moshi. Mradi huu unatekelezwa katika Miji 18 ya Tanzania Bara ikiwemo Miji ya Morogoro, Tabora, Moshi, Sumbawanga, Shinyanga, Songea, Singida, Musoma, Iringa, Njombe, Lindi, Bukoba, Kibaha, Babati, Geita, Korogwe, Mpanda na Bariadi. Mradi huo umetanguliwa na mradi mwingine wa Kuboresha Miji Tanzania (Tanzania Strategic Cities Programme) ulioanza mwaka 2010. Katika mradi huo kuna Halmashauri saba (7) za awali ambazo zinatekeleza Mradi huo. Halmashauri hizo ni Arusha, Mwanza, Kigoma, Mbeya, Dodoma, Tanga na Mtwara Mikindani pamoja na Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA). Kwa hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Mradi huu umebadilisha sura na Mandhari ya Miji hiyo na kuifanya ivutie kwa uwekezaji na kurahisisha utoaji wa huduma nyingine za Kijamii.


Mheshimiwa Spika,

    Napenda kutumia fursa hii kuzipongeza Halmashauri hizo saba (7) pamoja na CDA kwa kufanya vizuri katika kutekeleza mradi huo na hivyo kuiwezesha Benki ya Dunia kukubali kugharamia awamu nyingine ya Programu ya kuboresha Miji Nchini kwenye Halmashauri za Miji mingine 18, ambayo nimeizindua hivi karibuni pale Moshi. Benki ya Dunia pia imekubali kugharamia Mradi wa Kuboresha Jiji la Dar es Salaam (Dar es Salaam Metropolitan Development Project-DMDC) ambao utaanza kutekelezwa wakati wowote kuanzia sasa. Miradi hii mikubwa ya kuboresha Miji niliyoitaja itagharimu Dola za Kimarekani Milioni 455 kutoka Benki ya Dunia. Fedha hii inategemewa kutumika katika ujenzi wa jumla wa Miradi Midogo Midogo zaidi ya Kumi (10) itakayojumlisha barabara, mifereji, Mifumo ya Uzoaji Taka, Taa za Barabara, maeneo ya Kuegesha Magari, Masoko, Mipango Miji, Ukusanyaji Mapato ya Halmashauri, Uwajibika na Makazi holela. Ujenzi wa barabara katika Jiji la Dar es Salaam unajumuisha pia Barabara za Juu (Fly Overs) pale Ubungo. Sote tunakubaliana kwamba miradi hii ikikamilika, Miji hiyo itakuwa na Mandhari nzuri kwa Wananchi na kuwa kivutio kikubwa kwa Wawekezaji kutokana na kuboreshwa kwa madhari za kuweka mazingira ya usafi.

Mheshimiwa Spika,
    Nitumie nafasi hii kuishukuru Benki ya Dunia kwa kukubali kugharamia Miradi hii. Ni dhahiri tunafanya vizuri na ni wajibu wa kila mmoja wetu kusimamia Miradi hii itekelezwe vizuri kwa ubora unaostahili. Ili kuhakikisha kwamba mafanikio yanapatikana katika miradi hii, niwasisitize Wakurugenzi na Wakuu wa Idara wa Halmashauri kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi hiyo. Vilevile, Wakurugenzi wa Halmashauri na Wakandarasi wawajibike ipasavyo ili Mpango huu utekelezwe kwa wakati. Aidha, Halmashauri zote Nchini zijenge tabia ya kutenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya kutunza Barabara zinazojengwa ili ziweze kudumu kwa muda mrefu na kuleta manufaa yaliyokusudiwa.


Mheshimiwa Spika,
    Pamoja na mafanikio yanayoonekana wazi katika miradi hii, changamoto nyingine kubwa tuliyonayo kwenye Mpango huu, wa kuboresha Miji ni kuona Sehemu kubwa ya Miji yetu inaendelea kukua kiholela bila kuwepo kwa mipango makini ya kuongoza ukuaji wa Miji hiyo. Napenda kutumia fursa hii kuziagiza Halmashauri zote Nchini zisimamie kikamilifu upangaji Miji ili kuzuia ongezeko la ujenzi holela na uharibifu Miji, hali inayotugharimu fedha nyingi katika kuipanga upya. Aidha, Wananchi waelimishwe kuhusu umuhimu wa kuzingatia Sheria za uendelezaji Miji kwa mujibu wa Sheria za Mipango Miji. Halmashauri zisimamie kikamilifu Sheria zinazokataza ujenzi holela unaoharibu mandhari ya Miji yetu.


