2013-01-18 10:29:26

Kongamano la Kimataifa kufanyika Benin, kama kumbu kumbu ya Mwaka mmoja tangu Africae Munus ilipochapishwa


Baraza la Kipapa la Utamaduni kwa kushirikiana na Baraza la Maaskofu Katoliki Benin pamoja na Taasisi ya Elimu Katoliki Ufaransa, kwa pamoja wameandaa Kongamano la Kimataifa, kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka mmoja, tangu Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alipozindua Matunda ya Maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu Katoliki Afrika, huko nchini Benin, kunako Mwezi Novemba 2011. Viongozi mbali mbali wa Kanisa kutoka Benin na Vatican wanatarajiwa kushiriki kuanzia tarehe 21 hadi tarehe 25 Januari 2013.

Kongamano hili la Kimataifa linaoongozwa na kauli mbiu "Haki, utamaduni na Upendo". Wajumbe watapata fursa ya kusikiliza Falsafa inayofumbatwa katika Waraka wa Kichungaji wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Dhamana ya Afrika. Watajadili kwa kina na mapana kuhusu: haki na kipindi cha mpito kuelekea demokrasia; haki na utamaduni; vita vya wenyewe kwa wenyewe na mauaji ya kimbari; haki na upendo; mchango wa dini mbali mbali katika kudumisha fadhila hii.

Hapo tarehe 25 Januari 2013, wajumbe watahitimisha kwa kutoa muhtasari ya yale yatakayojiri kwenye kongamano ili yaweze kufanyiwa kazi katika mchakato wa kudumisha haki, amani na upatanisho.







All the contents on this site are copyrighted ©.