XI MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI

Mheshimiwa Spika,
    Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ni Wadau muhimu wa maendeleo ya Jamii na Taifa letu. Mashirika haya yamekuwa na mchango mkubwa hususan kwenye nyanja za afya ikiwemo maradhi yanayotokana na UKIMWI, huduma za Maji, Elimu, Ushiriki wa Jamii, Mazingira, Utawala Bora, Kilimo, Jinsia na Huduma kwa Yatima na Watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi. Aidha, Mashirika haya yamekuwa yakitoa ajira na fursa za kupata uzoefu wa kujitolea kwa Watanzania. kwa Mfano katika mwaka 2012 zaidi ya watu 60,700 waliajiriwa au kujitolea kwenye Mashirika haya.


    Kwa kuzingatia umuhimu huo, Serikali imekuwa ikijenga mazingira wezeshi ili yaendelee kukua na kutoa mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya Nchi yetu. Mazingira hayo ni pamoja kuyawezesha kutambulika kisheria kupitia usajili; pili, kuyalinda tatu, kuwezesha ubia baina ya Serikali na Mashirika hayo na nne, kuyawezesha kujitawala kupitia Baraza la Taifa la Mashirika yasiyo ya Kiserikali.


Mheshimiwa Spika,
    Kwa sasa, idadi ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ni kubwa na imekuwa ikiongezeka kila mwaka huku mazingira ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali kufanya kazi hapa Nchini yameendelea kuboreka. Kwa mwaka 2012/2013 pekee Jumla ya Mashirika 443 yalisajiliwa na kufanya idadi ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali hapa Nchini kufikia 5,734. Katika mazingira haya ikiwa kila Shirika lisilo la Kiserikali litatekeleza ipasavyo malengo yake iliyojiwekea kwa mujibu wa Sheria, ni matumaini ya Serikali kuwa hatua kubwa za maendeleo zitapatikana kwa haraka zaidi chini ya Mashirika hayo.


    Napenda kutumia fursa hii kuyataka Mashirika yote kufanya shughuli zao kwa uwazi zaidi, kushirikiana na Serikali katika kuiletea Jamii maendeleo. Pia Mashirika hayo yanakumbushwa kuwasilisha taarifa zao za mwaka Serikalini kwa mujibu wa Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Na. 2002 kama ilivyorekebishwa mwaka 2005. Vilevile, nawasihi kujiepusha na kujiiingiza katika masuala ya siasa na uchochezi kwa raia. Kutofanya hivyo, kutayawezesha Mashirika haya kuaminika zaidi katika Jamii na kuiwezesha Serikali kuainisha mchango wao katika maendeleo ya Jamii yetu na Taifa kwa ujumla.

Kinachotakiwa ni kila Shirika Lisilo la Kiserikali litimize wajibu wake kwa Wananchi ambao ndiyo walengwa bila ya kujinufaisha yenyewe.

XII VYAMA VYA SIASA

Mheshimiwa Spika,
    Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa Na. 5 ya 1992 na Kanuni za Maadili ya Vyama vya Siasa inaelekeza Wadau wote wa Demokrasia kutoa maoni yao kuhusiana na marekebisho hayo kwa lengo la kukabiliana na changamoto za Kisiasa na Ki-utendaji zilizopo na zitakazojitokeza katika masuala ya Siasa Nchini.

Mheshimiwa Spika,
    Katika kuhakikisha kuwa amani inadumishwa Nchini. Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa imewakutanisha Vyama vya Siasa na Jeshi la Polisi Nchini na kuzungumza juu ya dhima ya Jeshi la Polisi na Vyama vya Siasa katika kukua kwa Demokrasia na amani Nchini. Katika mazungumzo hayo Viongozi wa Vyama vya Siasa wamelaani tabia ya baadhi ya Vyama vya Siasa kujihusisha katika kuvunja amani Nchini.


Mheshimiwa Spika,
    Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na matukio mengi ya vurugu yanayohusishwa na Vyama vya Siasa. Sheria ya Vyama vya Siasa na Kanuni zake zinakataza Vyama kujihusisha na vurugu, kuigawa Nchi kwa udini, ukabila, rangi au aina yoyote ya ubaguzi ambayo itasababisha kutoweka kwa amani ya Nchi. Vilevile, Sheria hiyo imeweka bayana kuwa Chama kitakachobainika kufanya hayo, kitafutwa kwa mujibu wa Sheria.


Mheshimiwa Spika,
    Napenda kuwakumbusha Viongozi wenzangu hasa wa kisiasa kwamba, Demokrasia si kufuta Vyama wala kuvuruga Nchi na kuwagawa Watanzania, bali ni kuwa na Sera nzuri zinazowaunganisha Watanzania na kudumisha amani ya Nchi yetu. Kila Mtu pale alipo ana wajibu wa kulinda amani tuliyonayo na kuhakikisha kuwa Sheria za Nchi zinazingatiwa kwa lengo la kulinda haki za Wananchi wote. Nawaomba sana Wanasiasa na Viongozi wezangu tusijaribu kuweka rehani Nchi yetu kwa kuhamasisha kwa njia moja au nyingine Wananchi wetu kuvuruga amani ya Nchi yetu. Tuwafundishe Wananchi wetu kupendana kuvumiliana na kusaidiana.


XIII AMANI NA UTULIVU NCHINI

Mheshimiwa Spika,
    Nimeongelea kuhusu Vyama vya Siasa kutokana na hali halisi ya matukio yanayojitokeza Nchini. Hivi karibuni pamekuwepo na matukio ya vurugu, fujo na uvunjifu wa amani katika maeneo mbalimbali ya Nchi yetu. Katika kipindi cha mwaka mmoja tu uliopita vurugu zimetokea Arusha, Mwanza, Mbeya, Mtwara, Morogoro, Singida na Iringa. Hofu ya migogoro ya kidini imetokea Zanzibar, Dar es Salaam, Arusha, Mwanza na Geita. Baadhi ya matukio haya yamesababisha Vifo na majeruhi ikiwemo, kujeruhiwa Askari na Wananchi, uharibifu wa miundombinu, uharibifu wa mazingira na mali za Serikali na Watu binafsi.


Mheshimiwa Spika,
    Matukio mfululizo ya fujo, vurugu pamoja na tukio la kulipua mabomu Kanisani na hivi karibuni katika Mkutano wa hadhara huko katika Kata ya Soweto kule Arusha na katika Mkutano wa Kampeni ya Chama cha Chadema katika Uwanja wa Soweto Arusha yamesababisha hofu kubwa kwa Wananchi na hisia ya uwepo wa tishio la kuendelea kwa vitendo vinavyoashiria ugaidi katika Nchi yetu. Matukio ya aina hii yakiachwa yaendelee, uchumi wa Nchi yetu utadorora kutokana na ushiriki hafifu kwenye shughuli za maendeleo.


Mheshimiwa Spika,
    Vilevile, ziko dalili ya kuwepo kwa vikundi vya Watu wachache wasioitakia mema Nchi yetu. Vikundi hivi vinataka kupandikiza chuki za kisiasa na kidini miongoni mwa Watanzania na kuleta mapigano na mauaji miongoni mwao. Sina shaka kuwa fujo, vurugu, vitendo vya uvunjifu wa amani ikiwemo mashambulio ya Mabomu Arusha na vurugu za Mtwara ni sehemu ya mikakati hiyo mibovu. Nataka niwahakikishie Watanzania kuwa Serikali haitavumilia hata kidogo kuendelea kupandwa mbegu za chuki na za kidini na kisiasa miongoni mwa Watanzania. Serikali itachukua hatua kali bila huruma kuzimaliza njama hizi mbaya dhidi ya Taifa letu. Vilevile, hatua kali zitachukuliwa kwa Mtu yeyote atakayebainika kuhusika bila kujali hadhi na nafasi yake katika Jamii.


Mheshimiwa Spika,
    Nitumie nafasi hii tena kuwasihi Viongozi wa Serikali, Kisiasa, Kidini na Wananchi wote kwa ujumla, kila mmoja kwa nafasi yake kuwajibika ili kuhakikisha kuwa Nchi yetu inaendelea kuwa Kisiwa cha Amani na Utulivu. Watanzania wote tushirikiane na Vyombo vya Dola katika kubaini wahalifu hao. Tuendelee na mshikamano wa kukataa vitendo vya uvunjifu wa Amani katika Nchi yetu. Kila mwenye taarifa za kuwezesha kukamatwa kwa Watu wanaohatarisha amani ya Nchi yetu atoe taarifa kwa Jeshi letu la Polisi na taarifa hizo zitafanyiwa kazi kwa umakini mkubwa na kwa maslahi ya Taifa letu.

XIV HITIMISHO

Mheshimiwa Spika,
    Changamoto kubwa iliyoko mbele yetu baada ya kuwepo hapa Bungeni kwa takriban Siku 78 ni kusimamia utekelezaji wa Bajeti ya Serikali tuliyoipitisha. Sisi kama Wabunge tuondoke hapa kwa lengo moja la kushirikiana na Wananchi kusukuma maendeleo na Bajeti tuliyoipitisha ikiwa ndiyo kichocheo kikuu. Nchi yetu bado ni nzuri na ina amani. Wananchi wetu bado ni Watu wazuri, wastaarabu, wavumilivu na wapenda amani. Wananchi wanaelewa na ni watiifu. Twendeni tukasisitize umuhimu wa kuishi kwa amani, upendo na mshikamano. Tukiwasimamia vizuri na kuwaongoza katika matumizi ya rasilimali zilizopo, Nchi yetu itasonga mbele kimaendeleo na maisha bora kwa Wananchi wetu yatapatikana.

XV SHUKRANI

Mheshimiwa Spika,
    Napenda nimalizie kwa kuwashukuru wote waliosaidia kufanikisha Mkutano huu. Nikushukuru kwa namna ya pekee wewe mwenyewe Mheshimiwa Spika na Naibu Spika kwa kutuongoza vizuri kulingana na Kanuni za Bunge. Aidha, niwashukuru Wenyeviti wa Bunge, Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama, Mbunge wa Peramiho, Mheshimiwa Mussa Zungu Azzan, Mbunge wa Ilala na Mheshimiwa Muhammed Seif Khatib Mbunge wa Uzini kwa kuongoza vizuri baadhi ya Vikao vya Bunge wakati wa Mkutano huu. Ninawashukuru tena Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yenu ya dhati na yenye mantiki kwa ajili ya Maendeleo ya Nchi yetu. Niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri, Naibu Mawaziri, Watumishi na Wataalam wote wa Serikali waliosaidia kujibu Maswali na Hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge zilizojitokeza hapa wakati wa Mkutano huu. Vilevile, nawashukuru Waandishi wa Vyombo vya Habari kwa kuwapatia Wananchi habari kuhusu Majadiliano yaliyokuwa yanaendelea hapa Bungeni. Wote kwa ujumla wenu nawashukuru sana.


    Kipekee napenda kuwashukuru Madereva wote ambao wamekuwa makini katika kazi ya kuwaendesha Viongozi wote wakiwemo Waheshimiwa Wabunge na Wataalam kutoka sehemu mbalimbali Nchini na kuwawezesha kufika hapa Dodoma kuhudhuria Mkutano huu wa Kumi na Moja. Vilevile, nawashukuru Wananchi wa Mkoa wa Dodoma, Wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Dkt. Rehema Nchimbi kwa ukarimu wao kwa muda wote tuliokaa hapa Dodoma. Navishukuru pia Vyombo vya Ulinzi na Usalama ambavyo vimehakikisha muda wote tumekaa kwa Amani na kwa Utulivu mkubwa. Mwisho namshukuru Katibu wa Bunge Dkt. Thomas Kashilillah na Watumishi wote wa Ofisi ya Bunge kwa huduma nzuri zilizowezesha kukamilisha shughuli zilizopangwa katika Mkutano huu bila matatizo.


Mheshimiwa Spika,
    Nitumie fursa hii kuwaombea safari njema mnaporudi katika maeneo yenu ya kazi. Lakini pia niwaombee kheri na Baraka tele Waislamu wote ambao katika siku chache zijazo watashiriki katika Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Kila atakayeamua kufanya Ibada hiyo aifanye kikamilifu na kama Kitabu cha Quran Tukufu kinavyoelekeza.


Mheshimiwa Spika,
    Baada ya maelezo hayo, napenda kutoa hoja kwamba, Bunge lako Tukufu sasa liahirishwe hadi tarehe 27 Agosti, 2013 siku ya Jumanne, Saa 3:00 Asubuhi litakapokutana katika Mkutano wa 12 kwenye Ukumbi huu hapa Dodoma.


    Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.









All the contents on this site are copyrighted ©.